Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 HABARI KUU

Mwisho wa Jeuri Inayotokea Nyumbani

Mwisho wa Jeuri Inayotokea Nyumbani

Kisa cha 1: Wazazi wa Isabel * wamekuja kuwatembelea. Wanafurahia jioni nzuri pamoja na binti yao na mume wake, wakiwa na mazungumzo yenye kupendeza. Ni mzazi gani ambaye hangejivunia kuwa na mwana-mkwe kama huyo? Anamtendea binti yao kwa fadhili sana.

Kisa cha 2: Frank amewaka hasira. Kama kawaida yake, atatuliza hasira yake kwa kumpiga mke wake usoni, kumpiga mateke, kuvuta nywele zake, au kugongesha kichwa chake ukutani.

HUENDA ukashangaa kujua kwamba visa vyote viwili vinahusu wenzi walewale wa ndoa.

Kama watu wengi wanaotenda kwa jeuri nyumbani, Frank anajua jinsi ya kujifanya aonekana kuwa mtu mzuri mbele za watu, au akiwa pamoja na wazazi wa mke wake. Lakini yeye na mke wake wanapokuwa peke yao, Frank ni mkatili sana.

Kama Frank, wanaume wengi walilelewa katika familia ambamo jeuri ilikuwa jambo la kawaida, na sasa wakiwa watu wazima wanadhani kwamba tabia yao inakubalika au hata ni jambo la kawaida.  Lakini jeuri nyumbani si jambo la kawaida hata kidogo. Hiyo ndiyo sababu watu wengi hushtuka sana wanapojua kwamba mwanamume fulani amempiga mke wake.

Hata hivyo, bado jeuri nyumbani ni jambo lililoenea sana. Kwa mfano, nchini Marekani, uchunguzi mmoja ulionyesha kwamba katika siku moja, vituo vya kuwasaidia watu wanaotendewa kwa jeuri nyumbani vilijibu simu zaidi ya 16 kwa kila dakika. Jeuri nyumbani ni tatizo la ulimwenguni pote linalopatikana katika kila tamaduni, tabaka, na jamii. Kwa kuwa visa vingi vya jeuri nyumbani haviripotiwi, hali hiyo ni mbaya kuliko takwimu zinavyoonyesha. *

Ripoti za visa vya jeuri ya nyumbani zinafanya watu wajiulize swali hili: Mwanamume anawezaje kumtendea mtu yeyote—hasa mke wake—kwa ukatili hivyo? Je, wanaume ambao huwapiga wake zao wanaweza kusaidiwa wabadili tabia yao?

Mashahidi wa Yehova ambao ndio wachapishaji wa gazeti hili, wanaamini kwamba shauri la Biblia linaweza kuwasaidia wenzi wa ndoa wenye jeuri wabadili tabia yao. Je, ni rahisi kwa mtu kubadilika? La. Lakini, je, mtu anaweza kubadilika? Ndiyo! Mafundisho ya Biblia yamewasaidia wengi kubadili utu wao wenye jeuri na kuwa watu wenye fadhili na heshima. (Wakolosai 3:8-10) Ona mfano wa Troy na Valerie.

Uhusiano wenu ulikuwaje mwanzoni?

Valerie: Siku tulipotangaza uchumba wetu kirasmi, Troy alinizaba kofi lililoniacha na alama kwa juma moja. Aliniomba msamaha sana na kuahidi kwamba hatawahi kurudia tena jambo hilo. Katika  miaka yote ambayo tumeoana nimesikia maneno hayo mara nyingi.

Troy: Jambo lolote lingenifanya nilipuke kwa hasira—hata jambo dogo kama mke wangu kuchelewa kupika. Pindi moja nilimpiga Valerie kwa kitako cha bastola. Pindi nyingine, nilimpiga vibaya sana hivi kwamba nilidhani nimemwua. Kisha nilijaribu kumwogopesha kwa kumshikia mwana wetu kisu kooni na kutisha kumwua.

Valerie: Niliishi kwa woga sikuzote. Nyakati nyingine ilibidi niondoke nyumbani hadi Troy alipotulia. Ingawa alinipiga vibaya, jambo lililoniumiza zaidi ni matusi yake.

Troy, ulikuwa mwenye jeuri tangu utotoni?

Troy: Ndiyo, tangu utotoni na kuendelea. Nililelewa katika mazingira yenye jeuri. Baba yangu alikuwa akimpiga Mama mbele yetu. Baada ya baba kutuacha, Mama alianza kuishi na mwanamume mwingine, naye pia alikuwa akimpiga. Mwanamume huyo alimbaka dada yangu na kunilawiti. Alifungwa gerezani kwa sababu ya kosa hilo. Bila shaka, natambua kwamba hicho si kisingizio kwa tabia yangu.

Valerie, kwa nini uliendelea kuishi na mume wako?

Valerie: Nilikuwa na hofu. Nilijiambia, ‘Vipi akinifuata na kuniua au kuwaua wazazi wangu? Vipi nikimripoti kisha hali iwe mbaya hata zaidi?’

Mambo yalianza kubadilika wakati gani?

Troy: Mke wangu alianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Mwanzoni nilimwonea wivu kwa sababu alikuwa na marafiki wapya, na nilidhani kwamba ninahitaji kumwokoa kutoka kwa “madhehebu” hiyo ya kiajabu. Kwa hiyo, nikawa mwenye jeuri hata zaidi, si kumwelekea Valerie tu, bali pia kuwaelekea Mashahidi hao. Lakini siku moja, mwana wetu Daniel, mwenye umri wa miaka minne, ambaye alikuwa na ugonjwa wa kifafa, alilazwa hospitalini kwa karibu majuma matatu. Katika kipindi hicho, Mashahidi walitusaidia sana, hata walisaidia kumtunza binti yetu Desiree, mwenye umri wa miaka sita. Shahidi mmoja aliyekuwa amefanya kazi usiku kucha alijitolea kumtunza Daniel siku iliyofuata ili Valerie aweze kulala. Matendo ya fadhili ya watu hao—watu ambao nilikuwa nimewatendea kwa dharau—yalinigusa sana. Nilitambua kwamba Mashahidi  walitenda kama Wakristo wa kweli, kwa hiyo niliwaomba wanifundishe Biblia. Katika masomo yangu ya Biblia, nilijifunza mambo ambayo mwanamume anapaswa kumtendea mke wake na mambo ambayo hapaswi kumtendea. Niliacha kabisa tabia yangu ya jeuri na matusi. Mwishowe nikawa Shahidi wa Yehova.

Ni kanuni gani za Biblia zilizokusaidia kubadilika?

Troy: Ni nyingi. Kwenye 1 Petro 3:7, Biblia inasema kwamba ninapaswa ‘kumheshimu’ mke wangu. Wagalatia 5:23 inatutia moyo tuwe na sifa ya “upole” na “kujizuia.” Waefeso 4:31 inakataza “matukano.” Waebrania 4:13 inasema kwamba “vitu vyote . . . vimefunuliwa wazi machoni” pa Mungu. Kwa hiyo, Mungu huona matendo yangu hata ingawa majirani hawayaoni. Pia nilijifunza kwamba ninapaswa kubadili marafiki wangu, kwa kuwa “mashirika mabaya huharibu tabia nzuri.” (1 Wakorintho 15:33) Marafiki wangu wa zamani walinitia moyo niwe mjeuri. Walisema kwamba ni sawa kumpiga mwanamke ili “umdhibiti.”

Sasa mna maoni gani kuhusu ndoa yenu?

Valerie: Miaka 25 imepita tangu Troy awe Shahidi wa Yehova. Wakati huo wote amenionyesha upendo, fadhili, na kunijali.

Troy: Siwezi kubadili maovu yote niliyoitendea familia yangu, na mke wangu hakustahili kamwe kutendewa hivyo. Lakini ninatazamia kwa hamu kutimizwa kwa Isaya 65:17, wakati ambapo sitakuwa tena na kumbukumbu ya maovu niliyomtendea.

Mna mashauri gani kwa familia zenye jeuri?

Troy: Ikiwa unaitendea familia yako kwa jeuri iwe ni kuwapiga au kuwatukana, kubali kwamba unahitaji msaada na uutafute. Unaweza kupata msaada katika njia mbalimbali. Mimi nilisaidiwa kuacha tabia ya jeuri iliyokita mizizi kwa kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova na kushirikiana nao.

Valerie: Usilinganishe hali yako na ya mtu mwingine au kufuata mashauri ya watu wanaofikiri eti wanajua kinachokufaa. Ingawa si kila mtu atapata matokeo kama yangu, ninafurahi kwamba sikumwacha mume wangu kwa kuwa sasa tuna uhusiano mzuri sana.

JINSI YA KUACHA KUTENDA KWA JEURI NYUMBANI

Kujifunza Biblia kumewasaidia wanaume wengi wafanye mabadiliko yanayohitajika

Biblia inasema: “Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu nalo ni lenye faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo.” (2 Timotheo 3:16) Kama Troy ambaye kisa chake kimesimuliwa hapo juu, wenzi wengi wa ndoa ambao walikuwa wajeuri wamefuata shauri la Biblia na wameweza kubadili mawazo na mwenendo wao.

Je, ungependa kujifunza jinsi ambavyo Biblia inaweza kusaidia ndoa yako? Kwa habari zaidi wasiliana na Mashahidi wa Yehova mahali unapoishi, au tembelea tovuti ya www.pr418.com/sw.

^ fu. 3 Baadhi ya majina katika makala hii yamebadilishwa.

^ fu. 8 Ni kweli kwamba wanaume wengi hupigwa na wanawake. Lakini katika visa vingi vinavyoripotiwa, jeuri inayotendwa nyumbani husababishwa na wanaume.