Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Walijitoa Wenyewe kwa Hiari Nchini Brazili

Walijitoa Wenyewe kwa Hiari Nchini Brazili

MIAKA mingi iliyopita, Rúbia (1), dada mwenye umri wa miaka 30 sasa, alifunga safari ya kumtembelea Sandra (2), painia anayetumika kwenye kutaniko dogo kusini mwa Brazili. Alipokuwa huko, jambo fulani lilitukia ambalo lilimvutia sana Rúbia hivi kwamba likabadili maisha yake. Ni jambo gani hilo? Acheni tusikie kutoka kwa Rúbia mwenyewe.

“SIKUAMINI NILICHOSIKIA”

“Tulienda na Sandra kumtembelea mwanamke mmoja aliyekuwa akijifunza naye Biblia. Wakati wa funzo, mwanamke huyo alisema hivi bila kufikiri: ‘Sandra, wasichana watatu kazini wanataka kujifunza Biblia, lakini niliwaambia kwamba watahitaji kusubiri mpaka zamu yao ifike. Ninajua kwamba huna nafasi ya kujifunza na mtu mwingine mwaka huu.’ Sikuamini nilichosikia. Watu waliotaka kumjua Yehova walihitaji kuwekwa katika orodha ya wale wanaosubiri kujifunza! Katika kutaniko la nyumbani, ilikuwa vigumu sana kwangu kupata hata funzo moja. Wakati huohuo, nikiwa katika nyumba ya mwanafunzi huyo wa Biblia, nilitamani sana kuwasaidia watu katika mji wao mdogo. Baada ya muda mfupi, nilihama jiji nilimokuwa nikiishi na kwenda katika mji ambamo Sandra alikuwa akifanya upainia.”

Rúbia alipata matokeo gani? Anasema: “Miezi miwili tu baada ya kuhamia huko, nilikuwa nikiongoza mafunzo 15 ya Biblia, na amini usiamini, baada ya muda mfupi tu, kama Sandra, mimi pia nikawa na orodha ya wale wanaosubiri kujifunza!”

ACHOCHEWA KUCHUNGUZA UPYA HUDUMA YAKE

Diego (3), ndugu ambaye sasa ana umri wa miaka 20 hivi, aliwatembelea mapainia ambao ni wenzi wa ndoa wanaotumika Prudentópolis, mji mdogo ulio kusini mwa Brazili. Ziara hiyo ilimgusa moyo sana; na ikamchochea kuichunguza upya huduma yake. Anaeleza hivi: “Nilikuwa nikishirikiana kidesturi tu na kutaniko la nyumbani kwetu, nikitumia saa chache kila mwezi katika huduma. Lakini nilipowatembelea mapainia hao na kusikiliza mambo yaliyoonwa waliyosimulia, nililazimika kulinganisha furaha waliyokuwa nayo na tabia yangu ya kutopendezwa na huduma. Nilipoona jinsi walivyokuwa na msisimko na furaha, nilitamani maisha yangu pia yawe yenye kusudi kama yao.” Baada ya ziara hiyo, Diego akaanza upainia.

Sawa na Diego, je, wewe ni kijana Shahidi anayeshiriki katika kazi ya kuhubiri na anayehudhuria mikutano ya Kikristo lakini bado unahisi kwamba huduma imekuwa ya kawaida tu, na haina msisimko? Ikiwa ni hivyo, je, unaweza kufanya mabadiliko maishani mwako yatakayokuwezesha kuonja shangwe inayopatikana kwa kutumikia mahali penye uhitaji mkubwa zaidi wa wahubiri wa Ufalme? Ukweli ni kwamba wazo la kuacha maisha ya starehe huenda linakutia hofu. Hata hivyo, vijana wengi wamechagua kufanya hivyo. Wameamua kuacha miradi na mapendezi yao ili kumtumikia Yehova kikamili zaidi. Fikiria pia mfano wa Bruno.

MWALIMU (MAESTRO) AU MHUDUMU?

Miaka mingi iliyopita, Bruno (4), ambaye sasa ana umri wa miaka 28, alisomea muziki katika shule maarufu ya muziki akiwa na mradi wa kuwa kiongozi wa okestra. Alifanya vizuri sana katika masomo yake hivi kwamba alialikwa ili kuongoza kikundi fulani cha okestra. Angepata kazi nzuri sana. Bruno anasema hivi: “Bado nilihisi kwamba nilikosa kitu fulani katika maisha yangu. Nilijiweka wakfu kwa Yehova, lakini nilijua kwamba sikuwa nikimtumikia kwa moyo wote, na hilo lilinisumbua. Nikamweleza Yehova kuhusu hisia zangu katika sala, na pia nikazungumza na ndugu wenye uzoefu kutanikoni. Baada ya kufikiria hilo kwa uzito, niliamua kuitanguliza huduma yangu badala ya muziki, nikaacha shule ya muziki, na kuamua kwenda kutumikia katika eneo lililokuwa na uhitaji mkubwa wa wahubiri wa Ufalme.” Uamuzi wake ulikuwa na matokeo gani?

Bruno alihamia katika mji wa Guapiara (wenye idadi ya watu 7,000 hivi), ulio umbali wa kilomita 260 hivi kutoka jiji la São Paulo. Lilikuwa badiliko kubwa sana. Anasema: “Nilihamia katika nyumba ndogo ambayo haikuwa na friji, televisheni, au Intaneti. Hata hivyo, nilipokuwa katika nyumba hiyo niliweza kuwa na bustani ya matunda na mboga, vitu ambavyo sikuwa navyo kamwe mwanzoni!” Alipokuwa akitumikia katika kutaniko moja dogo, mara moja kila juma Bruno alibeba chakula, maji, na machapisho katika mkoba wake na kusafiri kwa pikipiki yake kwenda kuhubiri katika maeneo ya mashambani. Watu wengi katika maeneo hayo hawakuwa wamewahi kusikia habari njema. “Niliongoza mafunzo 18 hivi ya Biblia,” anasema. “Nilipata shangwe nyingi sana nilipoona wanafunzi hao wakifanya mabadiliko maishani mwao!” Anaongezea: “Hapo ndipo nilipotambua kwamba nilikuwa nimepata kile nilichokosa maishani mwangu, yaani, uradhi mwingi unaotokana na kutanguliza mambo ya Ufalme. Nisingepata furaha hiyo kamwe kama ningefuatia miradi ya kimwili.” Lakini, Bruno alijitegemeza kifedha namna gani alipokuwa Guapiara? Anasema hivi huku akitabasamu: “Niliwafundisha watu kupiga gitaa.” Kwa njia fulani, bado alikuwa mwalimu (maestro).

“ILINIBIDI TU NIBAKI”

Mariana (5), ambaye sasa ana umri wa karibu miaka 30, alijikuta katika hali kama ya Bruno. Alikuwa mwanasheria, na ingawa ilikuwa kazi nzuri sana, bado hakuwa na uradhi wa kweli. Anasema: “Nilihisi ni kana kwamba nilikuwa ‘nikifuatilia upepo.’” (Mhu. 1:17) Ndugu na dada kadhaa walimtia moyo afikirie kufanya upainia. Baada ya kufikiria jambo hilo, Mariana pamoja na marafiki zake Bianca (6), Caroline (7), na Juliana (8), waliamua kulisaidia kutaniko moja huko Barra do Bugres, mji wa mbali ulio karibu na Bolivia, maelfu ya kilomita mbali na nyumbani kwao. Ni nini kilichotokea?

Mariana anasema: “Nia yangu ilikuwa kukaa huko kwa miezi mitatu. Lakini mwishoni mwa kipindi hicho, nilikuwa nikiongoza mafunzo 15 ya Biblia! Bila shaka, wanafunzi hao walihitaji msaada zaidi ili kufanya maendeleo katika kweli. Kwa hiyo, nilikosa ujasiri wa kuwaambia kwamba ninaondoka. Ilinibidi tu nibaki.” Na hivyo ndivyo dada hao wanne walivyofanya. Je, kazi hiyo mpya ya Mariana ilimsaidia kuishi maisha yenye kusudi zaidi? Anasema: “Ninafurahi kujua kwamba Yehova ananitumia ili kuwasaidia watu wabadili na kuboresha maisha yao. Ninahisi kuwa ni baraka kujua kwamba sasa ninatumia wakati na nguvu zangu kufanya jambo lenye thamani ya kweli.” Akieleza kwa ufupi hisia za dada wote wanne, Caroline anasema: “Ninapolala usiku, ninakuwa na uradhi mkubwa kwa sababu nimejitahidi kabisa kufuatia mambo ya Ufalme. Ninatumia maisha yangu kuwasaidia wanafunzi wangu wa Biblia. Ni jambo zuri ajabu kuwaona wakifanya maendeleo. Ninajionea ukweli wa maneno haya: ‘Onjeni mwone ya kuwa Yehova ni mwema.’”​—Zab. 34:8.

Bila shaka, Yehova anafurahi sana anapoona idadi inayozidi kuongezeka ulimwenguni pote ya ndugu na dada vijana ‘wanaojitoa kwa hiari’ kuhubiri habari njema ya Ufalme wake katika maeneo ya mashambani! (Zab. 110:3; Met. 27:11) Kwa upande mwingine, wajitoleaji hao wote hupata baraka za Yehova zinazotajirisha.—Met. 10:22.