Hamia kwenye habari

Kwa Nini Mashahidi wa Yehova Hawasherehekei Ista?

Kwa Nini Mashahidi wa Yehova Hawasherehekei Ista?

Maoni yasiyofaa

Uwongo: Mashahidi wa Yehova hawasherehekei Ista kwa sababu si Wakristo.

 Ukweli: Tunaamini Yesu Kristo ni Mwokozi wetu, na tunajitahidi ‘kufuata hatua zake kwa ukaribu.’—1 Petro 2:21; Luka 2:11.

 Uwongo: Nyinyi hamwamini kwamba Yesu alifufuliwa kutoka kwa wafu.

 Kweli: Tunaamini ufufuo wa Yesu; tunatambua kwamba huo ndio msingi wa imani ya Kikristo na tunahubiri kuhusu jambo hilo.—1 Wakorintho 15:3, 4, 12-15.

 Uwongo: Hamjali kwamba watoto wenu hawafurahii sherehe za Ista.

 Ukweli: Tunawapenda watoto wetu, tunatumia muda mwingi kuwazoeza na kuwasaidia wawe na furaha.—Tito 2:4.

Kwa nini Mashahidi wa Yehova hawasherehekei Ista?

  •   Sherehe za sikukuu ya Ista hazitegemei Biblia.

  •   Yesu aliagiza kwamba tukumbuke kifo chake, bali si kufufuliwa kwake. Tunaadhimisha Ukumbusho huo kila mwaka kwenye tarehe ambayo alikufa, kulingana na kalenda ya miezi ya Biblia.—Luka 22:19, 20.

  •   Tunaamini kwamba desturi za Ista, zilizotokana na ibada ya kale ya uzazi, zinafanya Ista isikubalike machoni pa Mungu. Mungu anataka ‘tujitoe kikamili’ kwake, na anachukia ibada inayohusisha mazoea yasiyompendeza.—Kutoka 20:5; 1 Wafalme 18:21.

 Tunaamini kwamba uamuzi wetu wa kutosherehekea Ista unategemea kabisa Biblia, ambayo inatuhimiza tuwe na “hekima inayotumika na uwezo wa kufikiri” badala ya kufuata tamaduni za wanadamu. (Methali 3:21; Mathayo 15:3) Ingawa tunazungumza kuhusu Ista pamoja na wengine tunapopata nafasi, pia tunaheshimu haki ya kila mtu ya kuamua atakachofanya.—1 Petro 3:15.