Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nilipata Tumaini Nilipokuwa Nimekata Tamaa

Nilipata Tumaini Nilipokuwa Nimekata Tamaa

Ghafla nilikuta nimelala kifudifudi ndani ya maji. Nilijaribu kuinua kichwa ili nipumue, lakini misuli ya shingo ilikataa. Kwa woga, nilijaribu kujipindua, lakini mikono na miguu ilikataa kusogea. Maji yalianza kupenya ndani ya mapafu yangu. Maisha yangu yalibadilika kabisa siku hiyo ya majira ya kiangazi ya mwaka wa 1991.

NILIZALIWA jijini Szerencs na nikalelewa katika kijiji cha Tiszaladány kilichoko kaskazini-mashariki mwa nchi ya Hungaria. Mwezi wa Juni mwaka wa 1991, nikiwa na rafiki zangu, tulitembelea sehemu fulani ya Mto Tisza ambayo hatukuijua vizuri. Nikidhani maji yalikuwa na kina kirefu, nilipiga mbizi majini. Kumbe nilikuwa nimekosea! Niliumia uti wa mgongo na mifupa mitatu shingoni ikavunjika. Rafiki yangu mmoja alipoona sisogei aliniinua polepole na akanitoa kabla sijafa maji.

Nilijua kwamba mambo hayakuwa sawa. Mtu fulani alipiga simu kwa ajili ya huduma za dharura na helikopta ilikuja na kunipeleka hospitalini ambapo madaktari walijitahidi kunitibu uti wa mgongo ili nisipate madhara zaidi. Baadaye nilihamishiwa jijini Budapest, ili nipate msaada zaidi. Nililala chali kitandani kwa miezi mitatu. Ningeweza tu kusogeza kichwa changu, sehemu nyingine ya mwili wangu ilikuwa imepooza, kutoka mabegani hadi miguuni. Ingawa nilikuwa na umri wa miaka 20, nisingeweza kujifanyia chochote. Nilivunjika moyo sana hivi kwamba nilitamani kufa.

Niliporuhusiwa kwenda nyumbani, wazazi wangu walipata mafunzo ya jinsi ya kunitunza. Hata hivyo, kazi hiyo iliwalemea sana kimwili na kihisia, na baada ya mwaka mmoja hivi, nilipatwa na ugonjwa wa kushuka moyo. Wakati huo nilipata ushauri wa kitaalamu, ulionisaidia kuwa na mtazamo mzuri kuhusu ulemavu wangu.

Nilianza pia kutafakari maisha yangu kwa kina. Je, yalikuwa na kusudi lolote? Kwa nini nilipatwa na janga hili? Nilitafuta majibu kwenye magazeti na vitabu. Nilijaribu pia kusoma Biblia, lakini sikuielewa. Hivyo nikaacha kuisoma. Isitoshe, nilizungumza na kasisi, lakini sikuridhika na maelezo yake.

Kisha, katika majira ya kuchipua ya mwaka wa 1994, Mashahidi wawili wa Yehova walimtembelea baba yangu na akawaomba wazungumze nami. Niliwasikiliza wakifafanua kusudi la Mungu la kufanya dunia iwe paradiso na kuondoa magonjwa na kuteseka. Hizo zilikuwa habari nzuri, lakini bado nilikuwa na shaka. Hata hivyo, nilikubali vitabu viwili vya kujifunzia Biblia. Nilipomaliza kuvisoma, Mashahidi walinihimiza nijifunze Biblia pamoja nao, nami nikakubali. Pia walinitia moyo nisali.

Kadiri nilivyoendelea kujifunza Biblia pamoja nao, ndivyo  nilivyopata majibu ya maswali mengi niliyokuwa nayo. Pia nikaamini kwamba kweli Mungu ananijali.

Baada ya kujifunza Biblia kwa miaka miwili, hatimaye, Septemba 13, 1997, nilibatizwa nyumbani kwenye beseni kubwa la kuogea. Ilikuwa mojawapo ya siku zenye furaha sana maishani mwangu!

Nikaamini kwamba kweli Mungu ananijali

Mwaka wa 2007, nilihamia kwenye makao ya walemavu, jijini Budapest. Hilo limenipa nafasi nyingi za kuzungumza na wengine mambo mazuri ambayo nimejifunza. Kukiwa na hali nzuri ya hewa, ninaweza hata kutoka nje na kuzungumza na watu kwani nina kiti cha magurudumu chenye injini ninachokiendesha kwa kutumia kidevu changu.

Vilevile, familia moja katika kutaniko langu, ilininunulia kompyuta ndogo inayofanya kazi kwa kutambua ninavyosogeza kichwa changu. Kompyuta hii inaniwezesha kuwapigia simu watu kupitia Intaneti na kuwaandikia barua wale ambao hawakuwepo nyumbani walipotembelewa na Mashahidi wa kutaniko langu. Kuwasaidia wengine katika njia hiyo kumeboresha sana uwezo wangu wa kuwasiliana na kumenisaidia nisijifikirie kupita kiasi.

Kuwahubiria watu kupitia Intaneti kwa kutumia kompyuta inayotambua ninavyosogeza kichwa

Pia mimi huhudhuria mikutano ya Kikristo. Ninapofika kwenye Jumba la Ufalme, waamini wenzangu hunipandisha ghorofa moja hadi kwenye mikutano. Mikutanoni, wahudhuriaji wanapoombwa kutoa maelezo, ndugu aliyeketi karibu nami huinua mkono wake kwa ajili yangu. Kisha ninatoa maelezo akiwa amenifungulia Biblia yangu au kitabu cha kujifunzia.

Mimi hupatwa na maumivu siku zote na ninahitaji kusaidiwa kufanya karibu kila kitu. Hivyo bado ninavunjika moyo wakati mwingine. Hata hivyo, ninafarijika kwa kuwa na urafiki na Yehova Mungu na kujua kwamba ananisikiliza ninapomweleza mahangaiko yangu. Pia, ninapata nguvu kwa kusoma Biblia kila siku na nimeimarishwa sana na ndugu na dada zangu wa kiroho. Urafiki wao, faraja yao, na sala zao kwa niaba yangu zimenisaidia kubaki katika hali nzuri ya kiakili na kihisia.

Yehova alinifariji nilipokuwa nimekata tamaa. Alinipa pia tumaini la kuwa na afya kamilifu katika dunia mpya. Kwa hiyo, ninasubiri kwa hamu wakati ambapo nitaweza ‘kutembea na kuruka-ruka na kumsifu’ kwa sababu ya fadhili na upendo wake mwingi.—Matendo 3:6-9.