Hamia kwenye habari

BIBLIA INABADILI MAISHA

“Nilikuwa na Maswali Mengi Kuliko Majibu”

“Nilikuwa na Maswali Mengi Kuliko Majibu”
  • Alizaliwa: 1976

  • Nchi: Honduras

  • Historia: Kasisi

MAISHA YANGU YA ZAMANI

 Nilizaliwa katika jiji la La Ceiba, Honduras. Familia yetu ilikuwa na watoto watano. Nilikuwa mtoto wa mwisho na mvulana pekee. Pia, ni mimi tu niliyekuwa kiziwi katika familia yetu. Tuliishi katika eneo hatari na tulikuwa maskini sana. Maisha yalikuwa magumu zaidi baba yangu alipokufa kutokana na aksidenti iliyotokea kazini. Nilikuwa na umri wa miaka minne tu.

 Mama yangu alijitahidi sana kututunza, lakini mara nyingi hakuwa na pesa za kutosha kuninunulia nguo. Mvua iliponyesha, nilihisi baridi kwa kuwa sikuwa na nguo za kunipasha joto.

 Tangu utotoni, nilianza kujifunza Lugha ya Ishara ya Honduras (LESHO), ambayo ilinisaidia kuwasiliana na viziwi wengine. Lakini mama yangu na dada zangu hawakujua lugha hiyo kwa hiyo walitumia ishara chache tu na wakabuni ishara ili kuwasiliana nami. Hata hivyo, mama yangu alinipenda na alinilinda kutokana na hatari nyingi. Kwa kutumia ishara chache alizojua, alinionya niepuke mambo mabaya kama vile kuvuta sigara na ulevi. Kwa sababu hiyo, ninashukuru kwamba niliepuka mambo hayo.

 Nilipokuwa mdogo, mama yangu alikuwa akinipeleka kwenye Kanisa Katoliki, lakini sikuelewa jambo lolote kwa kuwa hakuna mtu aliyenitafsiria kwa lugha ya ishara. Hilo lilinichosha sana hivi kwamba nikaacha kwenda kanisani nilipokuwa na umri wa miaka kumi. Hata hivyo, bado nilitaka kujua mengi zaidi kumhusu Mungu.

 Mwaka wa 1999, nilipokuwa na umri wa miaka 23, nilikutana na mwanamke fulani kutoka Marekani aliyekuwa wa kanisa la kiinjilisti. Alinifundisha masomo ya Biblia na pia akanifundisha Lugha ya Ishara ya Marekani (ASL). Nilipendezwa sana na kile nilichojifunza katika Biblia hivi kwamba nikaamua kuwa kasisi. Hivyo, nilihamia Puerto Riko ili nipate mafunzo ya Kikristo kwa ajili ya viziwi. Niliporudi La Ceiba mwaka wa 2002, nilisaidiwa na rafiki zangu kuanzisha kanisa la viziwi. Mmoja wa rafiki hao alikuwa Patricia, ambaye baadaye alikuja kuwa mke wangu.

 Nikiwa kasisi wa kanisa letu, niliwahutubia washiriki wa kanisa katika Lugha ya Ishara ya Honduras, nikaonyesha picha za hadithi za Biblia, na kuigiza hadithi hizo ili viziwi wazielewe. Pia, niliwatembelea viziwi katika miji ya karibu ili kuwatia moyo na kuwasaidia kukabiliana na matatizo yao. Hata nilifunga safari ya umishonari kwenda Marekani na Zambia. Lakini ukweli ni kwamba sikujua mengi kuhusu Biblia. Niliwaambia tu kile nilichokuwa nimeambiwa na kile nilichoelewa kutoka kwenye picha. Kwa kweli, nilikuwa na maswali mengi kuliko majibu.

 Siku moja, washiriki fulani wa kanisa letu walianza kueneza uwongo kunihusu. Walisema kwamba nilikuwa mlevi na sikuwa mwaminifu kwa mke wangu. Nilivunjika moyo na kukasirika. Muda mfupi baadaye mimi na Patricia tulijitenga na kanisa hilo.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU

 Mashahidi wa Yehova walikuwa wametutembelea mara nyingi, lakini sikuzote hatukutaka kuwasikiliza. Hata hivyo, baada ya kuondoka katika kanisa letu, Patricia alikubali kujifunza Biblia na wenzi wa ndoa Mashahidi, Thomas na Liccy. Kilichonivutia ni kwamba ingawa hawakuwa viziwi, walijua lugha ya ishara. Hivyo baada ya muda mfupi nilijiunga na Patricia alipokuwa akijifunza.

 Tulijifunza kwa miezi kadhaa kwa kutumia video za Lugha ya Ishara ya Marekani. Lakini baadhi ya rafiki zetu walipodai kuwa Mashahidi wa Yehova ni wafuasi wa watu, tuliacha kujifunza Biblia. Ijapokuwa Thomas alinionyesha uthibitisho unaoonyesha kwamba Mashahidi wa Yehova hawana viongozi wanadamu, sikumwamini.

 Baada ya miezi kadhaa, Patricia alishuka moyo sana, kwa hiyo, akasali kwamba Mungu awalete tena Mashahidi wa Yehova nyumbani kwetu. Muda mfupi baadaye, jirani yetu, ambaye ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova alimtembelea Patricia na kumuuliza ikiwa angependa amwombe Liccy aje kumtembelea. Liccy alithibitika kuwa rafiki wa kweli. Alimtembelea Patricia kila juma kumtia moyo na kujifunza Biblia pamoja naye. Lakini bado nilikuwa na shaka kuwahusu Mashahidi wa Yehova.

 Mwaka 2012, Mashahidi wa Yehova walipanga kampeni ya pekee ya kuonyesha video yenye kichwa Je, Ungependa Kujua Ukweli? katika Lugha ya Ishara ya Honduras. Liccy alituletea nakala ya video hiyo. Nilipoitazama, nilishtuka kujua kwamba mafundisho mengi niliyokuwa nikifundisha, kama vile moto wa mateso na nafsi isiyoweza kufa, hayakuwa katika Biblia.

 Juma lililofuata, nilienda kwenye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova ili kuzungumza na Thomas. Nilimwambia kwamba nilitaka kuwafundisha viziwi kweli kuhusu Biblia, lakini sikutaka kuwa Shahidi wa Yehova. Wazo langu lilikuwa kuanzisha kanisa jipya kwa ajili ya viziwi. Thomas alinipongeza kwa bidii yangu mpya lakini akanionyesha andiko la Waefeso 4:5, linaloonyesha kwamba kutaniko la Kikristo la kweli linapaswa kuwa na umoja.

 Pia, Thomas alinipa video yenye kichwa Mashahidi wa Yehova—Imani Yenye Matendo, Sehemu ya 1: Kutoka Gizani katika Lugha ya Ishara ya Marekani. Video hiyo ilionyesha jinsi kikundi fulani cha wanaume kilivyoichunguza Biblia kwa makini ili kuelewa ukweli kuhusu mafundisho ya msingi. Nilipotazama video hiyo nilielewa jinsi wanaume hao walivyohisi. Kama wao, mimi pia nilikuwa nikitafuta kweli. Video hiyo ilinithibitishia kwamba Mashahidi wanafundisha ukweli kwa sababu mafundisho yao yanategemea Biblia tu. Hivyo nilianza tena kujifunza Biblia, na mwaka wa 2014, mimi na Patricia tulibatizwa na kuwa Mashahidi wa Yehova.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA

 Ninalipenda kutaniko la Mashahidi wa Yehova kwa sababu ni safi kiadili, kama Mungu alivyo safi. Waabudu wake ni safi, katika maneno na matendo. Wanapenda amani na kutiana moyo. Mashahidi wana umoja na wote hufundisha mafundisho yaleyale ya Biblia hata iwe wao ni wa nchi gani au wanazungumza lugha gani.

 Nimefurahi kujifunza kile ambacho Biblia inafundisha hasa. Kwa mfano, nimejifunza kwamba Yehova ndiye Mungu Mweza-Yote, Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote. Anawapenda viziwi na wale walio na uwezo wa kusikia. Ninathamini sana upendo ambao Mungu amenionyesha. Pia, nimejifunza kwamba dunia itakuwa paradiso maridadi na kwamba tutakuwa na nafasi ya kufurahia uzima wa milele tukiwa na afya kamilifu. Ninasubiri kwa hamu siku ambayo mambo hayo yatatokea!

 Mimi na Patricia tunapenda kuwaeleza viziwi kuhusu Biblia. Sasa tunajifunza Biblia na baadhi ya washiriki wa kanisa letu la zamani. Lakini sina maswali tena kuhusu mambo ninayofundisha kama niliyokuwa nayo hapo awali nilipokuwa kasisi. Hatimaye, nimepata majibu ya maswali yangu yote kwa kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova.