Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | KULEA WATOTO

Mtoto Wako Anaposema Uwongo

Mtoto Wako Anaposema Uwongo

KIKWAZO

Mtoto wako wa miaka mitano anacheza chumbani. Ghafla unasikia mlio. Unaingia na kumkuta amesimama kando ya chombo cha udongo kilichovunjika. Uso wake unaonyesha hatia ya kosa alilofanya.

Ukiwa umekasirika, unamuuliza mtoto wako, “Yaani, umevunja hicho chombo?”

Mtoto wako anajitetea haraka, “Hapana, Mama, siyo mimi!”

Hii siyo mara ya kwanza kwa mtoto wako wa miaka mitano kusema uwongo. Je, hilo linapaswa kukutia wasiwasi?

UNACHOPASWA KUJUA

Kusema uwongo ni kosa. Biblia inasema kwamba Yehova Mungu anachukia “ulimi wa uwongo.” (Methali 6:16, 17) Sheria waliyopewa Waisraeli ilikataza mtu kumdanganya mwenzake.—Mambo ya Walawi 19:11, 12.

Hata hivyo, uwongo unatofautiana. Baadhi ya uwongo ni hatari sana kwa sababu unakusudiwa kumdhuru mtu mwingine. Ilhali nyakati nyingine watu husema uwongo kwa sababu wameshinikizwa na hali au mtu, au ili tu waepuke aibu na adhabu. (Mwanzo 18:12-15) Ingawa kwa kweli aina zote za uwongo ni mbaya, baadhi ya uwongo ni hatari zaidi kuliko mwingine. Ikiwa mtoto wako anasema uwongo, fikiria umri wake na sababu inayomfanya afiche ukweli.

Unapaswa kumsaidia mtoto wako wakati angali mdogo. Dakt.  David Walsh anasema hivi: “Kusema ukweli, hata inapokuwa vigumu, ni somo muhimu sana kwa watoto. Kutumainiana ni muhimu ili kuimarisha uhusiano, ilhali kusema uwongo hufanya watu wakose kutumainiana.” *

Hata hivyo, usishtuke sana. Kwa sababu mtoto wako amesema uwongo haimaanishi kwamba punde si punde atakuwa mwovu. Kumbuka, Biblia inasema hivi: “Ujinga umefungwa pamoja na moyo wa mvulana.” (Methali 22:15) Baadhi ya watoto huonyesha ujinga wao kwa kusema uwongo, wakidhani kwamba kufanya hivyo ni njia rahisi ya kuepuka kuadhibiwa. Hata hivyo, la muhimu ni vile utakavyotenda.

 UNACHOWEZA KUFANYA

Jitahidi kutambua sababu ya mtoto wako kusema uwongo. Je, huenda anaogopa kuadhibiwa? Je, anaogopa kukukasirisha? Ikiwa mtoto wako anawaambia rafiki zake uwongo ili kuwafurahisha, je, ni kwa sababu bado hajatambua tofauti kati ya ukweli na maigizo? Ukijua sababu inayomfanya mtoto wako aseme uwongo, utaweza kumsaidia vizuri zaidi.—Kanuni ya Biblia: 1 Wakorintho 13:11.

Nyakati nyingine inafaa kusema moja kwa moja badala ya kumuuliza maswali. Katika kisa kilichotajwa mwanzoni mwa makala hii, mama alijua kilichotokea lakini alimuuliza kwa ukali mtoto wake: “Yaani, umevunja hicho chombo?” Huenda mtoto alisema uwongo kwa sababu aliogopa kuadhibiwa. Badala ya kumuuliza swali la kumfanya mtoto ajitetee ingefaa mama amwambie moja kwa moja: “Inaonekana chombo hicho kimevunjika!” Kwa kusema moja kwa moja badala ya kuuliza swali, hampi nafasi mtoto wake kusema uwongo—na pia anamsaidia azoee kusema ukweli.—Kanuni ya Biblia: Wakolosai 3:9.

Mpongeze anaposema ukweli. Kiasili watoto wanapenda kuwafurahisha wazazi wao, kwa hiyo tumia fursa hiyo kumsaidia aendelee kusema kweli. Acha mtoto wako ajue kwamba unyoofu ni sifa muhimu katika familia yenu na kwamba unatarajia yeye pia awe mnyoofu.—Kanuni ya Biblia: Waebrania 13:18.

Msaidie mtoto wako aelewe waziwazi kwamba kusema uwongo hufanya watu wakose kutumainiana na kwamba huchukua muda mrefu kurudisha hali hiyo ya kutumainiana. Endelea kumtia moyo asitawishe tabia njema kwa kumpongeza kila anaposema ukweli. Kwa mfano, unaweza kumwambia hivi: “Mimi hufurahi sana unaposema ukweli.”

Mwekee mfano. Bila shaka, usitarajie mtoto wako aseme ukweli ikiwa wewe humwambia aseme maneno kama “Amesema hayupo” wakati hutaki kupokea simu, au anakusikia ukisema, “Leo naumwa” huku akijua kwamba nia yako ni kupumzika.—Kanuni ya Biblia: Yakobo 3:17.

Tumia Biblia. Kanuni za Biblia na masimulizi ya watu yanayopatikana humo yanatutia moyo kuwa wanyoofu. Kitabu Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova, kinaweza kukusaidia umfundishe mtoto wako kanuni za Biblia. Sura ya 22 ina kichwa “Kwa Nini Hatupaswi Kusema Uwongo?” (Ona habari iliyonukuliwa kutoka kwenye kitabu hicho kwenye sanduku lenye kichwa “ Kitabu Kitakachomsaidia Mtoto Wako.”) Kitabu

^ fu. 11 Kutoka kwenye kitabu No: Why Kids—of All Ages—Need to Hear It and Ways Parents Can Say It.