Hamia kwenye habari

BIBLIA INABADILI MAISHA

“Uhalifu na Kupenda Pesa Kuliniletea Maumivu Makubwa”

“Uhalifu na Kupenda Pesa Kuliniletea Maumivu Makubwa”
  • Alizaliwa: 1974

  • Nchi: Albania

  • Historia: Mwizi, mlanguzi wa dawa za kulevya, mfungwa

MAISHA YANGU YA ZAMANI

 Nilizaliwa katika familia maskini huko Tiranë, mji mkuu wa Albania. Baba yangu alikuwa mwanamume mnyoofu aliyefanya kazi saa nyingi ili kututunza. Lakini ni kana kwamba hatukuwa na pesa za kutosha kushughulikia mahitaji yetu. Nilipokuwa mvulana, nilisikitishwa sana na umaskini wetu. Sehemu kubwa ya maisha yangu ya utotoni, sikuwa na viatu wala chakula cha kutosha.

 Nilianza kuiba nilipokuwa na umri mdogo sana. Nilijiambia kwamba nilikuwa nikisaidia familia yangu. Hatimaye, polisi walinikamata. Kwa hiyo, mnamo 1988, nilipokuwa na umri wa miaka 14, baba alinipeleka kwenye shule ya kurekebisha tabia. Nilikaa huko kwa miaka miwili na nikajifunza kuchomelea vyuma. Nilipomaliza shule, nilitaka kufanya kazi; hata hivyo, sikupata kazi. Watu wengi hawakuwa na kazi kwa sababu kulikuwa na msukosuko wa kisiasa nchini Albania. Nilivunjika moyo, kwa hiyo, nikaanza kutumia muda mwingi na marafiki wa zamani na nikaanza kuiba tena. Mwishowe, mimi na rafiki zangu tulikamatwa na kuhukumiwa miaka mitatu gerezani.

 Baada ya kuachiliwa kutoka gerezani, niliendelea na uhalifu. Uchumi wa Albania ulikuwa umeanguka, na kulikuwa na vurugu nchini kote. Wakati wa kipindi hicho cha msukosuko, nilipata pesa nyingi kutokana na shughuli za magendo. Pindi moja tulipoiba kwa kutumia bunduki, rafiki zangu wawili walikamatwa. Niliondoka nchini ili kuepuka kifungo cha muda mrefu. Wakati huo nilikuwa nimefunga ndoa na Julinda, na tulikuwa na mtoto wa kiume.

 Hatimaye, tulifika nchini Uingereza. Nilitaka sana kuanza maisha mapya nikiwa na mke wangu na mwana wetu, lakini ilikuwa vigumu kuacha tabia zangu za zamani. Nilianza tena maisha ya uhalifu, pindi hii nikijihusisha katika biashara ya dawa za kulevya, iliyoniletea pesa nyingi.

 Julinda alihisije kuhusu biashara hiyo ya dawa za kulevya? Acheni asimulie: “Nilipokuwa mdogo kule Albania, nilitamani sana kuukimbia umaskini. Nilikuwa tayari kujaribu jambo lolote ili nipate maisha mazuri zaidi. Nilifikiri pesa zingeboresha maisha yetu, kwa hiyo nilimuunga mkono Artan kikamili katika shughuli zake zilizohusisha kusema uwongo, kuiba, na kuuza dawa za kulevya—chochote ambacho kingetuletea pesa.”

“Nilimuunga mkono Artan kikamili katika shughuli zake zilizohusisha kusema uwongo, kuiba, na kuuza dawa za kulevya.”—Julinda.

 Kisha, mnamo 2002, maisha yetu yalibadilika na mipango yetu yote ya kuishi maisha bora yakakomeshwa. Nilikamatwa nilipokuwa nikisafirisha shehena kubwa ya dawa za kulevya na nikafungwa tena.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU

 Biblia ilianza kuwa na uvutano fulani maishani mwangu hata bila mimi kujua. Katika mwaka wa 2000, Julinda alikutana na Mashahidi wa Yehova na akaanza kujifunza Biblia pamoja nao. Sikupenda kuzungumzia Biblia kwa sababu niliona kwamba inachosha. Lakini Julinda alifurahia sana kufanya hivyo. Anaeleza hivi: “Familia yetu ilikuwa ya kidini, nami niliipenda na kuiheshimu Biblia. Nilitaka kujua inafundisha nini, na nilifurahi sana kujifunza Biblia na Mashahidi. Mafundisho mengi ya Biblia yalipatana sana na akili. Mambo niliyojifunza yalinisaidia kufanya mabadiliko fulani maishani. Hata hivyo, mtazamo wangu kuelekea pesa haukubadilika sana. Ulibadilika tu Artan alipokamatwa. Tukio hilo lilinishtua. Ghafla, nilitambua kile ambacho Biblia inasema kuhusu pesa ni kweli. Tulikuwa tumezitafuta kwa bidii, lakini hazikutuletea furaha. Hapo ndipo nilipotambua kwamba nilihitaji kufuata viwango vya Mungu kikamili.”

 Mnamo 2004, niliachiliwa kutoka gerezani, na mara tu baada ya hapo nikajaribu kuanza tena biashara ya dawa za kulevya. Hata hivyo, mtazamo wa Julinda ulikuwa umebadilika, naye alisema jambo fulani lililonifanya nifikiri kwa uzito: “Sitaki pesa zako tena. Sitaki mume wangu aondoke tena, na ningependa baba ya watoto wangu awe hapa kila wakati ili awatunze.” Nilishtuka, lakini hakuwa amekosea. Kwa miaka mingi sikuwa pamoja na familia yangu. Pia, nilifikiria kuhusu maumivu mengi niliyokuwa nimepata kwa sababu ya kukimbizana na pesa kwa njia isiyo halali. Kwa hiyo niliamua kubadili mwenendo wangu na kuacha kutumia muda na rafiki zangu wa zamani.

 Niliguswa moyo sana nilipoenda na mke wangu na wana wetu kwenye mkutano wa Mashahidi wa Yehova. Nilivutiwa sana na urafiki na unyoofu wa watu niliokutana nao huko. Hatimaye, nikaanza kujifunza Biblia.

Zamani nilifikiri kwamba ikiwa tungekuwa na pesa nyingi, tungekuwa na furaha

 Nilijifunza katika Biblia kwamba “kupenda pesa ndicho chanzo cha mambo mabaya ya kila aina, na kwa kujitahidi kufikia upendo huo, wengine . . . [wamejichoma] kila mahali kwa maumivu mengi.” (1 Timotheo 6:9, 10) Nilielewa vizuri kabisa ukweli wa andiko hilo! Nilisikitishwa sana na madhara na maumivu ambayo mimi na familia yangu tulipata kwa sababu ya maisha yangu ya zamani. (Wagalatia 6:7) Nilipojifunza kuhusu upendo ambao Yehova na Mwana wake, Yesu Kristo, wanao kutuelekea, nilianza kubadili utu wangu. Niliacha kujifikiria kupita kiasi na kuanza kufikiria kuhusu wengine, kutia ndani kutumia muda mwingi zaidi na familia yangu.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA

 Nimenufaika kwa kufuata ushauri huu wa Biblia: “Njia yenu ya maisha iwe bila upendo wa pesa, huku mkiridhika na vitu mlivyo navyo.” (Waebrania 13:5) Sasa nina amani ya akili na dhamiri safi. Hilo limeniletea shangwe ambayo sijawahi kuhisi tena. Ndoa yangu ni imara zaidi, na familia yangu ina uhusiano wa karibu zaidi.

 Zamani nilifikiri kwamba ikiwa tungekuwa na pesa nyingi, tungekuwa na furaha. Sasa ninaona wazi kwamba uhalifu na kupenda pesa kuliniletea maumivu mengi. Sisi si matajiri, lakini ninahisi kwamba tumepata kitu muhimu zaidi maishani—urafiki pamoja na Yehova Mungu. Kumwabudu kwa umoja tukiwa familia kunatuletea furaha nyingi sana.

Nikiwa na familia yangu katika kusanyiko la Mashahidi wa Yehova