Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 KICHWA KIKUU: JE, UNAPASWA KUOGOPA MWISHO WA ULIMWENGU?

Mwisho wa Ulimwengu—Hofu, Msisimuko, na Kuvunjika Moyo

Mwisho wa Ulimwengu—Hofu, Msisimuko, na Kuvunjika Moyo

Unahisije kuhusu Desemba 21, 2012, tarehe iliyo katika kalenda ya Wamaya ambayo watu wengi wamedai kwamba ingeleta mabadiliko makubwa ulimwenguni? Ikitegemea ulichokuwa ukitazamia, huenda umepata kitulizo, umevunjika moyo, au umekata tamaa. Je, ni utabiri mwingine usio sahihi kuhusu mwisho wa ulimwengu?

Vipi kuhusu “mwisho wa dunia” unaotajwa katika Biblia? (Mathayo 24:3, Zaire Swahili Bible) Watu fulani wanahofu kwamba dunia itachomwa kwa moto. Na wengine wanatamani sana kuona mambo yatakayotokea wakati huo wa mwisho. Watu wengi wamechoka kuambiwa kwamba mwisho uko karibu. Lakini je, hizo zinaweza kuwa hisia zinazosababishwa na hadithi za kutungwa wala si mambo halisi?

Huenda ukashangazwa kujifunza mambo ambayo Biblia inasema kuhusu mwisho wa ulimwengu. Biblia inatupa sababu za kutazamia kwa hamu mwisho huo na pia inaeleza kwamba huenda watu fulani wakahisi kuwa mwisho unakawia na wakachoka kusubiri. Tunakutia moyo uchunguze majibu ya Biblia ya maswali fulani kuhusu mwisho wa ulimwengu.

 Je, dunia itachomwa moto?

JIBU LA BIBLIA: [Mungu] ameiwekea dunia msingi juu ya mahali pake palipofanywa imara; haitatikiswa mpaka wakati usio na kipimo, au milele.”ZABURI 104:5.

Dunia haitaharibiwa kwa moto au kwa njia nyingine yoyote. Badala yake Biblia inafundisha kwamba dunia ni makao ya milele ya wanadamu. Andiko la Zaburi 37:29 linasema: “Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.”—Zaburi 115:16; Isaya 45:18.

Baada ya Mungu kuumba dunia, alisema kwamba ‘ilikuwa nzuri sana,’ na bado anahisi hivyo. (Mwanzo 1:31) Badala ya kuiharibu, anaahidi “kuwaharibu wale wanaoiharibu dunia,” na atailinda isiharibiwe kabisa.—Ufunuo 11:18.

Hata hivyo, huenda ukashangazwa na maneno ya 2 Petro 3:7. Andiko hilo linasema: “Mbingu na dunia za sasa zimewekwa akiba kwa ajili ya moto.” Je, andiko hilo halionyeshi kwamba dunia itachomwa kwa moto? Nyakati fulani Biblia hutumia maneno “mbingu,” “dunia,” na “moto” kwa njia ya mfano. Kwa mfano, andiko la Mwanzo 11:1 linaposema: “Dunia yote iliendelea kuwa na lugha moja,” linatumia neno “dunia” kumaanisha wanadamu.

Mistari inayotangulia andiko la 2 Petro 3:7 inaonyesha kwamba maneno mbingu, dunia, na moto yametajwa kwa njia ya mfano. Mistari ya  5 na 6 inalinganisha na wakati wa Gharika ya siku za Noa. Wakati huo, ulimwengu wa kale uliangamizwa lakini sayari yetu haikuangamia. Badala yake, Gharika ilifagilia mbali wanadamu wenye jeuri, au “dunia.” Pia, iliharibu “mbingu” ya mfano, yaani, watu waliotawala duniani. (Mwanzo 6:11) Katika njia hiyohiyo, andiko la 2 Petro 3:7 linatabiri uharibifu wa wanadamu waovu pamoja na serikali zao zenye ufisadi kwa njia ya moto.

Ni nini kitakachotokea kwenye mwisho wa ulimwengu?

JIBU LA BIBLIA: Ulimwengu unapitilia mbali na pia tamaa yake, lakini yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.”1 YOHANA 2:17.

“Ulimwengu” utakaopitilia mbali, si dunia, bali ni wanadamu ambao hawaishi kupatana na mapenzi ya Mungu. Kama vile tu daktari anavyoweza kufanya upasuaji na kuondoa uvimbe unaosababisha kansa ili kuokoa uhai, Mungu  ‘atawakatilia mbali’ watu waovu ili watu wazuri wafurahie kweli kweli kuishi duniani. (Zaburi 37:9) Kwa njia hiyo, “mwisho wa ulimwengu” utakuwa jambo zuri.

Mtazamo kama huo unaofaa kuhusu “mwisho wa ulimwengu” unaonyeshwa na tafsiri za Biblia, ambazo zinatafsiri maneno hayo kuwa “umalizio wa mfumo wa mambo” au “mwisho wa nyakati.” (Mathayo 24:3; New International Version) Kwa kuwa dunia na wanadamu fulani wataokoka mwisho, je, si jambo linalopatana na akili kusema kwamba kuna nyakati mpya, mfumo mpya wa mambo, utakaofuata? Biblia inajibu ndiyo, kwa sababu inataja kuhusu “mfumo wa mambo unaokuja.”—Luka 18:30.

Yesu alisema wakati huo ujao ni kipindi cha “kugeuzwa upya kwa kila kitu.” Wakati huo, atawarudishia wanadamu hali ambayo Mungu alikusudia mwanzoni. (Mathayo 19:28, NIV) Kisha tutafurahia

Ikiwa tutafanya “mapenzi ya Mungu,” yaani, mambo anayotaka tufanye, hatutaogopa mwisho wa ulimwengu. Badala yake, tutatazamia kwa hamu mwisho huo.

Je, kweli mwisho wa ulimwengu uko karibu?

JIBU LA BIBLIA: Wakati mnapoona mambo hayo yakitukia, jueni kwamba ufalme wa Mungu uko karibu.”LUKA 21:31.

Katika kitabu The Last Days Are Here Again, Profesa Richard Kyle aliandika kwamba “badiliko la ghafla na misukosuko ya kijamii inatokeza hali inayofaa kwa watu kutoa matabiri ya mwisho wa ulimwengu.” Inakuwa hivyo hasa inapokuwa vigumu kufafanua mabadiliko na misukosuko hiyo.

Hata hivyo, manabii wanaotajwa katika Biblia hawakuandika kuhusu mwisho ili kueleza mambo mabaya yaliyokuwa yakitukia katika siku zao. Badala yake, waliongozwa na Mungu kueleza hali ambazo zingeonyesha kwamba mwisho wa ulimwengu unakaribia. Fikiria baadhi ya unabii huo kisha ujiamulie mwenyewe ikiwa unatimizwa wakati huu wetu.

Kama Yesu alivyosema, tunapoona “mambo yote hayo” tunapaswa kujua kwamba mwisho wa ulimwengu uko karibu. (Mathayo 24:33) Mashahidi wa Yehova wanaamini kwamba uthibitisho huo ni hakika, na wanashiriki imani yao na wengine kwa kuhubiri katika nchi 236.

Je, matazamio ya kimakosa kuhusu mwisho yanamaanisha kwamba hautakuja kamwe?

JIBU LA BIBLIA: “Wakati watakapokuwa wakisema: ‘Amani na usalama!’ ndipo uharibifu wa ghafula utakapokuwa juu yao mara moja kama vile maumivu ya taabu juu ya mwanamke mwenye mimba; nao hawataponyoka hata kidogo.”1 WATHESALONIKE 5:3.

Biblia inafananisha kuharibiwa kwa ulimwengu na mwanzo wa uchungu—maumivu ya mwanamke mwenye mimba hayaepukiki na huja ghafla. Kipindi kinachotangulia mwisho kinafananishwa na mimba, mwanamke mwenye mimba hujua kuongezeka kwa dalili za kujifungua. Daktari wake anaweza kutabiri siku ya kujifungua, hata ikiwa tukio hilo linaweza kuchelewa, bado anaweza kuwa na uhakika kwamba mtoto wake atazaliwa karibuni. Vivyo hivyo, matazamio ya kimakosa ya mwisho hayabadili matukio yaliyotabiriwa yanayothibitisha kwamba hizi ni “siku za mwisho.”—2 Timotheo 3:1.

Huenda ukajiuliza, ‘Ikiwa ishara zinazoonyesha kwamba mwisho umekaribia zinaonekana wazi, kwa nini watu wengi hawazitambui?’ Biblia inasema kwamba mwisho utakapokaribia, watu wengi watapuuza uthibitisho huo. Badala ya kutambua mabadiliko muhimu katika siku za mwisho,  wangedhihaki na kusema: “Tangu siku mababu zetu walipolala katika kifo, mambo yote yanaendelea sawasawa kama tangu mwanzo wa uumbaji.” (2 Petro 3:3, 4) Kwa maneno mengine, ni kwamba ishara za siku za mwisho zinaonekana wazi, lakini wengi wanazipuuza.—Mathayo 24:38, 39.

Makala hii imechunguza baadhi ya uthibitisho wa Biblia unaoonyesha kwamba mwisho umekaribia. * Je, ungependa kujifunza mengi zaidi? Ikiwa ndivyo, kwa nini usiwasiliane na Mashahidi wa Yehova na ukubali wakufundishe Biblia bila malipo? Wanaweza kuja kujifunza nawe nyumbani kwako, au mahali pengine popote panapofaa, au kupitia simu. Unachohitaji kutoa ni wakati wako, nawe utafaidika sana.

^ fu. 39 Ili upate habari zaidi, ona sura ya 9, “Je, Tunaishi Katika ‘Siku za Mwisho’?,” kwenye kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.