Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Ninyi ni wenye thamani [zaidi].”​—MATHAYO 10:31

Je, Mungu Anakuona na Kukutambua?

Je, Mungu Anakuona na Kukutambua?

UUMBAJI UNATUFUNDISHA NINI?

Dakika 60 za kwanza baada ya mtoto kuzaliwa ni kipindi muhimu sana. Kwa nini? Kwa sababu uhusiano kati ya mama na mtoto aliyezaliwa ambao husitawishwa ndani ya dakika hizo 60, huboresha kwa kiwango kikubwa ukuzi na maendeleo ya mtoto huyo. *

Ni nini humsukuma mama aliyejifungua kumjali na kumshughulikia mtoto wake kwa wororo? Katika makala ya The Journal of Perinatal Education, Profesa Jeannette Crenshaw alieleza kwamba kiwango cha homoni aina ya oxytocin huongezeka na hivyo “kuchochea hisia za mama kila anapomgusa, anapomtazama, na kumnyonyesha mtoto wake mchanga.” Homoni nyingine ambayo pia hutokezwa wakati huo, “humsaidia mama kutambua na kushughulikia mahitaji ya mtoto wake” na kuimarisha uhusiano wa mama na mtoto. Kujua jambo hilo kuna umuhimu gani?

Uhusiano wa karibu kati ya mama na mtoto ulibuniwa na Muumba wetu mwenye upendo, Yehova Mungu. * Mfalme Daudi alisema kwamba Mungu ndiye ‘aliyemtoa tumboni’ na kumfanya ahisi akiwa salama mikononi mwa mama yake. Alisali hivi: “Nimewekwa chini ya utunzaji wako tangu nilipozaliwa; tangu nilipokuwa katika tumbo la mama yangu, umekuwa Mungu wangu.”—Zaburi 22:9, 10.

FIKIRIA HILI: Kwa kuwa Mungu alibuni mfumo tata hivyo ili mama aliyejifungua aweze kumtunza na kumshughulikia mtoto wake kwa wororo, basi je, si dhahiri kwamba anatukazia uangalifu sisi tukiwa “watoto” wake?—Matendo 17:29.

BIBLIA INAONYESHAJE KWAMBA MUNGU ANATUKAZIA UANGALIFU KWA UPENDO?

Yesu Kristo, ambaye anamjua Muumba wetu vizuri kuliko mtu mwingine yeyote, alisema hivi: “Shore wawili huuzwa kwa sarafu ya thamani ndogo, sivyo? Lakini hakuna hata mmoja wao atakayeanguka chini bila Baba yenu kujua. Lakini hata nywele zote za vichwa vyenu zimehesabiwa. Kwa hiyo msiogope; ninyi ni wenye thamani kuliko shore wengi.”—Mathayo 10:29-31.

Kwa kawaida, wengi wetu huwa hatuwakazii uangalifu ndege wadogo tunaowaona, sembuse kutambua ikiwa mmoja wao ameanguka chini! Lakini Baba yetu wa mbinguni anamtambua kila mmoja wao! Na ndege, hata wawe wengi kadiri gani, thamani yao machoni pake haiwezi kulinganishwa na ya mwanadamu. Somo ni wazi: ‘Usiogope’ na kudhani kwamba Mungu hakuoni. Badala yake anapendezwa sana na wewe!

Mungu anamthamini sana kila mmoja wetu, na upendo humsukuma kutuelekezea fikira

Maandiko yanatuhakikishia kwamba . . .

  • “Macho ya Yehova yako kila mahali, yakiwaangalia waovu na wema.”​—METHALI 15:3.

  • “Macho ya Yehova yanawatazama waadilifu, na masikio yake yanasikiliza kilio chao cha kuomba msaada.”​—ZABURI 34:15.

  • “Nitashangilia sana kwa sababu ya upendo wako mshikamanifu, kwa maana umeona dhiki yangu; unajua mateso makali yaliyo ndani yangu.”​—ZABURI 31:7.

“NILIHISI YEHOVA HANIPENDI”

Je, kujua kwamba Mungu anatutazama kwa makini na kutuhangaikia kwa upendo kunaweza kuboresha maisha yetu? Ndiyo. Hannah, * anayeishi Uingereza alijionea hivyo. Anasema:

“Mara nyingi sana nilihisi Yehova hanipendi na kwamba hakuwa akijibu sala zangu. Nilihisi huenda sikuwa na imani ya kutosha. Nilihisi nilikuwa nikiadhibiwa au kupuuzwa kwa sababu mimi si mtu muhimu. Nilihisi Mungu hanijali.”

Hata hivyo, sasa Hannah ana uhakika kwamba Yehova anamjali na kumpenda. Ni nini kilibadili maoni yake? Anasema: “Nilibadilika hatua kwa hatua. Nakumbuka hotuba moja ya Biblia iliyotolewa miaka mingi iliyopita kuhusu dhabihu ya fidia ya Yesu. Hotuba hiyo ilinigusa sana na kunisaidia kuhisi kwamba Yehova ananipenda. Na sala zangu zinapojibiwa, mimi hububujikwa na machozi kwa sababu ninatambua kwamba kumbe Yehova ananipenda. Pia, kujifunza Biblia na kuhudhuria mikutano ya Kikristo kumenifundisha mengi kumhusu Yehova, utu wake, na jinsi anavyohisi kutuhusu. Sasa ninajionea wazi jinsi Yehova anavyotutegemeza, anavyotupenda, na kwamba yuko tayari kumtunza kila mmoja wetu.”

Maneno ya Hannah yanatia moyo sana. Lakini unawezaje kuwa na uhakika kwamba Mungu anakuelewa na kujali hisia zako? Makala inayofuata itajibu swali hilo.

^ fu. 3 Huenda baadhi ya akina mama wanaopata ugonjwa wa kushuka moyo baada ya kujifungua wakashindwa kujenga uhusiano wa karibu na watoto wao. Hata hivyo, hawapaswi kujilaumu. Kulingana na Taasisi ya Kitaifa ya Afya ya Akili nchini Marekani (NIMH), inaelekea ugonjwa wa kushuka moyo baada ya kujifungua “unasababishwa na matatizo ya kimwili na ya kihisia . . . na hautokani na mambo ambayo mama anafanya au ambayo hafanyi.” Ili kupata habari zaidi kuhusu ugonjwa huo, soma makala “Kuelewa Mshuko wa Moyo Baada ya Kujifungua” katika gazeti la Amkeni! la Juni 8, 2003.

^ fu. 5 Yehova ni jina la Mungu kama linavyoonyeshwa katika Biblia.—Zaburi 83:18.

^ fu. 15 Baadhi ya majina katika makala za toleo hili yamebadilishwa.