Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Walijitoa Wenyewe kwa Hiari Nchini Norway

Walijitoa Wenyewe kwa Hiari Nchini Norway

MIAKA michache iliyopita, Roald na Elsebeth, wenzi wa ndoa wenye umri wa miaka karibu 50, waliishi maisha mazuri katika mji wa Bergen ambao ni mji wa pili kwa ukubwa nchini Norway. Walishiriki kwa uaminifu katika utendaji wa kutaniko hilo pamoja na binti yao Isabel na mwana wao Fabian. Roald alitumikia akiwa mzee na Elsebeth akiwa painia, nao Isabel na Fabian walikuwa wahubiri wenye bidii.

Hata hivyo, mnamo Septemba 2009, familia hiyo iliamua kufanya jambo tofauti, yaani, kuhubiri kwa juma zima katika eneo la mbali. Kwa hiyo, Roald na Elsebeth pamoja na Fabian, aliyekuwa na umri wa miaka 18 wakati huo, walisafiri mpaka rasi ya Nordkyn katika jimbo la Finnmark, juu ya Mzingo wa Aktiki. Walihubiri katika kijiji cha Kjøllefjord, pamoja na ndugu na dada wengine waliokuja kuhubiri katika eneo hilo la mbali. Roald anakumbuka hivi: “Mwanzoni mwa juma hilo, niliridhika kwamba nilipanga mambo yangu ili niweze kushiriki katika utendaji huo wa pekee kwa juma zima.” Hata hivyo, katika juma hilo, Roald alitambua kwamba kulikuwa na uhitaji mkubwa sana wa wahubiri katika eneo hilo. Kwa nini alihisi hivyo?

 OMBI AMBALO HAKUTARAJIA

“Bila kutarajia,” anasema Roald, “Mario, painia anayetumikia huko Finnmark, alituuliza ikiwa tungependa kuhamia katika mji wa Lakselv ili kusaidia kutaniko la huko lenye wahubiri 23.” Roald alishangazwa sana na ombi hilo ambalo hakutarajia. Anaeleza hivi: “Mimi na Elsebeth tulikuwa tumezungumzia uwezekano wa kutumikia katika eneo lililokuwa na uhitaji mkubwa zaidi, lakini tungefanya hivyo baada ya watoto wetu kuanza kujitegemea.” Hata hivyo, kwa siku chache ambazo alihubiri katika eneo hilo la mbali, Roald aliona wazi kwamba watu walifurahia kujifunza kumhusu Yehova. Walihitaji msaada sasa, wala si baadaye. “Ombi hilo lilinisumbua sana dhamiri na kunikosesha usingizi kwa siku kadhaa,” akumbuka Roald. Baadaye Mario alimsafirisha Roald na familia yake hadi Lakselv, umbali wa kilomita 240 hivi upande wa kusini wa Kjøllefjord. Mario alitaka wageni hao wajionee kutaniko dogo lililo katika mji huo.

Huko Lakselv, Andreas, mmoja kati ya wazee wawili wa kutaniko hilo, aliwaonyesha wageni hao eneo na Jumba la Ufalme. Kutaniko liliwakaribisha kwa uchangamfu sana na kuwaeleza Roald na Elsebeth kwamba wangefurahia sana ikiwa familia yao ingehamia huko ili kusaidia katika kazi ya Ufalme. Huku akitabasamu, Andreas alisema kwamba tayari amewatafutia kazi Roald na Fabian! Roald na familia yake wangefanya nini?

WANGEFANYA UAMUZI GANI?

Mara moja Fabian alisema hivi: “Sitamani kuhamia hapa.” Hakufurahia wazo la kuwaacha rafiki zake wa karibu alioshirikiana nao tangu utotoni katika kutaniko la nyumbani kwao na pia wazo la kuishi katika mji mdogo. Pia, hakuwa amemaliza masomo yake ya kuwa fundi-umeme. Hata hivyo, wakati Isabel (aliyekuwa na umri wa miaka 21 wakati huo) alipoulizwa maoni yake kuhusu kuhamia katika eneo hilo, alisema hivi: “Hilo hasa ndilo jambo nililotamani kufanya!” Lakini, Isabel anaendelea kusema hivi: “Nilipofikiria kwa makini jambo hilo, nilijiuliza, ‘Je, hili ni wazo zuri kweli? Je, nitawakosa sana rafiki zangu? Je, nibaki tu katika kutaniko langu, mahali ambapo nimezoea na mambo ni rahisi?’” Naye Elsebeth aliitikiaje mwaliko huo? Anasema hivi: “Nilihisi kwamba Yehova ameipa familia yetu mgawo, lakini pia nilifikiria kuhusu nyumba yetu tuliyotoka tu kuirekebisha na vitu vyote vilivyomo tulivyokusanya kwa miaka 25.”

Elsebeth na Isabel

Juma hilo la pekee lilipoisha, Roald na familia yake walirudi Bergen, lakini waliendelea kuwafikiria ndugu na dada zao Wakristo walioko Lakselv, umbali wa kilomita 2,100 hivi. “Nilitoa sala nyingi kwa Yehova,” anasema Elsebeth, “na niliendelea kuwasiliana na marafiki tuliokutana nao. Tulitumiana picha na mambo yaliyoonwa.” Roald anasema hivi: “Nilihitaji wakati ili kukubali kuhamia eneo la mbali. Pia, ilinibidi kufikiria ikiwa tutaweza kujitegemeza kimwili. Tungepataje mahitaji ya msingi? Nilisali sana kwa Yehova na kuzungumza na familia yangu na ndugu wakomavu pia.” Fabian anakumbuka hivi: “Kadiri nilivyofikiria jambo hilo, ndivyo nilivyozidi kutambua kwamba sikuwa na sababu nzuri ya kukataa kuhama. Nilisali mara nyingi kwa Yehova, na pole kwa pole nikawa na tamaa yenye nguvu ya kuhama.” Namna gani Isabel? Ili ajitayarishe kuhama, alianza kufanya upainia katika mji wa kwao. Baada ya kupainia kwa miezi sita, wakati ambapo alitumia pia muda mwingi kujifunza Biblia kibinafsi, alihisi kwamba yuko tayari kuhamia mbali.

KUCHUKUA HATUA ILI KUFIKIA LENGO LAO

Tamaa ya kutumikia katika eneo lenye uhitaji mkubwa zaidi wa wahubiri ilipozidi kukua, familia hiyo ilichukua hatua ili kufikia lengo lao. Roald alikuwa na kazi yenye mshahara mnono aliyopenda sana, lakini akaomba likizo ya mwaka mmoja. Hata hivyo mwajiri wake alimwomba awe kama mfanyakazi wa muda, yaani, afanye kazi majuma mawili mfululizo, kisha apumzike kwa majuma sita. “Mshahara wangu ulipunguzwa sana, lakini mambo hayakuwa mabaya,” asema Roald.

Naye Elsebeth anasema hivi: “Mume wangu aliniomba nijaribu kutafuta nyumba huko Lakselv kisha tukodishe nyumba yetu iliyokuwa Bergen. Jambo hilo lilihitaji wakati na jitihada nyingi, hata hivyo tulifanikiwa. Punde si punde, watoto wetu walipata kazi za muda.” Anaongezea hivi: “Wanatusaidia kulipia gharama za chakula na usafiri.”

Isabel anasema: “Kwa kuwa tulihamia mji mdogo, tatizo langu kubwa lilikuwa kupata kazi itakayonisaidia kujitegemeza nikiwa painia. Nyakati nyingine, nilikata  tamaa.” Hata hivyo, kwa sababu Isabel alifanya kazi yoyote ya muda aliyopata, katika mwaka wa kwanza alifanya kazi tisa tofauti-tofauti na kwa njia hiyo akaweza kulipia gharama zake. Mambo yalimwendeaje Fabian? “Ili nimalize masomo yangu ya kuwa fundi-umeme, bado nilihitaji kupata mazoezi kwa muda fulani. Nilifanya hivyo huko Lakselv. Baadaye, nilifaulu mtihani na kupata kazi ya muda nikiwa fundi-umeme.”

JINSI WENGINE WALIVYOPANUA HUDUMA YAO

Marelius na mke wake, Kesia, walitaka pia kutumikia katika eneo lililokuwa na uhitaji mkubwa zaidi wa wahubiri. Marelius, aliye na umri wa miaka 29 anasema hivi: “Mahojiano na hotuba zilizotolewa kusanyikoni kuhusu upainia zilinichochea nifikirie kupanua huduma yangu.” Hata hivyo, Kesia, ambaye sasa ana umri wa miaka 26, hakutaka kuhamia mbali na familia yake. “Niliogopa kuishi mbali sana na watu ninaowapenda,” anasema Kesia. Kwa kuongezea, Marelius alifanya kazi ya wakati wote ili kulipia mkopo wa nyumba. Anasema hivi: “Kwa msaada wa Yehova na sala nyingi tulizotoa tukimwomba atusaidie kufanya mabadiliko, tulifaulu kuhama.” Kwanza, walitumia wakati mwingi zaidi kujifunza Biblia. Kisha, wenzi hao waliuza nyumba yao, wakaacha kazi zao za kuajiriwa, na mnamo Agosti 2011 wakahamia katika mji wa Alta, kaskazini mwa Norway. Ili kujitegemeza wakiwa mapainia, Marelius anafanya kazi ya uhasibu naye Kesia anafanya kazi katika duka.

Knut na Lisbeth, wenzi wa ndoa walio na umri wa miaka zaidi ya 30 waliguswa moyo sana na masimulizi ya Kitabu cha Mwaka kuhusu wale wanaotumikia katika maeneo yenye uhitaji mkubwa zaidi wa wahubiri wa Ufalme. Lisbeth anasema hivi: “Masimulizi hayo yalitufanya tufikirie kutumikia katika nchi ya kigeni, lakini nilisita kwa sababu nilikuwa na shaka ikiwa mtu wa kawaida kama mimi angeweza kufanya hivyo.” Hata hivyo, walichukua hatua ili kufikia lengo lao. Knut anasema hivi: “Tuliuza nyumba yetu, tukaamua kuishi na mama yangu ili tuweke pesa akiba. Baadaye, ili kujitayarisha kutumikia katika eneo la kigeni, tulihamia kutaniko la Kiingereza huko Bergen, ambako tuliishi na mama ya Lisbeth.” Baada ya muda mfupi, Knut na Lisbeth walikuwa tayari kufanya uamuzi mkubwa wa kuhamia nchini Uganda. Kila mwaka wanarudi Norway kwa miezi miwili ili kufanya kazi. Mpango huo unawasaidia kupata pesa za kutosha za kuwawezesha kuishi na kuhubiri kwa wakati wote nchini Uganda kwa miezi inayobaki.

“ONJENI MWONE YA KUWA YEHOVA NI MWEMA”

Elsebeth na Isabel

Watumishi hao waliojitolea kwa hiari walipata matokeo gani? Roald anasema hivi: “Tunatumia wakati mwingi zaidi pamoja tukiwa familia katika eneo hili la mbali kuliko tulivyofanya huko Bergen. Tumesitawisha uhusiano wa karibu zaidi katika familia yetu. Ni baraka kuona watoto wetu wakifanya maendeleo ya kiroho.” Anaongeza hivi: “Pia, sasa tuna maoni yenye  usawaziko kuelekea vitu vya kimwili. Vitu hivyo si vya maana sana kama tulivyofikiri mwanzoni.”

Elsebeth aliona uhitaji wa kujifunza lugha nyingine. Kwa nini? Eneo la Kutaniko la Lakselv linatia ndani kijiji cha Karasjok, katikati ya eneo la Wasami, ambao ni wenyeji wa majimbo ya kaskazini mwa Norway, Sweden, Finland, na Urusi. Ili iwe rahisi zaidi kuwahubiria wenyeji hao, Elsebeth alijifunza lugha ya Kisami. Sasa anaweza kuanzisha mazungumzo akitumia lugha hiyo. Je, anafurahia eneo lake jipya? Anasema hivi kwa shangwe: “Ninaongoza mafunzo sita ya Biblia. Singependa kuwa mahali pengine popote isipokuwa hapa!”

Fabian, anayetumikia sasa akiwa painia na mtumishi wa huduma, anasema kwamba yeye na Isabel waliwasaidia vijana watatu katika kutaniko lao jipya waliohitaji kuhimizwa kushiriki zaidi katika utendaji wa kutaniko. Sasa vijana hao watatu wanashiriki kwa bidii katika huduma. Kwa kuongezea, wawili kati yao wamebatizwa na walikuwa mapainia wasaidizi katika mwezi wa Machi 2012. Mmoja wa vijana hao aliyekuwa karibu kuacha kweli aliwashukuru Fabian na Isabel kwa kumsaidia “kupata tena nguvu za kiroho.” Fabian anasema hivi: “Niliguswa moyo sana dada huyo aliposema maneno hayo. Ni furaha kama nini kumsaidia mtu mwingine!” Isabel anasema hivi: “Katika mgawo huu, kwa kweli ‘nimeonja na kuona ya kuwa Yehova ni mwema.’” (Zab. 34:8) Anaongezea hivi: “Na zaidi ya hayo, ninafurahia sana kutumikia hapa!”

Sasa Marelius na Kesia wanaishi maisha rahisi lakini yenye kusudi zaidi. Kutaniko walilohamia la Alta sasa lina wahubiri 41. Marelius anasema hivi: “Ninapotazama nyuma, inatia moyo kuona jinsi ambavyo maisha yetu yamebadilika. Tunamshukuru Yehova kwamba tunaweza kumtumikia hapa tukiwa mapainia. Hakuna jambo lenye kuridhisha kuliko hilo.” Kesia anaongezea hivi: “Nilijifunza kumtegemea Yehova kikamili zaidi, naye ametutunza vizuri. Nimegundua pia kwamba kuishi mbali na watu wangu wa ukoo kunanisaidia kuthamini hata zaidi pindi tunazotumia pamoja nao. Sijawahi kamwe kujutia uamuzi wetu.”

Knut na Lisbeth wanaendeleaje nchini Uganda? Knut anasema: “Ilichukua muda kuzoea mazingira na utamaduni mpya. Mara kwa mara tunakosa maji, umeme, na tunakuwa na matatizo ya tumbo, lakini tunaongoza mafunzo mengi ya Biblia tunavyotaka!” Lisbeth anasema hivi: “Mwendo wa nusu saa tu kutoka mahali tunapoishi, kuna maeneo ambayo hayajawahi kamwe kufikiwa na habari njema. Isitoshe, katika maeneo hayo, tunawakuta watu wakisoma Biblia, na wanatuomba tuwafundishe. Ni furaha isiyo na kifani kuwafundisha watu hao wanyenyekevu ujumbe wa Biblia!”

Bila shaka, Kiongozi wetu, Kristo Yesu, akiwa mbinguni anafurahi sana kuona jinsi ambavyo kazi ya kuhubiri aliyoianzisha inavyofanywa katika sehemu nyingi zaidi za dunia! Naam, watu wote wa Mungu wanapata shangwe moyoni wanapojitoa wenyewe kwa hiari ili kutimiza amri ya Yesu ya ‘kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.’—Mt. 28:19, 20.