Hamia kwenye habari

BIBLIA INABADILI MAISHA

Hatimaye Niliacha Kumchukia Baba Yangu

Hatimaye Niliacha Kumchukia Baba Yangu
  • ALIZALIWA: 1954

  • NCHI: Filipino

  • HISTORIA: Nilimchukia baba mwenye jeuri

MAISHA YANGU YA ZAMANI

 Watalii wengi hutembelea maporomoko ya maji yanayojulikana sana karibu na mji wa Pagsanjan nchini Filipino. Baba yangu, Nardo Leron, alilelewa huko katika hali ya umaskini. Baada ya kuona ufisadi katika serikali, kikosi cha polisi, na kazini, alichukizwa na akawa na hasira.

 Wazazi wangu walifanya kazi kwa bidii ili kutulea sisi watoto wanane. Muda mwingi hawakuwa nyumbani, wakitunza mashamba milimani. Mara nyingi, mimi na ndugu yangu Rodelio tulilazimika kujitunza, tulikuwa na njaa. Tukiwa watoto, hatukuwa na muda wa kucheza. Tulipofikia umri wa miaka saba, kila mtoto alilazimika kufanya kazi kwenye mashamba na kubeba mizigo mizito ya nazi kwenye njia za mlimani zenye mteremko mkali. Mzigo ukiwa mzito sana, tulilazimika kuuburuza ardhini.

 Tulivumilia kuchapwa na baba, lakini tuliumia hata zaidi kumwona akimpiga mama. Tulijaribu kumfanya aache, lakini hatukuwa na uwezo. Mimi na Rodelio tulikubaliana kisiri kwamba tutamuua baba tutakapokuwa wakubwa. Nilitamani sana kuwa na baba aliyetupenda!

 Nikiwa nimechukizwa na kukasirishwa na ujeuri wa baba, niliondoka nyumbani nilipokuwa na umri wa miaka 14. Kwa muda fulani niliishi mtaani na nikaanza kutumia bangi. Mwishowe nilifanya kazi kwenye mashua, niliwapeleka watalii kwenye maporomoko ya maji.

 Miaka michache baadaye, nilianza masomo ya chuo kikuu katika jiji la Manila. Lakini nilisafiri kila mwisho juma kwenda Pagsanjan ili kufanya kazi, kwa hiyo, nilikuwa na muda mchache wa kusoma. Maisha yangu hayakuwa na maana, na bangi iliacha kunisaidia kupunguza wasiwasi. Hivyo, nikaanza kutumia dawa kali zaidi za kulevya, yaani, methamphetamine, kokeini, na heroini. Mara nyingi, mtu anapotumia dawa za kulevya, anakuwa na maadili mapotovu. Nilizungukwa na umaskini, ukosefu wa haki, na kuteseka. Nilichukia serikali na kuilaumu kwa hali hizo mbaya. Nilimwuliza Mungu, “Kwa nini maisha yako hivi?” Lakini sikupata majibu katika dini mbalimbali nilizochunguza. Nilitumia dawa zaidi ili kuficha hali yangu ya kukata tamaa.

 Mwaka wa 1972, wanafunzi nchini Filipino walipanga maandamano dhidi ya serikali. Nilishiriki maandamano hayo, na baadaye yakasababisha vurugu. Watu wengi walikamatwa, na miezi kadhaa baadaye jeshi likaanza kutawala nchini kote.

 Nilirudi mitaani tena kwa kuwa niliwaogopa wenye mamlaka wangenifuata kwa sababu ya kushiriki uasi huo. Ili kuendeleza zoea langu la kutumia dawa za kulevya, nilianza kuiba na mwishowe nilijihusisha na maadili mapotovu ili nipate pesa kutoka kwa matajiri na watu wa nchi nyingine. Sikujali ikiwa ningeishi au kufa.

 Katika kipindi hichohicho, mama na ndugu yangu walianza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Baba alikasirika na kuteketeza machapisho yao ya Biblia. Lakini wote wawili walivumilia na wakabatizwa.

 Siku moja, Shahidi fulani alizungumza na baba kuhusu ahadi ya Biblia ya wakati ujao ambapo kutakuwa na haki ya kweli duniani pote. (Zaburi 72:12-​14) Tumaini hilo lilimpendeza sana baba hivi kwamba akaamua kulichunguza. Alipojifunza Biblia, alikuta ahadi ya Mungu ya serikali itakayoleta haki na pia akaona matakwa ya Mungu kwa waume na akina baba. (Waefeso 5:​28; 6:4) Muda mfupi baadaye, yeye na ndugu zangu wengine wote wakawa Mashahidi. Kwa sababu nilikuwa mbali na nyumbani, sikujua yote hayo yalikuwa yametukia.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU

 Mwaka wa 1978, nilihamia Australia. Lakini hata katika nchi hiyo yenye amani na ufanisi, sikupata amani ya akili. Niliendelea kutumia kileo na dawa za kulevya. Baadaye katika mwaka huo, Mashahidi wa Yehova walinitembelea. Nilifurahia mambo waliyonionyesha katika Biblia kuhusu dunia yenye amani, lakini niliogopa kujihusisha nao.

 Muda mfupi baadaye, nilirudi nchini Filipino kwa majuma kadhaa. Ndugu zangu waliniambia kwamba baba alikuwa amejitahidi na sasa alikuwa mtu bora zaidi, lakini nilikuwa na uchungu mwingi moyoni hivi kwamba sikutaka kukutana naye.

 Dada yangu mdogo alinieleza kupitia Biblia kwa nini maisha yamejawa na kuteseka na ukosefu wa haki. Nilishangaa kwamba msichana mdogo ambaye hakuwa amepitia mengi maishani angeweza kujibu maswali yangu. Kabla ya kuondoka, baba alinipa kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani. a Akaniambia: “Acha kuhangaika. Kitabu hiki kitakusaidia kupata unachotafuta.” Akanihimiza niwatafute Mashahidi wa Yehova nitakaporudi Australia.

 Nilifuata ushauri wa baba na nikapata Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova karibu na nyumbani kwangu jijini Brisbane. Nilikubali kujifunza Biblia. Unabii wa Biblia kama ule wa Danieli sura ya 7 na Isaya sura ya 9 linionyesha kwamba serikali ya Mungu, ambayo haina ufisadi hata kidogo, itatutawala wakati ujao. Nilijifunza kwamba tutafurahia Paradiso hapa duniani. Nilitaka kibali cha Mungu, lakini nilitambua kuwa nilihitaji kudhibiti hisia zangu, kuacha kutumia dawa za kulevya na kutumia kileo vibaya, na kuacha maadili mapotovu. Nilitengana na msichana niliyeishi naye, na nikashinda uraibu wangu. Kadiri nilivyoendelea kumtegemea Yehova, ndivyo nilivyosali ili nipate msaada wake nifanye mabadiliko mengine.

 Hatua kwa hatua, niligundua kwamba mambo niliyojifunza yangeweza kumbadili mtu. Biblia inasema kwamba tukijitahidi, tunaweza kujivika “utu mpya.” (Wakolosai 3:​9, 10) Nilipojaribu kufanya hivyo, nikagundua kwamba kile nilichosikia kuhusu baba kubadili utu wake huenda ni kweli. Badala ya kuwa na hasira na chuki, nilitaka kufanya amani pamoja naye. Mwishowe, nilimsamehe baba na nikaacha kufungia chuki niliyokuwa nayo tangu utotoni.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA

 Nikiwa kijana, mara nyingi niliwafuata wengine na kuingia katika mazoea yenye kudhuru. Onyo la Biblia lilinihusu​—marafiki wabaya walikuwa wamenipotosha. (1 Wakorintho 15:33) Lakini nimepata marafiki wanaotegemeka miongoni mwa Mashahidi wa Yehova, na wamenisaidia kuwa mtu bora zaidi. Pia nilipata mke wangu mpendwa, Loretta. Tukiwa pamoja, tunawafundisha watu jinsi Biblia inavyoweza kuwasaidia.

Kufurahia mlo pamoja na mke wangu na marafiki

 Kwa sababu ya Biblia, nimemwona baba akibadiIika na kuwa mtu ambaye sikuwahi kutarajia, yaani, amekuwa mume mwenye upendo na Mkristo mnyenyekevu anayependa amani. Tulipokutana baada ya mimi kubatizwa mwaka wa 1987, baba alinikumbatia kwa mara ya kwanza maishani mwangu!

 Kwa miaka zaidi ya 35, baba aliendelea kufanya kazi pamoja na mama ya kuwatangazia watu ujumbe wa tumaini ulio katika Biblia. Alikuwa mwanamume mwenye bidii na anayejali, na alijulikana kwa kuwasaidia watu. Katika miaka hiyo, nilijifunza kumheshimu na kumpenda. Nilijivunia kuwa mwana wake! Alikufa mwaka wa 2016, lakini nina kumbukumbu nzuri sana, nikijua kwamba sote tulifanya mabadiliko makubwa katika utu wetu tulipofuata mafundisho ya Biblia. Sina chuki yoyote moyoni. Ninathamini sana kwamba nilimpata Baba yangu wa mbinguni, Yehova Mungu, ambaye anaahidi kukomesha chanzo cha maumivu yote katika familia.

a Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova lakini sasa hakichapishwi tena.