Hamia kwenye habari

Jinsi ya Kusali​—Je, Kukariri Sala ya Bwana Ndiyo Njia Bora Zaidi ya Kusali?

Jinsi ya Kusali​—Je, Kukariri Sala ya Bwana Ndiyo Njia Bora Zaidi ya Kusali?

Jibu la Biblia

 Sala ya Bwana inatupatia mwongozo wa jinsi ya kusali na mambo tunayopaswa kusali kuyahusu. Yesu aliwafundisha wanafunzi wake sala hiyo baada ya wao kumwambia hivi: “Bwana, tufundishe jinsi ya kusali.” (Luka 11:1) Hata hivyo, Sala ya Bwana, au sala ya Baba Yetu, si sala pekee ambayo Mungu anakubali. a Yesu aliitoa kama kielelezo cha sala ambazo Mungu anakubali.

Katika makala hii

 Sala ya Bwana ni sala ipi?

 Sala ya Bwana, iliyorekodiwa kwenye Mathayo 6:9-13 imeandikwa kwa njia tofauti katika tafsiri mbalimbali za Biblia. Ona mifano miwili.

 Tafsiri ya Ulimwengu Mpya: “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe. Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni. Utupatie leo mkate wetu kwa ajili ya siku hii; na utusamehe madeni yetu, kama vile tunavyowasamehe wadeni wetu. Na usituingize katika majaribu, bali utukomboe kutoka kwa yule mwovu.”

 Union Version: “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litukuzwe. Ufalme wako uje. Mapenzi yako yatimizwe hapa duniani kama huko mbinguni. Utupate leo riziki yetu. Utusamehe deni zetu, kama sisi nasi tuwasamehevyo wadeni wetu. Na usitutie majaribuni, lakini utuokoe na yule mwovu.” b

 Ni nini maana ya sala ya Bwana?

 Mafundisho ya Yesu yanapatana na Maandiko yote, hivyo tunaweza kutarajia sehemu nyingine za Biblia zitusaidie kuielewa Sala ya Bwana.

“Baba yetu uliye mbinguni”

 Inafaa kumwita Mungu, “Baba yetu” kwa sababu alituumba na akatupatia uhai.​—Isaya 64:8.

“Jina lako na litakaswe”

 Jina la Mungu, Yehova, linapaswa kuheshimiwa na kutukuzwa. Wanadamu wanashiriki katika kutakasa jina la Mungu wanapozungumzia sifa zake na kuwajulisha wengine mapenzi yake.​—Zaburi 83:18; Isaya 6:3.

“Ufalme wako na uje”

 Ufalme wa Mungu ni serikali ya mbinguni na Mfalme wake ni Yesu. Yesu alitufundisha tusali kwamba serikali hiyo itawale dunia yote.​—Danieli 2:44; Ufunuo 11:15.

“Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni”

 Kama vile tu hakuna uovu au kifo mbinguni, Mungu anapenda wanadamu waishi milele duniani kwa amani na usalama.​—Zaburi 37:11, 29.

“Utupatie leo mkate wetu kwa ajili ya siku hii”

 Katika siku za Yesu, mkate ulipatikana kwa urahisi na ulitumiwa na kila mtu. Tunapaswa kukumbuka kwamba tunamtegemea Muumba wetu kupata vitu tunavyohitaji ili tuendelee kuishi.​—Matendo 17:24, 25.

“Utusamehe madeni yetu, kama vile tunavyowasamehe wadeni wetu”

 Katika muktadha huu neno “madeni” linarejelea dhambi. (Luka 11:4) Wanadamu wote hutenda dhambi na wanahitaji kusamehewa. Lakini ikiwa, tunataka Mungu atusamehe lazima tuwe tayari kuwasamehe wengine wanapotukosea.​—Mathayo 6:14, 15.

“Usituingize katika majaribu, bali utukomboe kutoka kwa yule mwovu”

 Yehova Mungu hatuletei majaribu kamwe. (Yakobo 1:13) Lakini tunajaribiwa na “yule mwovu,” Shetani Ibilisi ambaye pia anaitwa “Mjaribu.” (1 Yohana 5:19; Mathayo 4:1-4) Tunamwomba Yehova atusaidie tuwe watiifu kwake tunapojaribiwa na mambo mabaya.

 Je, kukariri Sala ya Bwana ndio njia pekee ya kusali?

 Yesu alitoa Sala ya Bwana kama kielelezo. Haikukusudiwa ikaririwe neno kwa neno. Kabla tu ya kutoa Sala ya Bwana, Yesu alionya hivi: “Mnaposali msiseme mambo yaleyale tena na tena.” (Mathayo 6:7) Pindi nyingine alipofundisha sala ya kielelezo alitumia maneno tofauti.​—Luka 11:2-4.

 Njia bora zaidi ya kusali ni kumweleza Mungu mawazo na hisia zetu kwa unyoofu.​—Zaburi 62:8.

 Tunapaswa kusali jinsi gani?

 Sala ya Bwana ni kielelezo kizuri cha jinsi ya kusali katika njia ambayo Mungu atasikiliza. Ona jinsi inavyopatana na mistari mingine ya Biblia inayozungumza kuhusu sala.

  •   Sali kwa Mungu peke yake

     Andiko: “Msihangaike kuhusiana na jambo lolote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani, mjulisheni Mungu maombi yenu.”​—Wafilipi 4:6.

     Maana: Sala zetu zinapaswa kuelekezwa kwa Mungu si kwa Yesu, Maria, au watakatifu. Sala ya Bwana inaanza kwa maneno “Baba yetu uliye mbinguni,” hivyo, inatufundisha tusali kwa Yehova Mungu tu.

  •   Sali kuhusu mambo yanayopatana na mapenzi ya Mungu

     Andiko: “Tukiomba chochote kulingana na mapenzi yake, yeye hutusikia.”​—1 Yohana 5:14.

     Maana: Tunaweza kusali kuhusu jambo lolote linalopatana na mapenzi ya Mungu. Yesu alifundisha jinsi mapenzi ya Mungu yalivyo muhimu kwa kutia ndani maneno haya katika Sala ya Bwana: “Mapenzi yako na yatendeke.” Tunapojifunza Biblia tunaweza kujua mapenzi ya Mungu kwa ajili ya dunia na wanadamu.

  •   Sali kuhusu mambo yanayokuhangaisha

     Andiko: “Mtupie Yehova mzigo wako, naye atakutegemeza.”​—Zaburi 55:22.

     Maana: Mungu anajali kuhusu mambo yanayotuhangaisha. Kama vile Yesu alivyotaja masuala kadhaa ya kibinafsi katika Sala ya Bwana, sisi pia tunaweza kusali kwa ajili ya mahitaji yetu ya kimwili ya kila siku, mwongozo wake tunapofanya maamuzi muhimu, utegemezo tunapokuwa na matatizo, na msamaha kwa ajili ya dhambi zetu. c

a Kwa mfano, Yesu na wanafunzi wake walitoa sala nyingine zilizokuwa tofauti na sala hiyo ya kielelezo.​—Luka 23:34; Wafilipi 1:9.

b Tafsiri ya Union Version inamalizia Sala ya Bwana kwa maneno: “Kwa kuwa ufalme ni wako, na nguvu, na utukufu, hata milele. Amina.” Maneno haya ya kumsifu Mungu yanapatikana pia kwenye Biblia nyingine. Hata hivyo, kitabu The Jerome Biblical Commentary kinasema hivi: “Maneno hayo ya kumsifu Mungu . . . hayapatikani katika [hati] zenye kutegemeka zaidi.”

c Watu wanaohisi kwamba wanahitaji msamaha wa Mungu wanaweza kujihisi wana hatia na hivyo wanashindwa kusali. Lakini Yehova anawasihi hivi: “Tunyooshe mambo kati yetu.” (Isaya 1:18) Mtu akiomba kwa unyenyekevu asamehewe, Yehova hatakataa kumsamehe.