Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Walijitoa Wenyewe kwa Hiari​—Nchini Myanmar

Walijitoa Wenyewe kwa Hiari​—Nchini Myanmar

“MAVUNO ni mengi, lakini wafanyakazi ni wachache. Kwa hiyo mwombeni Bwana wa mavuno awatume wafanyakazi katika mavuno yake.” (Luka 10:2) Maneno hayo yaliyosemwa na Yesu miaka 2,000 hivi iliyopita, yanafafanua vizuri hali iliyopo nchini Myanmar. Kwa nini? Kwa sababu kuna wahubiri wapatao 4,200 tu nchini Myanmar wanaowatangazia watu milioni 55 habari njema.

Hata hivyo, Yehova, “Bwana wa mavuno,” amewachochea mamia ya ndugu na dada kutoka nchi mbalimbali, kuja katika nchi hii iliyopo Kusini-mashariki mwa bara la Asia ili kusaidia katika mavuno ya kiroho. Ni nini kilichowachochea wahame nchi zao? Ni nini kilichowasaidia kuhamia nchi nyingine? Na wanafurahia baraka gani? Acheni tuone.

“NJOONI, TUNAHITAJI MAPAINIA WENGI ZAIDI!”

Miaka kadhaa iliyopita, Kazuhiro, ndugu painia kutoka Japani, alishikwa na ugonjwa wa kifafa, akapoteza fahamu, na kupelekwa hospitalini. Daktari alimwambia asiendeshe gari kwa miaka miwili. Kazuhiro alishtuka. Alijiuliza hivi: ‘Nitawezaje kuendelea na upainia—jambo ninalopenda sana?’ Alisali kwa bidii akimsihi Yehova afungue njia ili aendelee na upainia.

Kazuhiro na Mari

Kazuhiro anaeleza hivi: “Mwezi mmoja baadaye, rafiki yangu aliyekuwa akitumikia Myanmar alipata habari kuhusu hali yangu. Alinipigia simu na kuniambia: ‘Hapa Myanmar watu wengi husafiri kwa basi. Ukihamia huku, unaweza kuendelea na utumishi wako na hutahitaji gari!’ Nilimuuliza daktari wangu ikiwa hali yangu inaweza kuniruhusu kuhamia Myanmar. Nilishangaa daktari aliponiambia hivi: ‘Daktari wa matatizo ya ubongo kutoka Myanmar ametembelea Japani kwa sasa. Nitakutambulisha kwake. Ukishikwa na kifafa tena, atakusaidia.’ Niliona maelezo hayo ya daktari kuwa jibu kutoka kwa Yehova.”

Mara moja, Kazuhiro alituma barua-pepe kwenye ofisi ya tawi ya Myanmar akieleza tamaa ambayo yeye na mke wake walikuwa nayo ya kutumikia katika nchi hiyo wakiwa mapainia. Siku tano tu baadaye, ofisi ya tawi ilijibu hivi: “Njooni, tunahitaji mapainia wengi zaidi!” Kazuhiro na mke wake, Mari, waliuza magari yao, wakapata visa, na kununua tiketi za ndege. Leo, wanafurahia kutumikia kwenye kikundi cha lugha ya ishara huko Mandalay. Kazuhiro anasema hivi: “Tunahisi kwamba mambo hayo yote tuliyojionea, yameimarisha imani yetu katika ahadi ya Mungu iliyo kwenye Zaburi 37:5: ‘Mkabidhi Yehova njia yako; mtegemee yeye, naye atatenda kwa niaba yako.’”

YEHOVA AFUNGUA NJIA

Katika mwaka wa 2014, Mashahidi wa Yehova nchini Myanmar walipata pendeleo la kuwa na kusanyiko la pekee nchini humo. Ndugu na dada kutoka nchi mbalimbali walihudhuria. Mmoja wao alikuwa Monique, dada mwenye umri wa miaka 34 kutoka Marekani. Anasema hivi: “Niliporudi nyumbani baada ya kusanyiko, nilisali kwa Yehova kuhusu hatua niliyopaswa kuchukua sasa. Pia, nilizungumza na wazazi wangu kuhusu malengo yangu ya kiroho. Sote tuliona kwamba ingefaa nirudi Myanmar. Lakini ilichukua muda na sala nyingi zilihusika kabla ya kufikia uamuzi wa kuhamia huko.” Monique anaeleza sababu.

Monique na Li

“Yesu aliwatia moyo wafuasi wake ‘wahesabu gharama.’ Hivyo, nilijiuliza: ‘Je, nina pesa za kutosha? Je, nitaweza kujitegemeza katika nchi hiyo na nisitumie muda mwingi kufanya kazi ya kimwili?’” Anakiri hivi: “Mara moja nilitambua kwamba sikuwa na pesa za kutosha ili kuhamia nchi hiyo ya mbali.” Hivyo basi, alifauluje kuhama?—Luka 14:28.

Monique anaeleza hivi: “Siku moja mwajiri wangu alitaka kuzungumza nami. Nilikuwa na wasiwasi nikifikiri kwamba alitaka kuniachisha kazi. Lakini badala yake alinishukuru kwa kazi yangu nzuri. Kisha akaniambia kwamba alikuwa amefanya mipango ili nipate malipo ya ziada. Nilishangaa kuona kwamba yalikuwa sawa na kiasi cha pesa nilichohitaji!”

Monique amekuwa akitumikia nchini Myanmar tangu Desemba 2014. Anahisije kuhusu huduma yake katika eneo hilo lenye uhitaji? Anasema hivi: “Ninafurahi sana kuwa hapa. Ninaongoza mafunzo matatu ya Biblia. Mmoja wa wanafunzi wangu ana umri wa miaka 67. Sikuzote yeye hunisalimu kwa kunikumbatia kwa uchangamfu na tabasamu. Alipojifunza kwamba jina la Mungu ni Yehova, alitokwa na machozi. Alisema hivi: ‘Hii ndiyo mara yangu ya kwanza kusikia kwamba Mungu anaitwa Yehova. Nimekuzidi umri sana, lakini kati ya mambo yote niliyowahi kujifunza maishani, hili ndilo jambo muhimu zaidi.’ Maneno yake yalinifanya mimi pia nitokwe na machozi. Kujionea mambo kama hayo, hufanya maisha kwenye eneo lenye uhitaji yawe yenye kuridhisha sana.” Hivi karibuni, Monique alipata pendeleo la kuhudhuria Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme.

Jambo lingine lililowachochea baadhi ya ndugu na dada wahamie Myanmar ni masimulizi kuhusu nchi hiyo yanayopatikana kwenye Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova cha 2013. Dada anayeitwa Li, mwenye umri wa miaka 30 na kitu tayari alikuwa akiishi Kusini mashariki mwa bara la Asia. Alikuwa na kazi ya kimwili ya wakati wote, lakini simulizi kuhusu nchi ya Myanmar katika Kitabu cha Mwaka lilimchochea ahamie huko. Anasema hivi: “Mwaka wa 2014 nilipohudhuria kusanyiko la pekee huko Yangon, nilikutana na wenzi fulani wa ndoa waliokuwa wakitumikia katika eneo lenye uhitaji la lugha ya Kichina nchini Myanmar. Kwa kuwa ninazungumza Kichina, niliamua kuhamia Myanmar ili kusaidia katika kikundi cha Kichina nchini humo. Tuliungana na Monique, na kuhamia Mandalay. Yehova alitubariki kwa kutusaidia kupata kazi ya muda ya kufundisha katika shule ileile, na nyumba ya kuishi karibu na shule hiyo. Licha ya kwamba kuna joto kali na shida za hapa na pale, ninafurahia utumishi wangu hapa. Watu wa Myanmar wanaishi maisha ya hali ya chini, lakini ni wenye heshima na wako tayari kutumia muda wao kusikiliza habari njema. Inafurahisha sana kuona jinsi Yehova anavyoharakisha kazi. Ninaamini kabisa kwamba ni mapenzi ya Yehova niendelee kuwa hapa hapa Mandalay.”

YEHOVA HUSIKIA SALA

Ndugu na dada kadhaa ambao wamehamia eneo lenye uhitaji wamejionea jinsi Yehova anavyojibu sala zao. Mfikirie Jumpei mwenye umri wa miaka 37, na Nao, mke wake, mwenye umri wa miaka 35. Tayari walikuwa wakitumikia kwenye kutaniko la lugha ya ishara nchini Japani. Kwa nini walihamia Myanmar? Jumpei anaeleza hivi: “Sikuzote mimi na mke wangu tulikuwa na lengo la kutumikia katika eneo lenye uhitaji kwenye nchi nyingine. Ndugu mmoja wa kutaniko letu la lugha ya ishara nchini Japani alihamia Myanmar. Ingawa tulikuwa na akiba ya pesa kidogo tu, Mei 2010 sisi pia tulihamia Myanmar. Ndugu na dada nchini humo walitukaribisha kwa uchangamfu!” Anahisije kuhusu kazi ya kuhubiri katika eneo la lugha ya ishara nchini Myanmar? Anaeleza hivi: “Watu wengi wanapendezwa. Tunapowaonyesha viziwi video za lugha ya ishara wanafurahi sana. Tunafurahi sana kwamba tuliamua kuja hapa ili kumtumikia Yehova!”

Nao na Jumpei

Jumpei na Nao wamejitegemezaje kifedha? Jumpei anaeleza hivi: “Baada ya miaka mitatu, akiba yetu ya pesa ilikuwa imepungua sana na hatukuwa na pesa za kutosha kulipia kodi ya nyumba ya mwaka uliofuata. Mimi na mke wangu tulisali kwa bidii sana. Bila kutarajia tulipokea barua kutoka ofisi ya tawi ikituomba tutumikie tukiwa mapainia wa pekee wa muda! Tulimtegemea Yehova, na tukajionea kwamba hakutuacha kamwe. Amekuwa akitutunza katika kila njia.” Hivi karibuni, Jumpei na Nao pia walihudhuria Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme.

YEHOVA AWACHOCHEA WENGI

Ni nini kilichomchochea Simone, ndugu mwenye umri wa miaka 43, mwenye asili ya Italia, na Anna, mke wake mwenye umri wa miaka 37, mwenye asili ya New Zealand, kuhamia Myanmar? Anna anaeleza hivi: “Ni simulizi la nchi ya Myanmar lililo katika Kitabu cha Mwaka cha 2013!” Simone anasema hivi: “Ni pendeleo kubwa kuwa nchini Myanmar. Gharama ya maisha iko chini, hivyo ninaweza kutumia muda mwingi zaidi kufanya kazi ya Yehova. Inasisimua kuona jinsi Yehova anavyotutunza tunapotumikia katika eneo hili lenye uhitaji.” (Zab. 121:5) Anna anaeleza hivi: “Nina furaha kuliko wakati mwingine wowote maishani. Tunaishi maisha rahisi. Ninatumia muda mwingi zaidi pamoja na mume wangu, na uhusiano wetu umeimarika. Tumepata pia marafiki wapya wazuri. Watu hawawachukii Mashahidi, na wanaitikia vizuri sana!” Katika njia zipi?

Simone na Anna

Anna anaeleza hivi: “Siku moja, nilimhubiria mwanafunzi mmoja wa chuo kikuu sokoni na nikapanga kukutana naye tena. Tulipokutana naye alikuwa pamoja na rafiki yake. Pindi iliyofuata alikuja na rafiki zake wengine. Mwishowe, alileta wengine zaidi. Sasa ninajifunza na watano kati yao.” Simone anaeleza hivi: “Watu tunaowahubiria ni wenye urafiki na wanataka kujua mengi. Wengi wanapendezwa. Kwa kweli, hatuna muda wa kutosha kuwarudia wote wanaopendezwa.”

Sachio na Mizuho

Lakini vipi kuhusu hatua ambazo ndugu na dada walihitaji kuchukua ili kufanya uamuzi wa kuhamia Myanmar? Mizuho kutoka Japani anaeleza hivi: “Mimi na Sachio, mume wangu, tulitamani sikuzote kutumikia katika nchi yenye uhitaji lakini hatukujua twende wapi. Baada ya kusoma simulizi kuhusu nchi ya Myanmar kwenye Kitabu cha Mwaka cha 2013, tuliguswa moyo sana na mambo yaliyoonwa hivi kwamba tulianza kufikiria uwezekano wa kutumikia katika nchi ya Myanmar.” Sachio anasema hivi: “Tuliamua kutembelea Yangon, jiji kuu la Myanmar kwa juma moja, ili kuelewa vizuri hali ya eneo hilo. Ziara hiyo fupi ilitusadikisha kwamba tunapaswa kuhamia huko.”

JE, UTAKUBALI MWALIKO?

Jane, Danica, Rodney, na Jordan

Rodney na Jane mke wake, kutoka Australia, wenye umri wa miaka 50 na kitu, pamoja na mwana wao Jordan, na binti yao Danica, wamekuwa wakitumikia kwenye eneo lenye uhitaji nchini Myanmar tangu mwaka wa 2010. Rodney anaeleza hivi: “Tunachochewa sana kuona jinsi watu walivyo na njaa ya kiroho. Ninapendekeza kwa moyo wote kwamba familia nyingine pia zijaribu kuhamia katika eneo lenye uhitaji kama vile Myanmar.” Kwa nini? “Uamuzi wetu wa kuhamia huku umeiletea familia yetu baraka tele za kiroho! Vijana wengi leo wamekengeushwa na simu, magari, kazi, na kadhalika. Watoto wetu wanatumia muda wao mwingi kujifunza maneno mapya watakayotumia katika huduma. Wanajitahidi kujifunza jinsi wanavyoweza kujadiliana na wale ambao hawaifahamu Biblia vizuri na jinsi ya kutoa maelezo kwenye mikutano, na wanajishughulisha na mambo mengine mengi ya kiroho yenye kufurahisha.”

Oliver na Anna

Oliver, ndugu mwenye umri wa miaka 37 kutoka Marekani, anaeleza kwa nini anawapendekezea wengine wajiunge na utumishi huo: “Kuacha maisha niliyokuwa nimezoea na kwenda kumtumikia Yehova mahali pengine kumeniletea faida nyingi. Kuhamia mbali na nyumbani kumenisaidia kuwa na ujasiri na kumtegemea Yehova hata nikabili hali ya aina gani. Kutumikia pamoja na ndugu na dada ambao sikuwajua hapo awali na ambao wana imani kama yangu, kumenisaidia sana kuona kwamba hakuna chochote katika ulimwengu huu kilicho muhimu kama Ufalme wa Mungu.” Leo, Oliver na Anna mke wake, wanaendelea kutumikia kwa bidii katika eneo la lugha ya Kichina.

Trazel

Trazel, dada mwenye umri wa miaka 52 kutoka Australia, amekuwa akitumikia nchini Myanmar tangu mwaka wa 2004. Anasema hivi: “Kwa wale ambao hali zao zinaruhusu, ninapendekeza kabisa kwamba watumikie kwenye eneo lenye uhitaji. Nimejionea kwamba ikiwa una nia ya kutumikia, Yehova hubariki jitihada zako. Sikuwahi kuwazia ningeishi maisha mazuri kama haya. Haya ndiyo maisha yenye kuthawabisha na yenye kuridhisha zaidi.”

Maneno hayo yenye kugusa moyo kutoka kwa ndugu na dada wanaotumikia kwenye eneo lenye uhitaji nchini Myanmar, na yakuchochee kufikiria jinsi unavyoweza kuwasaidia watu wenye mioyo minyoofu katika maeneo ambayo hayajahubiriwa. Naam, ndugu na dada hao wanatoa mwaliko huu, “Tafadhali, vuka uje Myanmar utusaidie!”