Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU | JE, UTAITHAMINI ZAWADI BORA ZAIDI YA MUNGU?

Zawadi Bora Zaidi ya Mungu—Kwa Nini Ni Yenye Thamani Sana?

Zawadi Bora Zaidi ya Mungu—Kwa Nini Ni Yenye Thamani Sana?

Ni nini hufanya zawadi iwe yenye thamani kwako? Huenda mambo manne yanahusika: (1) aliyetoa zawadi, (2) sababu ya kutoa, (3) jinsi alivyojidhabihu, na (4) ikiwa zawadi inatimiza uhitaji muhimu kwako. Kufikiria mambo hayo kunaweza kutusaidia kuthamini zaidi fidia—zawadi bora zaidi ya Mungu.

NI NANI ALIYETOA?

Tunathamini zawadi fulani kwa sababu tulipewa na mtu mwenye mamlaka au tunayemheshimu sana. Pia, tunathamini zawadi zingine kwa sababu tulipewa na washiriki wa familia au rafiki zetu wapendwa, ingawa ni za bei ya chini. Ilikuwa hivyo kuhusiana na zawadi ya Russell aliyetajwa katika makala iliyotangulia. Hilo linahusianaje na zawadi ya fidia?

Kwanza, Biblia inasema kwamba “Mungu alimtuma Mwana wake mzaliwa-pekee kuja ulimwenguni ili tupate uzima kupitia yeye.” (1 Yohana 4:9) Hiyo ni sababu inayofanya zawadi hiyo iwe yenye thamani kubwa sana. Hakuna aliye na mamlaka kuu kuliko Mungu. Mtunga zaburi Mwebrania alisema hivi kumhusu Mungu: “Wewe, ambaye jina lako ni Yehova, Wewe peke yako ndiye Uliye Juu Zaidi, juu ya dunia yote.” (Zaburi 83:18) Fidia ni zawadi kutoka kwa mwenye mamlaka kuu kuliko zote.

Pili, Mungu ni “Baba yetu.” (Isaya 63:16) Jinsi gani? Ametupatia uhai. Kwa kuongezea, yeye hutuandalia mahitaji yetu kwa ushikamanifu kama vile baba mwenye bidii anavyowajali watoto wake. Akizungumza kuhusu watu wake walioitwa Efraimu, Mungu alisema hivi: “Efraimu ni mwanangu mpendwa . . . Moyo wangu wamwelekea kwa wema; hakika nitamhurumia.” (Yeremia 31:20 Habari Njema) Mungu anahisi vivyo hivyo kuhusu watumishi wake leo. Zaidi ya kuwa Muumba mweza yote, Yeye pia ni Rafiki na Baba mshikamanifu. Bila shaka, zawadi zote kutoka kwake ni zenye thamani!

KWA NINI ILITOLEWA?

Baadhi ya zawadi zinathaminiwa kwa kuwa zilitolewa kwa sababu ya upendo wa kweli wala si kwa kulazimishwa. Mtu anayetoa kwa kupenda hatazamii kulipwa kwa sababu ya fadhili zake.

Mungu alimtoa Mwana wake kwa ajili yetu kwa sababu anatupenda. Biblia inasema hivi: “Kwa hili upendo wa Mungu ulifunuliwa kwa habari yetu, kwa sababu Mungu alimtuma Mwana wake mzaliwa-pekee kuja ulimwenguni.” Kwa kusudi gani? “Ili tupate uzima kupitia yeye.” (1 Yohana 4:9) Je, Mungu alilazimishwa kufanya hivyo? La hasha! “Fidia ambayo Kristo Yesu alilipa” ni wonyesho wa Mungu wa “fadhili zake zisizostahiliwa.”—Waroma 3:24.

Kwa nini zawadi ya Mungu ni tendo la “fadhili zisizostahiliwa”? Biblia inajibu hivi: “Mungu hupendekeza upendo wake mwenyewe kwetu kwa kuwa, tulipokuwa tungali watenda-dhambi, Kristo alikufa kwa ajili yetu.” (Waroma 5:8) Upendo wa kweli ulimchochea Mungu kuwakomboa wanadamu dhaifu na wenye dhambi. Hatukustahili upendo huo, na hatuwezi kamwe kumlipa. Zawadi hiyo ndiyo wonyesho mkubwa zaidi wa upendo mkuu katika historia yote ya mwanadamu.

ALIJIDHABIHU NINI ILI KUITOA?

Zawadi zingine zina thamani kwa sababu yule aliyetoa alijidhabihu sana. Ni wazi kwamba tutathamini sana zawadi ambayo ingawa ni yenye thamani sana kwa mtoaji, anajidhabihu ili kutupatia.

Mungu alimtoa “Mwana wake mzaliwa-pekee.” (Yohana 3:16) Alimtoa Mwana ambaye alimpenda zaidi. Kwa kipindi kirefu Mungu alipokuwa akiumba ulimwengu, Yesu alifanya kazi kando yake, naye akawa “yule ambaye yeye alimpenda sana kwa njia ya pekee.” (Methali 8:30) Yesu ndiye ‘Mwana mpendwa’ wa Mungu na “mfano wa Mungu asiyeonekana.” (Wakolosai 1:13-15) Hakuna viumbe ambao wamewahi kuwa na uhusiano wa karibu kama Yehova na Yesu.

Hata hivyo, Mungu “hakujizuia [kumtoa] hata Mwana wake mwenyewe.” (Waroma 8:32) Yehova alimtoa yule anayempenda zaidi kwa ajili yetu. Hiyo ni zawadi iliyomgharimu zaidi kuliko zote.

KUTIMIZA UHITAJI MUHIMU

Zawadi zingine ni zenye thamani kwa sababu zinatimiza uhitaji muhimu au wa haraka. Kwa mfano, bila shaka ungemshukuru sana mtu ambaye angejitolea kukulipia gharama za matibabu ambazo umeshindwa kulipa na hivyo kuokoa uhai wako! Zawadi hiyo ingekuwa na thamani kubwa sana kwako, sivyo?

“Kama vile katika Adamu wote wanakufa, vivyo hivyo pia katika Kristo wote watafanywa kuwa hai.” (1 Wakorintho 15:22) Tukiwa wazao wa Adamu, sote ‘tunakufa,’ hatuwezi kuepuka maumivu yanayosababishwa na magonjwa na kifo au kujipatanisha na Mungu na kuwa bila hatia mbele zake. Pia, tukiwa wanadamu wasiokamilika, hatuwezi kujikomboa au “kumkomboa” mtu yeyote. Biblia inaeleza hivi waziwazi: “Hakuna hata mmoja wao anayeweza kumkomboa hata ndugu, wala kumpa Mungu fidia kwa ajili yake.” (Zaburi 49:7) Kwa kweli hatuwezi kulipia fidia. Bila msaada, hatungeweza kujikomboa.

Kwa kuwa anatupenda sana, Yehova alitulipia kwa hiari “matibabu” ili kuokoa uhai wetu, hivi kwamba kwa njia ya Yesu ‘wote wafanywe kuwa hai.’ Fidia inatimizaje jambo hilo? “Damu ya Yesu Mwana wake hutusafisha kutoka katika dhambi yote.” Naam, imani katika damu ya Yesu iliyomwagwa hufungua njia ya kupata msamaha wa dhambi na uzima wa milele. (1 Yohana 1:7; 5:13) Fidia itawafaidi jinsi gani wapendwa wetu waliokufa? “Kwa kuwa kifo ni kupitia mwanadamu, ufufuo wa wafu pia ni kupitia mwanadamu [Yesu].”—1 Wakorintho 15:21. *

Dhabihu ya Yesu ndiyo zawadi tuliyopewa na mwenye mamlaka kubwa kuliko zote akichochewa upendo mkubwa. Hakuna yeyote ambaye amewahi kujitoa kama Yehova Mungu. Na hakuna zawadi inayotimiza uhitaji mkubwa kuliko dhabihu inayotukomboa kutoka kwenye dhambi na kifo. Naam, hakuna zawadi inayoweza kulingana kikamili na thamani ya fidia.

 

^ fu. 19 Ili kupata habari zaidi kuhusu ahadi ya Mungu ya kuwafufua waliokufa, soma sura ya 7 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova, pia kinapatikana kwenye tovuti ya www.pr418.com/sw.