Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Biblia Kitabu cha Unabii Sahihi—Sehemu ya 5

Habari Njema kwa Watu Wote

Biblia Kitabu cha Unabii Sahihi—Sehemu ya 5

Katika mfululizo huu wa makala nane, gazeti la “Amkeni!” litazungumzia jambo la pekee kuhusu Biblia—unabii wake, au utabiri. Makala hizi zitakusaidia kujibu maswali haya: Je, unabii wa Biblia ulibuniwa na wanadamu werevu? Au kuna mambo yanayoonyesha kwamba uliongozwa na roho ya Mungu? Tunakukaribisha uchunguze uthibitisho.

UJUMBE wa Mungu kwa wanadamu unapatikana katika Biblia, na ujumbe huo unahusu habari njema. Kwa sababu hiyo, Yesu Kristo alitumia maisha yake kutangaza “habari njema ya ufalme.” (Luka 4:43) Biblia inaonyesha kwamba Ufalme huo ni serikali ya Mungu na kwamba itaondoa utawala wa wanadamu wenye kukandamiza, ilete amani, na kuondoa mambo yote yanayowafanya wanadamu wateseke. (Danieli 2:44; Mathayo 6:9, 10) Hizo ni habari njema kwelikweli!

Bila shaka, habari njema kama hizo zinapaswa kutangazwa kwa mapana na marefu. Hata hivyo, Yesu alipouawa, aliacha wafuasi wachache tu. Je, ujumbe wake ungepotea baada ya yeye kufa? Biblia ilitabiri jambo lililo kinyume na hilo. Ilitabiri mambo yafuatayo: (1) Habari njema ingeenea katika mataifa yote. (2) Wanaoieneza wangevumilia upinzani mkali. (3) Wakristo wa uwongo, au bandia, wangetokea na kuwapotosha watu wengi. Acheni tufikirie unabii huo mbalimbali.

Habari Njema Itatangazwa Katika Mataifa Yote

Unabii:

“Katika mataifa yote lazima habari njema ihubiriwe kwanza.” (Marko 13:10) “Mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu na pia katika Yudea yote na Samaria na mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.”​—Matendo 1:8.

Utimizo: Punde baada ya kifo cha Yesu katika mwaka wa 33 W.K., wanafunzi wake walijaza Yerusalemu ujumbe wa Ufalme. Walienea kotekote katika Yudea na Samaria iliyokuwa karibu, na katika muda wa miaka 15, wamishonari Wakristo walikuwa wametumwa katika sehemu nyingine za Milki ya Roma. Kufikia mwaka wa 61 W.K., ingeweza kusemwa kwamba habari njema ilikuwa imehubiriwa katika sehemu nyingi za “mbali” za dunia.

Historia inafunua nini?

  • Maandishi ya kihistoria ya karne ya pili yanathibitisha kwamba Ukristo wa awali ulienea upesi sana. Mwanahistoria Mroma Suetonius anadai kwamba Wakristo walikuwepo huko Roma katika mwaka wa 49 W.K. Barua iliyoandikwa kwa Maliki Trajani katika mwaka wa 112 W.K. hivi na Plini Mdogo, gavana wa Bithinia (ambayo siku hizi iko nchini Uturuki), inasema kwamba Ukristo ulikuwa “ambukizo” lililokuwa “limeenea si katika miji tu, bali pia katika vijiji na mashamba.” Akichunguza tena uthibitisho, mwanahistoria mmoja alifikia kauli hii: “Katika miaka isiyozidi mia moja baada ya enzi ya mitume majengo ya ibada ya Wakristo yalionekana katika majiji makubwa ya Milki [ya Roma].”

  • Katika kitabu chake The Early Church, Profesa Henry Chadwick anasema: “Kupanuka kwa kanisa kulionekana kuwa mfuatano wa matukio mengi yasiyotarajiwa. Hakuna mtu aliyetarajia kwamba lingepanuka na kufaulu kama ilivyotukia.”

Upinzani Dhidi ya Habari Njema

Unabii:

“Watu watawapeleka mahakamani, nanyi mtapigwa katika masinagogi na kusimamishwa mbele ya magavana na wafalme kwa ajili yangu, kuwa ushahidi kwao.”​—Marko 13:9.

Utimizo: Wayahudi na Waroma waliwatesa Wakristo. Waliwakamata, wakawafunga, wakawapiga, na kuwaua.

Historia inafunua nini?

  • Flavio Yosefu, mwanahistoria Myahudi akiandika katika karne ya kwanza, anaeleza kuhusu kuuawa kwa Yakobo ndugu ya Yesu mikononi mwa viongozi wa kidini Wayahudi. Biblia inaonyesha kwamba Gamalieli, aliyekuwa mshiriki mwenye kuheshimika wa mahakama kuu ya Wayahudi, aliwasihi wenzake wawe waangalifu wakati ambapo wanafunzi wa Yesu waliletwa kwao ili wahukumiwe. (Matendo 5:34-39) Vitabu vya wasomi vinathibitisha kwamba Gamalieli alikuwa mtu halisi na vinasema kwamba alikuwa na akili iliyofunguka.

  • Wanahistoria wanatuambia kwamba kuanzia na Maliki Nero katika mwaka wa 64 W.K., maliki Waroma waliwatesa Wakristo. Barua kati ya Maliki Trajani na Plini Mdogo zinazungumzia adhabu ambayo Wakristo waliokataa kukana imani yao wangepewa.

  • “Badala ya kulifanya kanisa lianze kuabudu kisiri, mateso yalileta matokeo yaliyo kinyume,” anasema Profesa Chadwick, aliyenukuliwa awali. Wakristo walipokimbia ili kuepuka mateso, walipeleka ujumbe wao katika maeneo mapya. (Matendo 8:1) Walivumilia licha ya kwamba mara nyingi walitengwa na watu wa familia na marafiki. Hilo ni jambo lenye kushangaza, kwa kuwa wafuasi wa Yesu walikuwa watu “wasio na elimu na wa kawaida tu,” na hawakuwa na uvutano wowote wa kisiasa. (Matendo 4:13) Wanahistoria wanakubali kwamba “Injili ilienea kwa urahisi zaidi, . . . miongoni mwa wenye maduka na wafanyabiashara.”

Wanapochunguza historia, wasomi hustaajabu jinsi kikundi kidogo hivyo kingeweza kueneza Ukristo upesi kadiri hiyo kukiwa na upinzani mkubwa hivyo. Hata hivyo, Yesu alitabiri mambo hayo yasiyotarajiwa hata kabla hayajatukia. Maandiko pia yalitabiri kwamba utendaji huo wa kuhubiri ungekatizwa.

Wakristo Bandia Watokea

Unabii:

“Mbwa-mwitu wenye kukandamiza wataingia katikati yenu nao hawatalitendea kundi kwa wororo, na kutoka katikati yenu ninyi wenyewe watu watasimama na kusema mambo yaliyopotoka ili kuwavuta wanafunzi wawafuate wao wenyewe.” (Matendo 20:29, 30) “Pia [kutakuwa] na walimu wa uwongo katikati yenu. Hawa wataingiza ndani kimya-kimya madhehebu yenye kuharibu . . . , na kwa sababu ya hao ile njia ya kweli itatukanwa.”​—2 Petro 2:1, 2.

Utimizo: Kutaniko la Kikristo lilipotoshwa na watu wakali, wadanganyifu, na wenye kujitakia makuu.

Historia inafunua nini?

  • Hasa baada ya kifo cha wafuasi wa kwanza wa Yesu, Ukristo wa kweli uliathiriwa na watu wenye cheo ambao walitoka ndani ya kutaniko na waliochanganya mafundisho ya Kikristo na falsafa za Kigiriki. Punde si punde, makasisi walisitawi na wakaanza kujitwalia mamlaka na utajiri kama ule wa watawala wa kisiasa. Kulingana na wanahistoria, kufikia wakati ambapo “Ukristo” ulikubaliwa kuwa dini ya Serikali ya Roma, haukufanana hata kidogo na kutaniko la karne ya kwanza.

  • Kwa karne nyingi, aina hiyo ya Ukristo uliopotoshwa ilitenda kwa jeuri na kwa pupa. Badala ya kuthibitisha kwamba wao ni wafuasi wa Yesu, makasisi waliwatesa wale walioiga njia ya Yesu ya kuhubiri na wale waliojaribu kuchapisha Biblia katika lugha iliyotumiwa na watu wa kawaida.

Katika kipindi hicho ambacho Ukristo bandia ulikuwa na uvutano mkubwa, ni kana kwamba hakuna mtu aliyekuwa akihubiri habari njema. Hata hivyo, Yesu alionyesha kwamba habari njema ingetokea tena katika siku za mwisho. Alilinganisha kipindi hicho na mavuno wakati ambapo Wakristo wa uwongo, waliofananishwa na magugu, wangetenganishwa na Wakristo wa kweli, waliofananishwa na ngano. (Mathayo 13:24-30, 36-43) Wakati huo, unabii kuhusu kazi ya kuhubiri habari njema ungetimizwa kwa njia kubwa zaidi. (Mathayo 24:14) Sehemu inayofuata katika mfululizo huu itazungumzia unabii huo wenye kusisimua.