Hamia kwenye habari

BIBLIA INABADILI MAISHA

“Sasa Sioni Aibu Tena”

“Sasa Sioni Aibu Tena”
  • Alizaliwa: 1963

  • Nchi: Mexico

  • Historia: Mtoto wa mitaani; hisia za kujidharau

MAISHA YANGU YA ZAMANI

 Nilizaliwa Ciudad Obregón kaskazini mwa Mexico, nikiwa mtoto wa tano katika familia ya watoto tisa. Tuliishi pembeni ya mji, ambako baba alikuwa na shamba dogo. Lilikuwa eneo zuri la kuishi, na familia yetu ilikuwa na umoja na furaha. Lakini kwa kusikitisha, nilipokuwa na umri wa miaka mitano tu, kimbunga kiliharibu shamba letu na tukalazimika kuhamia mji mwingine.

 Baba alianza kupata pesa nyingi. Lakini wakati huohuo, akawa mlevi. Hilo liliathiri ndoa yao na kutuathiri sisi watoto. Tulianza kuvuta sigara, ambazo tulimwibia baba. Nilipokuwa na umri wa miaka sita, nililewa kwa mara ya kwanza. Muda mfupi baada ya hapo, wazazi wangu waliachana na mazoea yangu mabaya yakazidi kuongezeka.

 Mama alituchukua alipoanza kuishi na mwanamume mwingine. Mwanamume huyo hakumpa pesa zozote, na mama hangeweza kututegemeza kwa pesa kidogo alizopata. Hivyo, sisi watoto tukaanza kufanya kazi zozote tulizopata, lakini bado hatukupata pesa za kutosha kushughulikia mahitaji yetu. Nilipiga viatu rangi, na kuuza mikate, magazeti, chingamu, na vitu vingine. Pia, nilizurura jijini nikitafuta chakula katika mapipa ya takataka ya matajiri.

 Nilipokuwa na umri wa miaka kumi, mwanamume fulani alinialika nikafanye kazi naye katika eneo ambapo takataka zote za jiji zilitupwa. Nilikubali, nikaacha shule, na kuondoka nyumbani. Alinilipa pesa kidogo sana, na kunipa chakula kutoka kwenye takataka zilizokusanywa. Niliishi katika nyumba niliyojenga kutokana na vitu vilivyotupwa. Watu walionizunguka walitumia lugha chafu na walikuwa na maadili mapotovu. Wengi wao walikuwa waraibu wa dawa za kulevya na kileo. Kilikuwa kipindi kibaya zaidi maishani mwangu, na nililia kila usiku na kutetemeka kwa woga. Kwa sababu ya umaskini na elimu kidogo, nilikuwa na aibu sana. Niliishi kwenye eneo hilo la takataka kwa miaka mitatu hivi, kisha nikahamia jimbo lingine la Mexico. Huko nilifanya kazi shambani nikichuma maua na pamba, kukusanya miwa, na kuvuna viazi.

Niliishi katika eneo la kutupa takataka kama hili kwa miaka mitatu

 Miaka minne baadaye nilirudi Ciudad Obregón. Shangazi mmoja ambaye alikuwa mganga wa kienyeji, alinikaribisha nikae kwake. Nilianza kupata ndoto zenye kuogopesha na nikashuka moyo sana hivi kwamba nikaanza kuwa na mawazo ya kujiua. Siku moja nilisali kwa Mungu na kusema: “Bwana, ikiwa upo, ningependa kukujua, na nitakutumikia milele. Ikiwa kuna dini ya kweli, ningependa kuijua.”

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU

 Tangu zamani nilitaka sana kujifunza kumhusu Mungu. Nilipokuwa mtoto, nilienda kwenye makanisa ya dini mbalimbali, lakini zote zilinikatisha tamaa. Hakuna hata moja iliyozungumzia Biblia sana au iliyonisaidia kutimiza uhitaji wangu wa kumjua Mungu. Baadhi ya makanisa hayo yalikazia sana pesa, na mengine yalikuwa na waumini walioishi maisha mapotovu kiadili.

 Nilipokuwa na umri wa miaka 19, ndugu-mkwe aliniambia kwamba Mashahidi wa Yehova walimwonyesha maoni ya Biblia kuhusu sanamu. Akanisomea Kutoka 20:4, 5. Inasema kwamba hatupaswi kutengeneza sanamu za kuchongwa. Mstari wa 5 unasema: “Usiviinamie wala kushawishiwa kuviabudu, kwa sababu mimi, Yehova Mungu wako, ni Mungu ninayetaka watu waniabudu mimi peke yangu.” Kisha akaniuliza, “Ikiwa Mungu anatumia sanamu kufanya miujiza au anataka tuzitumie katika ibada, kwa nini ametukataza kuzitengeneza?” Hilo lilinifanya nianze kudadisi. Baada ya hapo, tukawa na mazungumzo mara kadhaa kuhusu habari zilizo katika Biblia. Nilifurahia sana mazungumzo hayo hivi kwamba muda ulikuwa ukipita haraka sana.

 Baadaye, alinipeleka kwenye mkutano wa Mashahidi wa Yehova. Nilifurahishwa sana na mambo niliyoona na kusikia. Hata vijana walishiriki programu hiyo na kuzungumza kwa ufasaha wakiwa jukwaani! Nilijiambia, ‘Watu hawa wanapata elimu ya hali ya juu!’ Licha ya kuwa na nywele ndefu na kutokuwa nadhifu, Mashahidi walinikaribisha kwa uchangamfu. Familia moja hata ilinikaribisha nyumbani kwao kwa ajili ya mlo baada ya mikutano!

 Kadiri nilivyojifunza Biblia na Mashahidi, niligundua kwamba Yehova Mungu ni Baba mwenye upendo ambaye anatujali licha ya hali yetu ya kiuchumi, msimamo katika jamii, rangi, au elimu tuliyo nayo. Hana ubaguzi hata kidogo. (Matendo 10:34, 35) Mwishowe, mahitaji yangu ya kiroho yalikuwa yakitimizwa. Sikuhisi tena kuwa sina furaha au nimekosa jambo muhimu maishani.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA

 Maisha yangu yalianza kubadilika kabisa na kuwa bora! Niliacha kuvuta sigara, kutumia kileo vibaya, na kutumia lugha chafu. Hisia za chuki nilizokuwa nazo tangu utotoni zilianza kupotea, na vilevile nikaacha kuota ndoto zenye kuogopesha. Niliacha kuwa na hisia za kujiona kuwa duni, hisia zilizotokana na maisha mabaya ya utotoni na kutopata elimu ya kutosha.

 Nina mke mzuri ambaye anampenda Yehova na ananitegemeza sana. Sasa mimi ni mwangalizi wa mzunguko, ninayatembelea makutaniko ya Mashahidi wa Yehova ili kuwatia moyo na kuwafundisha ndugu na dada ambao ni familia yangu ya kiroho. Kwa sababu ya uwezo wa Biblia wa kuponya na elimu ya hali ya juu ambayo Mungu hutoa, sasa sioni aibu tena.

Mimi na mke wangu tunafurahia kuwasaidia wengine kama nilivyosaidiwa