Hamia kwenye habari

BIBLIA INABADILI MAISHA

“Mimi Si Mkatili Tena”

“Mimi Si Mkatili Tena”
  • Alizaliwa: 1973

  • Nchi: Uganda

  • Historia: Alipenda jeuri na mlevi

MAISHA YANGU YA ZAMANI

 Nilizaliwa nchini Uganda katika wilaya ya Gomba. Watu wengi walikuwa maskini katika eneo hilo. Mji wetu haukuwa na umeme, kwa hiyo ilipofika usiku tulitumia taa za mafuta.

 Wazazi wangu, ambao walikuwa wakulima, walihamia Uganda kutoka Rwanda. Walilima kahawa na ndizi, na kwa kutumia ndizi hizo, walitengeneza pombe maarufu ya kienyeji inayoitwa waragi. Pia walifuga kuku, mbuzi, nguruwe, na ng’ombe. Utamaduni wangu na malezi yangu yalinifanya niamini kwamba mke anapaswa kumtii mume wake wakati wote na kwamba mke hakupaswa kueleza maoni yake.

 Nilipokuwa na umri wa miaka 23, nilihamia Rwanda. Nilipokuwa huko nilienda kwenye klabu za muziki pamoja na vijana wengine wa rika langu. Nilirudi mara nyingi kwenye klabu moja hivi kwamba wasimamizi walinipa kadi iliyoniruhusu kuingia katika klabu hiyo bila kulipa kiingilio. Vilevile, nilipenda kutazama sinema zilizohusisha kupigana na ukatili. Mazingira yangu na burudani nilizochagua ziliniathiri sana hivyo nikawa mkatili na mlevi kupindukia.

 Mwaka 2002, nilianza kuishi na mwanamke anayeitwa Skolastique Kabagwira na tukapata watoto watatu. Kama nilivyoamini tangu nilipokuwa mdogo, nilitarajia apige magoti kila mara aliponisalimu au alipokuwa akiniomba kitu fulani. Pia, niliamini kwamba vitu vyote tulivyokuwa navyo ni vyangu mwenyewe na nilikuwa na uhuru wa kuvitumia kama nilivyopenda. Mara nyingi niliondoka nyumbani usiku na kurudi saa tisa alfajiri nikiwa nimelewa. Nilibisha mlango, na ikiwa Skolastique angechelewa kufungua, nilimpiga.

 Wakati huo, nilikuwa nikifanya kazi katika kampuni binafsi ya ulinzi nikiwa kama msimamizi, kwa hiyo nilipata mshahara mzuri. Skolastique alijaribu kunishawishi nijiunge naye katika kanisa la Kipentekoste, akifikiri kwamba kufanya hivyo kungenibadilisha. Lakini sikupendezwa na wazo hilo. Badala yake, nilianzisha uhusiano wa kimapenzi na mwanamke mwingine. Kwa sababu ya ukatili na mwenendo wangu mpotovu, Skolastique aliondoka na watoto wetu watatu na kurudi nyumbani kwa wazazi wake.

 Rafiki yetu mmoja mwenye umri mkubwa, alizungumza nami kuhusu maisha yangu. Alinitia moyo nimrudie Skolastique. Alisema kwamba watoto wetu walipaswa kuwa na baba yao. Kwa hiyo, mwaka 2005, niliacha kunywa pombe, nikamwacha yule mwanamke mwingine, na nikarudiana na Skolastique. Tulioana mwaka 2006. Hata hivyo bado nilikuwa mkatili na nilimpiga mke wangu.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU

 Mwaka 2008, Joël, mmoja wa Mashahidi wa Yehova, alitutembelea nyumbani na nilisikiliza ujumbe wake. Kwa miezi kadhaa, yeye na Shahidi mwingine anayeitwa Bonaventure, walinitembelea mara kwa mara, na tulikuwa mazungumzo mengi ya Biblia. Niliuliza maswali mengi, hasa maswali yanayohusu kitabu cha Ufunuo. Jambo nililokuwa nikijaribu kufanya ni kuthibitisha kwamba Mashahidi walikuwa wamekosea. Kwa mfano, niliwauliza wanawezaje kusema kwamba “umati mkubwa” unaotajwa kwenye Ufunuo 7:9 utaishi duniani, ilhali mstari huo unasema walikuwa “wamesimama mbele ya kiti cha ufalme [cha Mungu] na mbele ya Mwanakondoo,” Yesu Kristo. Joël alijibu maswali yangu kwa subira. Kwa mfano, alinionyesha Isaya 66:1, ambapo Mungu anasema dunia ni ‘kiti cha miguu yake.’ Kwa hiyo, umati mkubwa umesimama kihalisi mbele ya kiti cha ufalme cha Mungu. Kisha nikasoma Zaburi 37:29, inayoonyesha kwamba waadilifu wataishi milele duniani.

 Hatimaye, nilikubali funzo la Biblia. Kwa hiyo, Bonaventure akaanza kujifunza Biblia pamoja nami na Skolastique. Tulipokuwa tukijifunza Biblia, nilianza kuchochewa kufanya mabadiliko maishani. Nilijifunza kumtendea mke wangu kwa heshima. Sikutaka tena apige magoti aliponisalimu au alipoomba kitu fulani, na nikaacha kudai kwamba vitu vyote tulivyokuwa navyo ni vyangu. Pia niliacha kutazama sinema zinazohusisha jeuri. Haikuwa rahisi kufanya mabadiliko hayo na nilihitaji kujizuia sana na kuwa mnyenyekevu.

Biblia imenisaidia kuwa mume mzuri.

 Miaka kadhaa kabla ya hapo, nilikuwa nimempeleka mwana wangu mkubwa, Christian, akaishi na ndugu zangu huko Uganda. Lakini baada ya kusoma Kumbukumbu la Torati 6:4-7, nilitambua kwamba mimi na mke wangu tuna jukumu kutoka kwa Mungu la kuwatunza watoto wetu, ambalo linatia ndani kuwafundisha kanuni za Biblia. Tulifurahi sana aliporudi nyumbani naye pia alifurahi sana.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA

 Nimejifunza kwamba Yehova ni Mungu mwenye rehema, na ninaamini kwamba amesamehe mwenendo na mtazamo wangu wa zamani. Ninafurahi kwamba Skolastique alijiunga nami kujifunza Biblia. Tulijiweka wakfu kwa Yehova na sote wawili tulibatizwa Desemba 4, 2010. Sasa tunaaminiana, na tunafurahia kutumia kanuni za Biblia katika familia yetu. Mke wangu anafurahi sana kwa kuwa sasa ninarudi nyumbani moja kwa moja baada ya kutoka kazini. Pia anathamini kwamba sasa ninamtendea kwa heshima, nimeamua kuacha kunywa pombe kabisa, na kwamba mimi si mkatili tena. Mwaka 2015, niliwekwa rasmi kuwa mzee wa kutaniko ili kusaidia kulichunga kutaniko letu. Tuna watoto watano na watatu kati yao wamebatizwa.

 Nilipoanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova, sikukubali tu mambo waliyonifundisha bila kujithibitishia. Nilipendezwa na jinsi walivyotumia Biblia kujibu maswali yangu. Mimi na Skolastique tumefurahi kujua kwamba wale wanaodai kumtumikia Mungu wanapaswa kutii kila kitu anachofundisha si kutii tu mambo wanayotaka. Ninamshukuru Yehova zaidi kwa kunivuta kwake na sasa mimi ni sehemu ya familia yake ya kiroho. Ninapotafakari kuhusu maisha yangu ya zamani, nina hakika kwamba kwa msaada wa Mungu, mtu yeyote mnyoofu anaweza kufanya mabadiliko yanayohitajika ili kumpendeza.