Hamia kwenye habari

BIBLIA INABADILI MAISHA

Nilipata Utajiri wa Kweli

Nilipata Utajiri wa Kweli
  • Alizaliwa: 1968

  • Nchi: Marekani

  • Historia: Mfanyabiashara aliyesali awe tajiri

MAISHA YANGU YA ZAMANI

 Nililelewa katika familia ya Kikatoliki, katika Rochester, New York. Wazazi wangu walitengana nilipokuwa na umri wa miaka nane. Basi, siku za katikati ya juma niliishi na mama yangu katika nyumba za watu maskini na miisho juma nilikaa na baba yangu katika eneo la matajiri. Nilipoona jinsi mama yangu alivyopata taabu kunilea mimi na ndugu zangu watano, niliazimia kwamba siku moja nitaiwezesha familia yetu iwe tajiri.

 Baba yangu alitaka nifanikiwe maishani, basi akafanya mipango nikatembelee shule maarufu zaidi inayotoa masomo ya usimamizi wa hoteli. Niliipenda sana na mara moja nikaanza masomo, nikiwa na uhakika kwamba Mungu amejibu sala yangu ya kuwa tajiri na mwenye furaha. Nilijifunza jinsi ya kusimamia hoteli, sheria ya biashara, na jinsi ya kusimamia fedha za shirika kwa miaka mitano huku nikifanya kazi katika hoteli yenye kasino katika jiji la Las Vegas, Nevada.

Kazi yangu ilitia ndani kuwapikia chakula watu matajiri waliocheza kamari

 Nikiwa na umri wa miaka 22, nilikuwa makamu wa rais msaidizi wa hoteli yenye kasino. Nilionwa kuwa tajiri, mwenye mafanikio na mara nyingi nilifurahia chakula bora na divai na pombe za bei ghali. Rafiki zangu tuliofanya nao biashara walikuwa wakiniambia “Pesa ndiyo kila kitu katika dunia hii.” Waliona kwamba pesa huleta furaha ya kweli.

 Kazi yangu ilitia ndani kuwapikia chakula watu matajiri zaidi waliokuja Las Vegas ili kucheza kamari. Ingawa walikuwa matajiri sana hawakuwa na furaha. Mimi pia nilianza kukosa furaha. Kwa kweli, kadiri nilivyopata pesa nyingi zaidi, ndivyo nilivyozidi kuwa na mahangaiko mengi na kukosa usingizi. Nilianza kufikiria kujiua. Nikiwa nimevunjika moyo kutokana na hali ya maisha yangu, niliamua kumuuliza Mungu, “Nitapata wapi furaha ya kweli?”

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU

 Kufikia wakati huo, dada zangu wawili waliokuwa Mashahidi wa Yehova walihamia Las Vegas. Ijapokuwa nilikataa machapisho yao, nilikubali kujifunza Biblia kwa kutumia nakala yangu. Katika Biblia yangu, maneno ya Yesu yalikuwa yameandikwa kwa wino mwekundu. Kwa kuwa nilikubali kila kitu alichosema Yesu, dada zangu walizungumzia yale aliyosema. Pia, nilijisomea mwenyewe Biblia.

 Nilishangazwa na mambo mengi niliyosoma. Kwa mfano, Yesu alisema: “Mkiwa katika kusali, msipayuke-payuke, kama watu wa mataifa; maana wao hudhani ya kuwa watasikiwa kwa sababu ya maneno yao kuwa mengi.” (Mathayo 6:7, Union Version) Hata hivyo, kasisi alinipa picha ya Yesu na aliniambia kwamba nikisali kwa kutumia picha hiyo, huku nikirudia mara kumi sala ya Baba Yetu na mara kumi Maria Mtakatifu, Mungu angenipa kiasi chochote cha pesa nilichohitaji. Hata hivyo, niligundua kwamba kurudia-rudia maneno kulikuwa kupayuka-payuka. Pia, nilisoma maneno haya ya Yesu: “Wala msimwite mtu baba duniani; maana Baba yenu ni mmoja, aliye wa mbinguni.” (Mathayo 23:9, UV) Basi, nikajiuliza tena, ‘Kwa nini mimi na Wakatoliki wenzangu tunawaita makasisi wetu “Baba”?’

 Nilipofika katika kitabu cha Biblia cha Yakobo katika usomaji wangu, nilianza kutafakari zaidi kuhusu maisha yangu. Katika sura ya 4, Yakobo ameandika hivi: “Hamjui ya kwamba kuwa rafiki wa dunia ni kuwa adui wa Mungu? Basi, kila atakaye kuwa rafiki wa dunia hujifanya kuwa adui wa Mungu.” (Yakobo 4:4, UV) Niliguswa zaidi na mstari wa 17: “Basi yeye ajuaye kutenda mema, wala hayatendi, kwake huyo ni dhambi.” Kisha niliwapigia simu dada zangu na kuwaeleza kwamba ninaacha kazi yangu ya hoteli na kasino kwa sababu ilihusisha mambo ambayo sikukubali, kutia ndani kucheza kamari na pupa.

“Nilipofika katika kitabu cha Biblia cha Yakobo katika usomaji wangu, nilianza kutafakari zaidi kuhusu maisha yangu”

 Nilitaka kuboresha uhusiano wangu na Mungu, wazazi na ndugu zangu. Basi nikaazimia kutumia wakati kurahisisha maisha yangu. Hata hivyo, haikuwa rahisi kufanya mabadiliko hayo. Kwa mfano, nilipewa nafasi za kufanya kazi na kuwa na mafanikio zaidi katika biashara ya kasino na hoteli na hata kupata mshahara mara mbili au tatu zaidi ya niliokuwa napata awali. Hata hivyo, baada ya kusali kuhusu jambo hilo, niliamua kuachana kabisa na maisha hayo. Niliacha kazi yangu, nikahamia katika gereji iliyokuwa kwenye nyumba ya mama yangu na nikaanzisha biashara ndogo ya kuweka jalada menyu za mikahawa.

 Ingawa Biblia ilinisaidia kuwa na malengo yanayofaa, bado sikuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova. Dada zangu waliniomba niwaambie kinachonizuia kuhudhuria mikutano ya Mashahidi. Niliwajibu hivi: “Mungu wenu Yehova, anatenganisha familia. Wakati pekee ambao ninaweza kuwa pamoja na familia ni katika sikukuu za Krismasi na kuzaliwa, sherehe ambazo ninyi hamsherehekei.” Dada yangu mmoja alianza kulia huku akiniuliza: “Siku nyingine za mwaka unakuwa wapi? Sisi tungependa kuwa pamoja nawe siku zote. Lakini wewe unapenda kuja wakati wa sikukuu hizo tu—ili tu utimize wajibu.” Maneno yake yaligusa moyo, nami nikaanza kulia pamoja naye.

 Nilipojua jinsi Mashahidi wa Yehova wanavyopenda familia zao, tofauti kabisa na nilivyokuwa nikifikiri, niliamua kuhudhuria mkutano mmoja katika Jumba la Ufalme. Nikiwa katika mkutano huo, nilikutana na Kevin, mwalimu wa Biblia mwenye uzoefu aliyeanza kunifundisha Biblia.

 Kevin na mke wake waliishi maisha rahisi ili watumie muda wao mwingi zaidi kuwasaidia watu waifahamu Biblia. Kiasi cha pesa walichopata kilitosha kuwasaidia kutembelea bara la Afrika na Amerika ya Kati, ili kusaidia kujenga ofisi za tawi za Mashahidi. Walikuwa na furaha sana na walipendana sana. Nilijiambia, ‘Ningependa sana kuwa na maisha kama yao.’

 Kevin alinionyesha video iliyozungumzia shangwe za utumishi wa umishonari, nami nikaamua kwamba hiyo ndiyo kazi ninayopenda kufanya. Mwaka wa 1995, baada ya kujifunza Biblia kwa bidii kwa miezi sita, nilibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova. Badala ya kumwomba Mungu anipe utajiri, nilisali na kusema:“Usinipe umaskini wala utajiri.”—⁠Methali 30:8.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA

 Sasa nimepata utajiri wa kweli—⁠si wa pesa, bali wa kiroho. Nilikutana na mke wangu mpendwa Nuria, nchini Honduras, na kwa pamoja tumetumikia kama wamishonari nchini Panama na Mexico. Maneno haya ya Biblia ni ya kweli kabisa: “Baraka ya Yehova ndiyo inayomtajirisha mtu, naye haichanganyi na maumivu”!—⁠Methali 10:22.