Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Musa—Mtu Halisi au wa Hadithi?

Musa—Mtu Halisi au wa Hadithi?

MUSA alizaliwa wakati wa hatari. Familia yao ilikuwa kati ya familia ambazo zilihamia Misri pamoja na baba yao Yakobo, au Israeli, ili kuepuka njaa. Waliishi kwa amani na jirani zao Wamisri kwa miaka mingi. Lakini kukawa na badiliko lenye kuogopesha sana. Ripoti moja ya historia inayoheshimika inasema: “Mfalme mpya . . . akainuka juu ya Misri. Naye akawaambia watu wake: ‘Tazama! Watu wa wana wa Israeli ni wengi zaidi na wenye nguvu kuliko sisi. Haya! Na tuwatendee kwa werevu, wasije wakaongezeka.’” Wamisri walipanga kufanya nini? Kuwafanya Waisraeli kuwa “watumwa chini ya uonevu” ili wasiongezeke na kuwaamuru wazalishaji Waebrania kuwaua watoto wote wa kiume wanaozaliwa. (Kutoka 1:8-10, 13, 14) Licha ya dhuluma hiyo, Waisraeli waliongezeka kwa sababu ya ujasiri wa wazalishaji wao waliokataa kutii amri hiyo. Hivyo, mfalme wa Misri akaamuru: “Kila mwana anayezaliwa mtamtupa kwenye mto Nile.”—Kutoka 1:22.

Wenzi wawili Waisraeli, Amramu na Yokebedi, “hawakuliogopa agizo la mfalme.” (Waebrania 11:23) Yokebedi akamzaa mwana ambaye baadaye alisemwa kuwa “mwenye sura nzuri machoni pa Mungu.” * (Matendo 7:20) Huenda walitambua kwamba mtoto huyo alikuwa na kibali cha Mungu. Vyovyote vile, walikataa kumtoa mtoto wao auawe. Huku wakihatarisha uhai wao, waliamua kumficha.

Baada ya miezi mitatu, wazazi wa Musa hawangeweza kuendelea kumficha. Basi, waliamua kuchukua hatua. Yokebedi alimweka mtoto huyo katika safina ya mafunjo na kuiweka kwenye Mto Nile. Bila kujua, hatua hiyo ya Yokebedi ilimfanya Musa kuwa mtu maarufu katika historia!—Kutoka 2:3, 4.

Je, Matukio Hayo Ni ya Kweli?

Wasomi wengi leo husema kwamba matukio hayo ni hadithi tu. Gazeti Christianity Today linasema “ukweli ni kwamba hakuna uthibitisho wowote wa kiakiolojia unaoonyesha kwamba wana wa Israeli waliishi Misri kwa muda.” Ingawa hakuna uthibitisho wa moja kwa moja unaoonyesha jambo hilo, kuna uthibitisho mwingi usio wa moja kwa moja unaoonyesha kwamba simulizi hilo la Biblia ni la kweli. Katika kitabu chake Israel in Egypt, James K. Hoffmeier, mtaalamu wa vitu vya kale vya Misri, anasema: “Habari za kiakiolojia zinaonyesha kwamba watu wa upande wa mashariki wa Mediterania walitembelea Misri mara nyingi hasa kwa sababu ya ukame . . . Hivyo, kuanzia mwaka wa 1800 mpaka 1540 K.W.K. hivi, Wasemiti kutoka magharibi mwa Asia waliiona nchi ya Misri kuwa mahali pazuri pa kuhamia.”

Isitoshe, kwa muda mrefu imekubaliwa kwamba masimulizi ya Biblia kuhusu utumwa wa Waisraeli huko Misri ni sahihi. Kitabu Moses—A Life kinasema: “Masimulizi ya Biblia kuhusu kudhulumiwa kwa Waisraeli yanaungwa mkono na picha moja ya kaburi la Misri ya kale ambayo imechorwa mara nyingi inayoonyesha waziwazi kikundi cha watumwa kikitengeneza matofali.”

Masimulizi ya Biblia kuhusu safina ndogo ambayo Yokebedi alitumia ni ya kweli pia. Biblia inasema kwamba ilitengenezwa kwa mafunjo ambayo kulingana na kitabu Commentary cha Cook, “yalitumiwa sana na Wamisri kutengeneza mashua nyepesi zinazoenda mbio.”

Hata hivyo, je, kweli kiongozi wa nchi angeamuru watoto wachanga wauawe bila huruma? Msomi George Rawlinson anatukumbusha hivi: “Mauaji ya watoto . . . yametukia wakati na mahali mbalimbali, na yameonwa kuwa jambo dogo.” Ama kweli, hata katika nyakati zetu kumekuwa na mauaji ya watu wengi. Huenda simulizi la Biblia likahuzunisha, lakini ni la kweli kabisa.

Alelewa Nyumbani mwa Farao

Yokebedi hakuacha mtoto wake apotee tu. Aliiweka “[safina] katikati ya matete kando ya mto Nile.” Huenda aliiweka hapo kwa sababu alitarajia kwamba itagunduliwa. Huenda hapo ndipo binti ya Farao alipokuwa akioga kwa ukawaida. *Kutoka 2:2-4.

Safina hiyo ndogo iligunduliwa haraka. “[Binti ya Farao] alipoifungua akamwona yule mtoto, na tazama, mvulana huyo alikuwa akilia. Kwa hiyo akamwonea huruma, ingawa alisema: ‘Huyu ni mmoja wa watoto wa Waebrania.’” Binti huyo wa Mfalme wa Misri aliamua kumlea. Jina ambalo wazazi wake walimpa lilisahauliwa. Leo, anajulikana duniani pote kwa jina alilopewa na mama yake mlezi, yaani, Musa. *Kutoka 2:5-10.

Hata hivyo, je, haishangazi kwamba binti ya Mfalme wa Misri angemlea mtoto kama huyo? Sivyo, kwa kuwa dini ya Wamisri ilifundisha kwamba matendo ya fadhili yalikuwa takwa la kwenda mbinguni. Kuhusiana na hatua ya kumlea mtoto huyo, mwanaakiolojia Joyce Tyldesley anasema: “Wanawake Wamisri walikuwa na usawa na wanaume Wamisri. Walipaswa kuwa na haki sawa kisheria na kiuchumi, na . . . wanawake wangewalea watoto wa wengine.” Hati moja ya kale ya mafunjo inayohusu kuwalea watoto wa wengine inasema kuhusu mwanamke Mmisri aliyewalea watumwa wake. Kuhusu jinsi mama ya Musa alivyopewa kazi ya kumnyonyesha, kitabu The Anchor Bible Dictionary kinasema: “Mpango wa kumlipa mama ya Musa amtunze Musa . . . unafanana na mipango ya kuwalea watoto huko Mesopotamia.”

Kwa kuwa Musa alilelewa na mtu mwingine, je, angefichwa asili yake ya Kiebrania? Sinema fulani za Hollywood zimewafanya watu wafikiri hivyo. Hata hivyo, Maandiko yanasema tofauti. Kwa hekima, dada ya Musa, Miriamu, alipanga Musa alelewe na mama yake mwenyewe, Yokebedi. Bila shaka, mwanamke huyo mcha-Mungu angemweleza mwana wake ukweli kuhusu asili yake! Kwa kuwa watoto katika nyakati za kale walinyonyeshwa kwa miaka kadhaa, Yokebedi alikuwa na wakati wa kutosha kumfundisha Musa kumhusu ‘Mungu wa Abrahamu, Isaka, na Yakobo.’ (Kutoka 3:6) Msingi huo wa kiroho ulimsaidia Musa kwa sababu baada ya kupelekwa kwa binti ya Farao, “Musa akafundishwa hekima yote ya Wamisri.” Dai la mwanahistoria Josephus kwamba Musa alipanda cheo na kuwa jenerali katika vita dhidi ya Ethiopia haliwezi kuthibitishwa. Hata hivyo, Biblia inasema kwamba Musa “alikuwa mwenye nguvu katika maneno na matendo.” *Matendo 7:22.

Alipofikisha umri wa miaka 40, Musa angeweza kuwa mtawala mashuhuri wa Misri. Ikiwa angebaki nyumbani mwa Farao angepata mamlaka na utajiri. Kisha jambo fulani likatukia lililobadili maisha yake.

Akimbilia Midiani

Siku moja Musa ‘alimwona Mmisri fulani akimpiga Mwebrania fulani, mmoja wa ndugu zake.’ Kwa miaka mingi Musa alifurahia faida za kuwa Mwebrania na kuwa Mmisri. Lakini alipomwona Mwisraeli mwenzake akipigwa, labda kiasi cha kuuawa, Musa aliamua kuchukua hatua kubwa. (Kutoka 2:11) “Alikataa kuitwa mwana wa binti ya Farao, akachagua kutendewa vibaya pamoja na watu wa Mungu.”—Waebrania 11:24, 25.

Musa alichukua hatua ya haraka na ya kukata maneno: ‘Alimpiga Mmisri huyo na kumuua, halafu akamficha ndani ya mchanga.’ (Kutoka 2:12) Hilo halikuwa tendo la mtu “mwenye mazoea ya kukasirika haraka,” kama mhakiki mmoja alivyodai. Ingawa halikufaa, hilo lilikuwa tendo la imani kwamba Mungu angewakomboa Waisraeli kutoka Misri. (Mwanzo 15:13, 14) Labda kwa kukosa hekima, Musa aliamini kwamba matendo yake yangewachochea watu wake kuasi. (Matendo 7:25) Hata hivyo, alikata tamaa Waisraeli wenzake walipokataa uongozi wake. Farao alipopata habari kuhusu mauaji hayo, Musa alilazimika kukimbia. Alikimbilia Midiani, akamwoa mwanamke anayeitwa Sipora, binti ya Yethro, mkuu wa kabila la wahamaji.

Kwa miaka 40, Musa alikuwa mchungaji tu, na tumaini lake la kuwa mkombozi lilikuwa limedidimia. Hata hivyo, siku moja aliwapeleka kondoo wa Yethro karibu na Mlima Horebu. Akiwa hapo, malaika wa Yehova akamtokea Musa katika mti uliokuwa ukiwaka moto. Hebu wazia ilivyokuwa. Mungu anamwamuru: ‘Watoe watu wangu wana wa Israeli kutoka Misri.’ Lakini Musa anasitasita, hajiamini, na ana wasiwasi. Anauliza hivi: “Mimi ni nani hata niende kwa Farao, nikawatoe wana wa Israeli kutoka Misri?” Hata anafunua udhaifu wake ambao watengenezaji fulani wa sinema wameficha: Kwamba ana tatizo la kusema. Jinsi Musa alivyo tofauti na mashujaa wa hadithi za kale! Ile miaka 40 akiwa mchungaji ilimnyenyekeza. Ingawa Musa hajiamini, Mungu ana uhakika kwamba anafaa kuwa kiongozi!—Kutoka 3:1–4:20.

Kukombolewa Kutoka Misri

Musa anaondoka Midiani na kumwendea Farao, akitaka awaachilie watu wa Mungu. Mtawala huyo mkaidi anapokataa, nchi ya Misri inakumbwa na mapigo kumi makali. Pigo la kumi linawaua wazaliwa wa kwanza wa Misri, na Farao mwenye huzuni anawaachilia Waisraeli.—Kutoka, sura ya 5-13.

Watu wengi wanayajua matukio hayo. Lakini je, ni matukio ya kweli? Wengine wanadai kwamba kwa kuwa jina la Farao huyo halijatajwa, basi simulizi hilo si la kweli. * Hata hivyo, Hoffmeier, aliyenukuliwa awali, anasema kwamba mara nyingi waandishi Wamisri hawakuyataja majina ya adui za Farao kimakusudi. Anasema: “Wanahistoria hawawezi kusema kwamba Mfalme Thutmose wa 3 hakupigana huko Megido eti kwa sababu majina ya wafalme wa Kadeshi na Megido hayakutajwa.” Hoffmeier anasema kwamba Farao huyo hakutajwa “kwa sababu nzuri za kidini.” Sababu moja ni kwamba kwa kutotaja jina la Farao huyo, simulizi hilo linaelekeza uangalifu kwa Mungu, wala si kwa Farao.

Hata hivyo, wahakiki hawaamini kwamba Wayahudi wengi walitoka Misri. Msomi Homer W. Smith alisema kwamba uhamaji mkubwa kama huo “ungejulikana sana katika historia ya Misri au Siria . . . Yaelekea hadithi ya kuhama ni simulizi lililopotoshwa na la kuwaziwa la watu wachache waliokimbia kutoka Misri hadi Palestina.”

Ni kweli kwamba maandishi ya Kimisri kuhusu tukio hilo hayajapatikana. Lakini Wamisri wangeweza kubadilisha maandishi yao ya kihistoria yalipowaaibisha au kuhatarisha masilahi yao ya kisiasa. Thutmose wa 3 alipoanza kutawala, alijaribu kufuta maandishi yote kumhusu Hatshepsut, mtawala aliyemtangulia. Mtaalamu wa vitu vya kale vya Misri John Ray anasema: “Maandishi yake yalifutwa, piramidi zake zikazungushiwa ukuta, na sanamu zake za ukumbusho zikasahauliwa. Jina lake halipatikani katika maandishi ya baadaye.” Jitihada kama hizo za kufuta au kuficha mambo yenye kuaibisha zimefanywa katika nyakati za sasa.

Kwa kuwa Wayahudi walikuwa wanahamahama, hakuna uthibitisho wa kiakiolojia unaoonyesha maisha yao nyikani. Hawakujenga majiji wala kupanda mimea. Inaelekea kuna mambo machache yanayoonyesha kwamba waliishi huko. Hata hivyo, uthibitisho wa kutosha kuhusu maisha yao nyikani unaweza kupatikana katika Biblia. Kitabu hicho kitakatifu kinazungumzia sana maisha yao ya nyikani. (1 Samweli 4:8; Zaburi 78; Zaburi 95; Zaburi 106; 1 Wakorintho 10:1-5) Jambo muhimu ni kwamba Yesu Kristo pia alitoa ushahidi kwamba matukio ya nyikani yalifanyika.—Yohana 3:14.

Basi, bila shaka simulizi la Biblia kumhusu Musa ni la kweli kabisa. Lakini aliishi zamani sana. Je, Musa ana umuhimu wowote maishani mwako?

^ fu. 3 Kihalisi, “mzuri machoni pa Mungu.” Kulingana na The Expositor’s Bible Commentary, maneno hayo yanaweza kumaanisha “sifa za moyoni” za mtoto huyo, wala si sura ya nje tu.

^ fu. 11 Kitabu Commentary cha Cook kinasema kwamba “ilikuwa kawaida katika Misri ya kale” kuoga katika Mto Nile. “Mto Nile ulionwa kuwa . . . ulitokana na Osiris na maji yake yalionwa kuwa yenye nguvu za ajabu za kutokeza uhai na uzazi.”

^ fu. 12 Asili ya jina hilo imezua ubishi miongoni mwa wasomi. Katika Kiebrania, jina Musa linamaanisha “Kuchotwa; Kuokolewa Kutoka Majini.” Mwanahistoria Flavius Josephus alisema kwamba jina Musa limeundwa kwa maneno mawili ya Kimisri yanayomaanisha “maji” na “kuokolewa.” Leo vilevile, wasomi fulani wanaamini kwamba jina Musa ni la asili ya Kimisri lakini wanaona kwamba huenda linamaanisha “Mwana.” Hiyo ni kwa sababu neno “Musa” linatamkwa sawa na majina fulani ya Kimisri. Kwa kuwa hakuna anayejua jinsi Kiebrania au Kimisri cha kale kilivyotamkwa, dhana hizo ni za kukisia tu.

^ fu. 14 Kitabu Israel in Egypt kinasema: “Dhana ya kwamba Musa alilelewa katika jumba la kifalme la Misri inaonekana kuwa hadithi tu. Lakini uchunguzi wa makini wa jumba la kifalme wakati wa falme za kati ya mwaka wa 1550 mpaka 1070 K.W.K. hivi, hauungi mkono dhana hiyo. Mfalme Thutmose wa 3 . . . alianzisha zoea la kuwapeleka Misri wana wa wafalme vibaraka wa mataifa ya magharibi mwa Asia ili wazoezwe desturi za Misri . . . Hivyo, wana na binti za wafalme wa mataifa mengine walikuwapo katika jumba la kifalme la Misri.”

^ fu. 22 Wanahistoria fulani wanasema kwamba Farao aliyetawala wakati Waisraeli walipotoka Misri ni Thutmose wa 3. Wengine wanasema alikuwa Amenhotep wa 2, Ramses wa 2, na kadhalika. Kwa sababu ya mvurugo wa rekodi za ukoo za Misri, ni vigumu kujua kwa hakika jina la Farao huyo.