Hamia kwenye habari

MISTARI YA BIBLIA YAFAFANULIWA

Zaburi 46:10​—“Acheni, Mjue ya Kuwa Mimi Ni Mungu”

Zaburi 46:10​—“Acheni, Mjue ya Kuwa Mimi Ni Mungu”

 “Salimuni amri na mjue kwamba mimi ni Mungu. Nitakwezwa miongoni mwa mataifa; nitakwezwa duniani.”​—Zaburi 46:10, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

 “Acheni, mjue ya kuwa Mimi ni Mungu, nitakuzwa katika mataifa, nitakuzwa katika nchi.”​—Zaburi 46:10, Union Version.

Maana ya Zaburi 46:10

 Mungu anawahimiza watu wote wamwabudu na kutambua haki yake ya kuitawala dunia. Hakuna anayeweza kupinga nguvu na mamlaka yake, na hilo ni jambo ambalo mtu yeyote anayetaka kuishi milele anapaswa kukubali.​—Ufunuo 4:11.

 “Salimuni amri na mjue kwamba mimi ni Mungu.” Tafsiri fulani za Biblia zinatafsiri sehemu ya kwanza ya sentensi hiyo kuwa “tulieni.” Hilo limewafanya watu wengi wafikirie kimakosa kwamba hii ni amri ya kuketi kwa heshima au kimya wanapokuwa kanisani. Hata hivyo, maneno ya Kiebrania “salimuni amri na mjue kwamba mimi ni Mungu” ni himizo kutoka kwa Yehova a Mungu mwenyewe kwa watu wa mataifa yote. Anawahimiza waache kumpinga na watambue kwamba yeye tu ndiye anayestahili kuabudiwa.

 Himizo kama hilo linapatikana katika Zaburi 2. Hapo, Mungu anaahidi kuchukua hatua dhidi ya wale wanaompinga. Kwa upande mwingine, wale wanaotambua mamlaka ya Mungu wanamtegemea ili kupata mwongozo, nguvu, na hekima. ‘Wanapomkimbilia Yeye,’ wanapata furaha na usalama, hasa katika nyakati ngumu.​—Zaburi 2:9-12.

 “Nitakwezwa miongoni mwa mataifa; nitakwezwa duniani.” Zamani, Yehova Mungu alikwezwa alipotumia nguvu zake kuu kuwalinda watu wake. (Kutoka 15:1-3) Wakati ujao, atakwezwa kwa njia kubwa hata zaidi wakati ambapo kila mtu duniani atajitiisha kwa mamlaka yake na kumwabudu.​—Zaburi 86:9, 10; Isaya 2:11.

Muktadha wa Zaburi 46:10

 Kitabu kimoja cha marejeo kinaita Zaburi 46 “wimbo wa kutukuza nguvu za Mungu, mlinzi jasiri wa watu wake.” Watu wa Mungu walipoimba Zaburi 46, walionyesha kwamba wanatumaini uwezo wa Yehova wa kuwalinda na kuwasaidia. (Zaburi 46:1, 2) Maneno hayo yaliwakumbusha kwamba Yehova alikuwa pamoja nao sikuzote.​—Zaburi 46:7, 11.

 Ili kuimarisha tumaini lao katika nguvu za Yehova Mungu za kuwalinda, zaburi hiyo iliwaalika watafakari kazi zake zenye nguvu. (Zaburi 46:8) Zaburi hiyo ilielekeza fikira zao hasa kwenye uwezo wake wa kukomesha vita. (Zaburi 46:9) Kwa njia fulani, Yehova alikomesha vita katika nyakati za Biblia kwa kuwalinda watu wake dhidi ya mataifa adui. Hata hivyo, Biblia inaahidi kwamba hivi karibuni Mungu atafanya hivyo kwa njia kubwa zaidi atakapokomesha vita duniani kote.​—Isaya 2:4.

 Je, bado Yehova anawasaidia waabudu wake leo? Ndiyo. Kwa kweli, mtume Paulo aliwatia moyo Wakristo waendelee kumtegemea Yehova ili kupata msaada. (Waebrania 13:6) Mawazo yaliyo katika Zaburi 46 yanaimarisha tumaini letu katika nguvu za Mungu za kutulinda. Yanatusaidia kumwona Mungu akiwa “kimbilio letu na nguvu zetu.”​—Zaburi 46:1.

 Tazama video hii fupi uone muhtasari wa kitabu cha Zaburi.

a Yehova ni jina la kibinafsi la Mungu. (Zaburi 83:18) Ona makala yenye kichwa “Yehova Ni Nani?”