Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuwafundisha Watoto Kutimiza Madaraka Yao

Kuwafundisha Watoto Kutimiza Madaraka Yao

Siri ya Furaha ya Familia

Kuwafundisha Watoto Kutimiza Madaraka Yao

George: * “Jambo hilo lilitukia kila jioni. Michael, mwana wangu mwenye umri wa miaka minne, aliacha vitu vyake vya kuchezea vikiwa vimetapakaa kila mahali katika nyumba. Nilijaribu kumwambia avikusanye kabla ya kwenda kulala. Lakini Michael alikuwa akikasirika, anapiga mayowe na kutenda bila adabu. Nyakati nyingine nilikuwa nikikasirika sana na kumzomea, lakini hilo lilifanya sote wawili tuhisi vibaya. Nilitaka wakati wa kulala uwe kipindi cha furaha. Kwa hiyo, niliacha kumlazimisha na nikaanza kuvikusanya vitu hivyo mimi mwenyewe.”

Emily: “Tatizo lilianza wakati Jenny, binti yangu mwenye umri wa miaka 13, alipokosa kuelewa jinsi mwalimu wake alivyotaka afanye kazi yake ya shule. Jenny alilia kwa saa moja aliporudi nyumbani kutoka shuleni. Nilimtia moyo aombe msaada shuleni, lakini Jenny alisisitiza kwamba mwalimu wake alikuwa mkali, na hivyo aliogopa kuzungumza naye. Nilifikiria kwenda shuleni nikiwa nimekasirika na kumwambia mwalimu huyo jinsi nilivyohisi kumhusu. Nilihisi kwamba hakuna mtu ambaye alikuwa na haki ya kumkasirisha mtoto wangu!”

JE, HALI yako ni kama ya George na Emily? Kama wazazi hao, wengi wanaona kwamba ni vigumu kumtazama mtoto akipambana na tatizo au akikosa furaha. Ni jambo la kawaida kwa wazazi kujaribu kuwalinda watoto wao. Hata hivyo, hali zilizotajwa hapo juu ziliwapa wazazi hao nafasi ya kuwafundisha watoto wao somo la maana kuhusu kutimiza madaraka yao. Bila shaka, mambo ambayo mtoto wa umri wa miaka 4 anaweza kujifunza ni tofauti na yale ambayo mtoto wa umri wa miaka 13 anaweza kujifunza.

Hata hivyo, ukweli ni kwamba sikuzote hutakuwapo ili kuwakinga watoto wako wasipate matatizo maishani. Mwishowe, mtoto atamwacha baba na mama yake na “ataubeba mzigo wake mwenyewe” wa madaraka. (Wagalatia 6:5; Mwanzo 2:24) Ili watoto wajue jinsi ya kutimiza madaraka yao, lazima wazazi wakazie fikira mradi wa kuwafundisha wasiwe na ubinafsi, wawe wenye kujali, na wawe watu wazima wanaotimiza madaraka yao. Hiyo si kazi rahisi!

Inapendeza kwamba wazazi wanaweza kuiga mfano mzuri wa Yesu na jinsi alivyoshughulika na wanafunzi wake. Yesu hakuwa mzazi. Lakini alipowachagua na kuwazoeza wanafunzi wake, alikuwa na kusudi la kuwawezesha kuendelea na kazi hiyo, hata baada ya yeye kuondoka. (Mathayo 28:19, 20) Yesu alitimiza kusudi ambalo kila mzazi anatazamia kufikia, yaani, kuwalea watoto wanaoweza kutimiza madaraka yao. Chunguza mambo matatu tu ambayo katika hayo Yesu aliwawekea wazazi mfano.

‘Mwekee Kielelezo’ Mtoto Wako Karibu mwisho wa maisha yake, Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Niliweka kielelezo kwa ajili yenu, ili, kama vile nilivyowafanyia ninyi, ninyi pia mfanye hivyo.” (Yohana 13:15) Vivyo hivyo, wazazi wanahitaji kuwaeleza watoto na kuwaonyesha kupitia mfano wao maana ya kutimiza madaraka yao.

Jiulize hivi: ‘Je, mara kwa mara ninazungumza inavyofaa kuhusu kutimiza madaraka yangu? Je, ninazungumza kuhusu furaha ninayopata ninapojitahidi kuwasaidia wengine? Au je, mara nyingi ninalalamika na kujilinganisha na watu ambao wanaonekana hawana shughuli nyingi?’

Ni kweli kwamba hakuna mtu aliye mkamilifu. Nyakati nyingine sote tunahisi tumelemewa. Lakini huenda mfano wako ndilo jambo la maana zaidi ambalo linaweza kuwasaidia watoto wako waone kwa nini kutimiza madaraka yao ni zoea la maana na lenye faida.

JARIBU KUFANYA HIVI: Ikiwezekana, pindi nyingine nenda pamoja na mtoto wako kazini na umwonyeshe kazi unayofanya ili kuitegemeza familia kifedha. Msaidie mtu anayehitaji msaada ukiwa pamoja na mtoto wako. Baadaye, zungumzia jinsi ulivyofurahia kutimiza daraka hilo.—Matendo 20:35.

Uwe na Usawaziko Kuhusu Mambo Unayotaka Watimize Yesu alitambua kwamba muda ulihitajiwa ili wanafunzi wake wawe tayari kutimiza madaraka na majukumu aliyotaka watimize. Pindi moja aliwaambia hivi: “Bado nina mambo mengi ya kuwaambia, lakini hamwezi kuyastahimili kwa sasa.” (Yohana 16:12) Yesu hakuwaambia wanafunzi wake waanze papo hapo kufanya jambo fulani peke yao. Badala yake, alitumia muda mwingi kuwafundisha mambo mengi. Yesu aliwatuma wanafunzi wake wakiwa peke yao wakati tu alipoona kwamba wako tayari.

Vivyo hivyo, ni jambo lisilopatana na akili kwa wazazi kuwaomba watoto wao watimize madaraka ya watu wazima kabla hawajakuwa tayari. Hata hivyo, watoto wanapoendelea kukua, wazazi wanapaswa kuamua kazi na madaraka ambayo watoto wao wanaweza kutimiza. Kwa mfano, wazazi wanapaswa kuwafundisha watoto wao kutunza usafi wao wa kibinafsi, kusafisha vyumba vyao, kutunza wakati, na kutumia pesa kwa hekima. Mtoto anapoanza kwenda shuleni, wazazi wanapaswa kumfundisha kuona kazi ya shuleni kuwa daraka la maana ambalo ni lazima atimize.

Wazazi wanahitaji kufanya mengi zaidi ya kumpa mtoto wao madaraka ya kutimiza. Ni lazima pia wamsaidie mtoto anapojitahidi kufaulu. George, baba aliyetajwa mwanzoni, alitambua kwamba sababu moja iliyomfanya Michael akasirike sana alipoambiwa akusanye vitu vyake vya kuchezea ni kwamba aliona kazi hiyo kuwa ngumu sana. George anasema hivi: “Badala ya kumzomea tu Michael akusanye vitu vyake vya kuchezea, nilijaribu kumfundisha utaratibu fulani wa kufanya kazi hiyo.”

Alifanya nini hasa? George anasema, “Kwanza niliweka wakati hususa wa kukusanya vitu vya kuchezea kila jioni. Kisha, tulishirikiana na Michael kukusanya vitu hivyo hatua kwa hatua. Nilifanya kazi hiyo iwe kama mchezo, tukaanza kushindana ili kuona ni nani ambaye angekusanya vitu hivyo haraka zaidi. Baada ya muda mfupi, tulizoea kufanya hivyo kabla ya kulala. Nilimwahidi Michael kwamba ikiwa angefanya kazi hiyo haraka ningemsomea hadithi moja ya ziada kabla ya kulala. Lakini ikiwa angefanya kazi hiyo polepole, ningefupisha kipindi cha hadithi.”

JARIBU KUFANYA HIVI: Chunguza kazi ambayo kila mtoto anaweza kufanya ambayo itarahisisha kazi za nyumbani. Jiulize hivi: ‘Je, bado kuna mambo ambayo ninawafanyia watoto wangu ambayo wanaweza kujifanyia?’ Ikiwa ndivyo, fanya kazi pamoja na watoto wako mpaka uwe na hakika kwamba wanaweza kufanya kazi hiyo wakiwa peke yao. Waeleze waziwazi kwamba watapata matokeo mazuri au mabaya ikitegemea jinsi watakavyofanya kazi waliyopewa. Kisha, uwaadhibu au uwape zawadi baada ya kazi yao.

Toa Maagizo Hususa Kama vile kila mwalimu mzuri anavyojua, Yesu pia alijua kwamba njia bora ya kujifunza jambo fulani ni kulifanya. Kwa mfano, Yesu alipohisi kwamba wakati ulikuwa umefika, aliwatuma wanafunzi wake “wawili-wawili, wamtangulie kuingia katika kila jiji na mahali ambako yeye mwenyewe alikuwa aende.” (Luka 10:1) Hata hivyo hakuwaacha bila maagizo. Kabla ya kuwatuma, aliwapa maagizo hususa kabisa. (Luka 10:2-12) Wanafunzi waliporudi na kuripoti jinsi walivyofanikiwa, Yesu aliwapongeza na kuwatia moyo. (Luka 10:17-24) Aliwaonyesha kwamba alikuwa na hakika wangefanya kazi hiyo na kwamba wanastahili.

Unatenda jinsi gani watoto wako wanapopata madaraka mazito? Je, unajaribu kuwakinga watoto wako kutokana na mambo wanayoogopa ili wasivunjike moyo na kushindwa kutimiza mambo hayo? Mwanzoni huenda ukaona kwamba inafaa “kumwokoa” mtoto wako au kubeba mzigo huo wewe mwenyewe.

Lakini fikiria jambo hili: Kila mara unapokimbilia “kuwaokoa” watoto wako kwa njia fulani, unawafundisha jambo gani? Je, unawaonyesha kwamba una hakika nao na unaamini kwamba wana uwezo wa kufanya mambo? Au je, unawaonyesha kwamba bado wao ni watoto wachanga wasio na uwezo, na ambao lazima wakutegemee katika kila jambo?

Kwa mfano, Emily aliyetajwa mwanzoni alishughulikia jinsi gani tatizo la binti yake? Badala ya kuingilia kati, aliamua kumwacha Jenny azungumze moja kwa moja na mwalimu wake. Emily pamoja na Jenny waliandika orodha ya maswali ambayo Jenny angeenda nayo shuleni. Kisha wakazungumza kuhusu wakati unaofaa wa kuzungumza na mwalimu. Hata walifanya mazoezi kuhusu mazungumzo hayo. Emily anasema hivi: “Jenny alijipatia ujasiri wa kuzungumza na mwalimu wake, na mwalimu akampongeza kwa kuchukua hatua hiyo. Jenny alifurahi sana kutimiza jambo hilo, na mimi pia nilifurahishwa naye.”

JARIBU KUFANYA HIVI: Andika tatizo ambalo sasa linamhangaisha mtoto wako. Kando ya tatizo hilo, andika jambo ambalo unaweza kufanya ili kumsaidia mtoto wako akabiliane na tatizo hilo bila wewe “kumwokoa.” Fanya mazoezi pamoja na mtoto wako kuhusu hatua anazopaswa kuchukua ili kushinda tatizo hilo. Onyesha una hakika kwamba mtoto wako anaweza kukabiliana na tatizo hilo.

Ikiwa sikuzote unawakinga watoto wako kutokana na matatizo, huenda ukafanya wasiwe na uwezo wa kukabiliana na matatizo maishani. Badala yake, waimarishe watoto wako kwa kuwazoeza kutimiza madaraka yao. Hiyo ni moja kati ya zawadi zenye thamani zaidi ambazo unaweza kuwapa watoto wako.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

JIULIZE . . .

▪ Je, nina usawaziko kuhusu mambo ninayotazamia watoto wangu watimize?

▪ Je, ninawaambia na pia kuwaonyesha mambo wanayohitaji kufanya ili wafanikiwe?

▪ Ni muda gani ambao umepita tangu nilipomtia moyo au kumpongeza mtoto wangu?