Hamia kwenye habari

MISTARI YA BIBLIA YAFAFANULIWA

Yeremia 33:3—“Niite, Nami Nitakuitikia”

Yeremia 33:3—“Niite, Nami Nitakuitikia”

 “Niite, nami nitakujibu na kukuambia kwa utayari mambo makubwa na yasiyoeleweka ambayo hujayajua.”​—Yeremia 33:3, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

 “Niite, nami nitakuitikia, nami nitakuonyesha mambo makubwa, magumu usiyoyajua.”​—Yeremia 33:3, Union Version.

Maana ya Yeremia 33:3

 Kupitia maneno hayo, Mungu aliwaalika watu wasali kwake. Ikiwa wale waliosikia mwaliko wake wangeukubali na kusali kwake, Mungu angewafunulia mambo ambayo yangetokea wakati ujao.

 “Niite, nami nitakujibu.” Neno “niite” halimaanishi tu kupaza sauti au kuliita jina la Mungu kwa sauti. Badala yake, katika mstari huu linamaanisha kutafuta msaada na mwongozo wa Mungu kupitia sala.​—Zaburi 4:1; Yeremia 29:12.

 Inaonekana kwamba mwaliko huo ulitolewa kwa taifa la kale la Israeli. Taifa hilo lilikuwa limemwasi Mungu, na sasa lilikuwa likishambuliwa na jeshi la Babiloni. (Yeremia 32:1, 2) Yehova a aliwaalika Waisraeli wamrudie kwa kumwita kupitia sala.

 “[Nitakuambia] kwa utayari mambo makubwa na yasiyoeleweka ambayo hujayajua.” Mambo ambayo Mungu anaahidi kuyafunua ‘hayaeleweki’ (au, hayapatikani) katika maana ya kwamba wanadamu hawawezi kuyaelewa bila msaada. Maneno “mambo . . . yasiyoeleweka” yanaweza pia kutafsiriwa “mambo yaliyofichika.”

 Ni ‘mambo gani yaliyofichika’ ambayo Mungu angefunua? Mambo ambayo yangetendeka wakati ujao, yaani, kwamba jiji la kale la Yerusalemu lingeharibiwa na kuachwa likiwa magofu, na pia kwamba baadaye lingerudishwa. (Yeremia 30:1-3; 33:4, 7, 8) Hata hivyo, Mungu alitangaza pia kwamba waabudu wake hawangeangamizwa wote wakiwa taifa.​—Yeremia 32:36-38.

Muktadha wa Yeremia 33:3

 Nabii Yeremia alipokea ujumbe huo kutoka kwa Yehova mwaka wa 608 K.W.K., katika mwaka wa kumi wa utawala wa Mfalme Sedekia. Yeremia alitabiri kwamba Yerusalemu lingeanguka na kwamba Sedekia angepelekwa utekwani. Kwa kuwa mfalme huyo hakupenda ujumbe huo, aliamuru Yeremia afungwe.​—Yeremia 32:1-5; 33:1; 37:21.

 Mambo hayo yalipokuwa yakitendeka ndipo Mungu alitoa mwaliko unaopatikana kwenye Yeremia 33:3. Kwa kusikitisha, Mfalme Sedekia na watu wengi katika taifa hilo waliendelea kuasi. (Yeremia 7:26; 25:4) Hawakumwita Mungu na kutafuta mwongozo wake. Mwaka mmoja baadaye, Sedekia alipoteza mamlaka yake, Yerusalemu likaharibiwa, na wengi kati ya waokokaji wakakamatwa na kupelekwa Babiloni.​—Yeremia 39:1-7.

 Maneno ya Yeremia 33:3 yanawakumbusha wasomaji leo kwamba Mungu anaweza kuandaa “ujuzi sahihi wa mapenzi yake” na kuwafunulia “mambo mazito” wale wanaosali kwake na kujifunza Neno lake, Biblia. (Wakolosai 1:9; 1 Wakorintho 2:10) Mambo hayo mazito yanatia ndani mambo ambayo Mungu anaahidi kufanya hivi karibuni.​—Ufunuo 21:3, 4.

 Tazama video hii fupi inayoonyesha muhtasari wa kitabu cha Yeremia.

a Yehova ni jina la kibinafsi la Mungu. (Zaburi 83:18) Ona makala yenye kichwa “Yehova Ni Nani?”