Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | WAZAZI

Umuhimu wa Kazi za Nyumbani

Umuhimu wa Kazi za Nyumbani

CHANGAMOTO

Katika baadhi ya familia watoto wanatarajiwa wasaidie kufanya kazi za nyumbani, nao hufanya hivyo bila kulalamika. Katika familia nyingine, wazazi wamepuuza jambo hilo na watoto wanafurahi kwamba hawapewi kazi.

Watafiti wameona kwamba hali hiyo imeenea sana katika nchi za Magharibi, ambako watoto wanaonwa kuwa watumiaji badala ya kuwa watoaji. Mzazi anayeitwa Steven alisema hivi: “Leo, watoto huachwa wacheze michezo ya video, watumie Intaneti, na kutazama televisheni. Wanatarajiwa kufanya mambo machache sana.”

Wewe una maoni gani? Je, kweli kazi za nyumbani ni muhimu ili kudumisha hali nzuri ya nyumba na vilevile katika ukuzi wa mtoto?

MAMBO UNAYOHITAJI KUJUA

Baadhi ya wazazi husita kuwapatia watoto wao kazi za nyumbani, hasa ikiwa tayari ratiba ya juma ya mtoto ina mambo mengi kama vile kazi za shuleni na utendaji wa baada ya shule. Hata hivyo, fikiria faida za kufanya kazi za nyumbani.

Kazi za nyumbani huchangia ukuzi wa mtoto. Haishangazi kwamba mtoto anayeshiriki kufanya kazi za nyumbani ana uwezekano mkubwa wa kufanya vizuri shuleni. Kufanya kazi za nyumbani humsaidia mtoto ajiamini, awe na nidhamu, na kuwa na msimamo thabiti, sifa ambazo ni muhimu katika kujifunza.

Kazi za nyumbani huwaandaa watoto kuwatumikia wengine. Wengine wameona kwamba watoto wanaokuwa na kawaida ya kusaidia kazi za nyumbani wana mwelekeo mkubwa wa kushiriki kazi za kusaidia jamii wanapokuwa watu wazima. Hilo halishangazi kwa kuwa kazi za nyumbani huwazoeza kutanguliza mahitaji ya wengine kuliko mahitaji yao. Kwa upande mwingine, Steven, aliyenukuliwa awali alisema hivi: “Ikiwa hakuna jambo lolote linalotarajiwa kutoka kwao, watoto wanajua kwamba wao wapo ili wahudumiwe, hivyo, wanakua wakiwa na mawazo yaliyopotoka kwamba hawana majukumu na hawahitaji kufanya kazi kwa bidii.”

Kazi za nyumbani huchangia umoja wa familia. Wanapojitahidi kufanya kazi za nyumbani, watoto hutambua kwamba mbali na wao kuwa na thamani katika familia, wana daraka la kutimiza. Watoto wanaweza kushindwa kujifunza jambo hilo ikiwa wazazi watakazia mno utendaji wa baada ya shule kuliko kazi za nyumbani. Jiulize hivi, ‘Kuna faida gani ikiwa mtoto atakuwa na uhusiano mzuri na timu yake ya mpira lakini hana uhusiano na familia?’

MAMBO UNAYOWEZA KUFANYA

Anza kuwazoeza tangu wakiwa wachanga. Baadhi ya watu husema kwamba wazazi wanaweza kuwapa watoto kazi za nyumbani wanapofikisha umri wa miaka mitatu. Wengine wanapendekeza miaka miwili au chini ya hapo. Wazo ni hili, watoto wachanga wanapenda kufanya kazi pamoja na wazazi wao na kuwaiga.—Kanuni ya Biblia: Methali 22:6.

Wape kazi kulingana na umri wao. Kwa mfano, mtoto mwenye umri wa miaka mitatu anaweza kusaidia kuokota midoli, kusafisha madoa, au kutenganisha nguo zinazohitaji kufuliwa. Watoto wenye umri mkubwa wanaweza kufagia, kuosha gari, na kuandaa chakula. Wape kazi kulingana na uwezo wao. Utashangaa jinsi watakavyofurahia kufanya kazi hizo.

Tanguliza kazi za nyumbani. Inaweza kuwa vigumu kufanya hivyo ikiwa mtoto wako ana kazi nyingi za shuleni ambazo anafanyia nyumbani. Hata hivyo, kitabu The Price of Privilege kinasema kwamba kumwondolea kazi zote za nyumbani ili apate maksi nzuri ni “ishara ya kutanguliza mambo yasiyofaa.” Kama ilivyoelezwa mapema, kufanya kazi za nyumbani kunawasaidia watoto wawe wanafunzi bora. Na mazoezi hayo wanayojifunza yatawasaidia wakati ujao watakapokuwa na familia zao.—Kanuni ya Biblia: Wafilipi 1:10.

Kazia lengo badala ya matokeo. Huenda mtoto akachukua muda mrefu zaidi kumaliza kazi kuliko vile ulivyotazamia. Inaelekea pia ubora wa kazi hautakuwa kama unavyotaka. Hali hiyo inapojitokeza, epuka mwelekeo wa kuchukua kazi na kuifanya mwenyewe. Lengo lako si kwamba kazi ifanywe kwa ubora kama ambavyo ingefanywa na mtu mzima, bali ni kumsaidia mtoto ajifunze majukumu na kupata shangwe inayotokana na kufanya kazi.—Kanuni ya Biblia: Mhubiri 3:22.

Kazia thawabu kuu. Baadhi ya watu husema kwamba kumlipa mtoto ili afanye kazi za nyumbani humsaidia kuwa mwenye kutegemeka. Wengine husema kwamba kumpa pesa kunamfanya mtoto akazie fikira kile anachopata kutoka katika familia badala ya kile anachochangia. Pia, wanaonya kwamba mtoto anaweza kukataa kazi za nyumbani anapokuwa na pesa za kutosha, ishara ya kwamba kusudi la kazi za nyumbani limepotea. Tunajifunza nini? Tunajifunza kwamba ni vizuri mtoto ajue kwamba pesa unazompa si malipo ya kazi za nyumbani anazofanya.