Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 2

Biblia Inatupatia Tumaini

Biblia Inatupatia Tumaini

Watu ulimwenguni pote wanakabili matatizo yanayowafanya wawe na huzuni, wasiwasi, na hata maumivu. Je, umewahi kupatwa na hali iliyofanya uhisi hivyo? Labda unateseka kwa sababu ya ugonjwa au kwa sababu umefiwa na mtu unayempenda. Huenda unajiuliza, ‘Je, maisha yangu yatabadilika na kuwa mazuri?’ Biblia inajibu swali hilo kwa njia yenye kufariji.

1. Biblia inatupatia tumaini gani?

Biblia inaeleza sababu zinazofanya ulimwengu ujae matatizo, vilevile inatupatia habari njema kwamba matatizo haya ni ya muda mfupi na yatakwisha hivi karibuni. Ahadi za Biblia zinaweza kukupatia “wakati ujao na tumaini.” (Soma Yeremia 29:11, 12.) Ahadi hizo zinatusaidia kukabiliana na matatizo sasa, kuwa na mtazamo mzuri, na kupata furaha ya kudumu.

2. Biblia inaahidi nini kuhusu wakati ujao?

Biblia inaeleza kwamba wakati ujao “kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena.” (Soma Ufunuo 21:4.) Matatizo yanayofanya tukate tamaa maishani leo, kama vile umaskini, ukosefu wa haki, magonjwa, na kifo, hayatakuwapo tena. Biblia inaahidi kwamba wanadamu watafurahia kuishi milele katika Paradiso duniani.

3. Unawezaje kuwa na hakika kwamba ahadi za Biblia zitatimia?

Watu wengi wangependa kuwa na maisha mazuri, lakini hawana hakika ikiwa matarajio yao yatatimia. Hata hivyo, ahadi zilizo katika Biblia zitatimia. Tunaweza kuwa na uhakika kuhusu ahadi hizo kwa ‘kuyachunguza Maandiko kwa uangalifu.’ (Matendo 17:11) Unapojifunza Biblia, utapata usadikisho ambao utakusaidia kuamini mambo ambayo Biblia inasema kuhusu wakati ujao.

CHIMBA ZAIDI

Chunguza baadhi ya hali ambazo Biblia inaahidi kuhusu wakati ujao. Ona jinsi tumaini ambalo Biblia inatupatia linavyowasaidia watu leo.

4. Biblia inatupatia tumaini la kuishi milele bila matatizo

Ona orodha ifuatayo ya ahadi zilizo katika Biblia. Ni ahadi gani ambazo unapenda zaidi? Kwa nini?

Soma maandiko yaliyoambatanishwa na ahadi hizi, kisha ufikirie maswali haya:

  • Je, maandiko haya yanakupatia tumaini? Je, yanaweza kuwapatia tumaini watu wa familia yako na marafiki?

Wazia ukiishi katika ulimwengu ambao

HAKUNA MTU AMBAYE . . .

KILA MTU . . .

  • atahisi maumivu, atadhoofika kwa sababu ya kuzeeka, au kufa.​—Isaya 25:8.

  • atawaona wapendwa wake wakifufuliwa, na kuishi duniani.​—Yohana 5:28, 29.

  • atafurahia kuwa na afya nzuri na nguvu za ujana.​—Ayubu 33:25.

  • atasumbuliwa na mawazo au kumbukumbu mbaya.​—Isaya 65:17.

5. Tumaini la Biblia linaweza kubadili maisha yako

Watu wengi huvunjika moyo au kukasirika kwa sababu ya matatizo wanayokabili. Wengine hujitahidi sana kuleta mabadiliko. Ona jinsi ahadi ya Biblia kwamba hali zitabadilika inavyowasaidia watu leo. Onyesha VIDEO, kisha mzungumzie maswali haya:

  • Katika video hiyo, ni ukosefu gani wa haki ambao ulimhangaisha Rafika?

  • Ingawa ukosefu wa haki alioona haukwisha, Biblia ilimsaidiaje?

Biblia inatupatia tumaini la wakati ujao ambalo linatusaidia kuwa na furaha na kutovunjika moyo ingawa tuna matatizo. Soma Methali 17:22 na Waroma 12:12, kisha mzungumzie maswali haya:

  • Je, unafikiri tumaini ambalo Biblia inatupatia linaweza kubadili maisha yako sasa? Kwa nini?

WATU FULANI HUSEMA: “Ahadi za Biblia kuhusu wakati ujao ni mambo ya kuwaziwa tu.”

  • Kwa nini unapaswa kuchunguza uthibitisho?

MUHTASARI

Biblia inatupatia tumaini zuri la wakati ujao ambalo hutusaidia kukabiliana na matatizo.

Ungejibuje?

  • Kwa nini watu wanahitaji tumaini?

  • Biblia inaahidi nini kuhusu wakati ujao?

  • Tumaini la wakati ujao linaweza kukusaidiaje sasa?

Lengo

CHUNGUZA ZAIDI

Jifunze jinsi tumaini linavyoweza kukusaidia kukabiliana na matatizo.

“Tumaini​—Je, Linaweza Kutusaidia?” (Amkeni!, Aprili 22, 2004)

Ona jinsi ambavyo tumaini la wakati ujao limewasaidia watu wenye magonjwa ya kudumu.

“Je, Biblia Inaweza Kunisaidia Ikiwa Nina Ugonjwa wa Kudumu?” (Makala iliyo kwenye mtandao)

Unapotazama video hii ya muziki, jiwazie wewe na familia yako mkifurahia maisha katika Paradiso ya wakati ujao iliyoahidiwa katika Biblia.

Wazia Maisha Paradiso (3:37)

Soma jinsi maisha ya mwanaharakati wa masuala ya kijamii yalivyobadilika alipojifunza kuhusu tumaini la wakati ujao ambalo linapatikana katika Biblia.

“Sitamani Tena Kuubadili Ulimwengu” (Mnara wa Mlinzi, Julai 1, 2013)