Hamia kwenye habari

MISTARI YA BIBLIA YAFAFANULIWA

Methali 22:6—“Mlee Mtoto Katika Njia Impasayo”

Methali 22:6—“Mlee Mtoto Katika Njia Impasayo”

 “Mzoeze mvulana njia anayopaswa kuifuata; hata atakapozeeka hataiacha.”​—Methali 22:6, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

 “Mlee mtoto katika njia impasayo, naye hataiacha, hata atakapokuwa mzee.”​—Mithali 22:6, Union Version.

Maana ya Methali 22:6

 Wazazi wanaowafundisha watoto wao kumpenda Mungu na kuheshimu sheria zake wanaweza kutarajia kwamba mazoezi hayo yatawasaidia watoto wao maisha yao yote.

 “Mzoeze mvulana njia anayopaswa kuifuata.” Maneno hayo yanaweza pia kutafsiriwa “mwanzishe mtoto kwenye barabara inayofaa.” Kitabu cha Methali kinawasihi wazazi tena na tena wawafundishe watoto wao kuhusu mema na mabaya wakiwa wachanga. (Methali 19:18; 22:15; 29:15) Hata hivyo, wazazi wenye upendo wanatambua kwamba kama tu watu wazima, watoto wao pia wana uhuru wa kuchagua. Kwa hiyo, badala tu ya kuwaambia watoto mambo ya kufanya, wanazungumza nao ili kuwaelewesha na kuwasaidia kukua wawe watu wazima wakomavu na wanaowajibika wanaoweza kujifanyia maamuzi mazuri.​—Kumbukumbu la Torati 6:6, 7; Wakolosai 3:21.

 Wasomi fulani wa Biblia wanasema kwamba maneno hayo yanamaanisha “mzoeze mtoto kulingana na utu wake,” au kulingana na mwelekeo wake. Huenda ufafanuzi huo ukaonekana kuwa unafaa, hata hivyo, inaonekana maneno ya Kiebrania yaliyotafsiriwa “njia anayopaswa kuifuata” yanarejelea njia ya maisha ambayo ni nzuri na ya uadilifu. Kitabu cha Methali kinaonyesha njia mbili ambazo mtu anaweza kufuata. Moja inaitwa “njia ya watu wema,” “njia ya hekima,” na “njia inayofaa.” (Methali 2:20; 4:11; 23:19) Njia ile nyingine inaitwa “njia ya watu wabaya,” “njia ya mpumbavu,” na “njia isiyofaa.” (Methali 4:14; 12:15; 16:29) Hivyo, njia ambayo mtoto ‘anapaswa kuifuata’ inarejelea “njia inayofaa,” yaani, njia ya maisha inayofundishwa katika Neno la Mungu, Biblia.​—Zaburi 119:105.

 “Hata atakapozeeka hataiacha.” Wazazi wanapomfundisha mtoto wao viwango vya Mungu vya maadili, kuna uwezekano mkubwa kwamba atabaki kwenye njia inayofaa maisha yake yote. Hata hivyo, hilo halimaanishi kwamba mtoto anayezoezwa vizuri hatawahi kamwe ‘kuiacha’ njia inayofaa, yaani, hatawahi kuasi sheria za Mungu. Kwa mfano, mtu anapotumia wakati na watu wanaowachochea wengine kutenda mabaya, huenda akaacha “vijia vya unyoofu” na kutenda mabaya. (Methali 2:12-16; 1 Wakorintho 15:33) Hata hivyo, wazazi wanapowazoeza watoto wao kufuata viwango vya Mungu, wanawapa nafasi bora ya kufanikiwa maishani.​—Methali 2:1, 11.

Muktadha wa Methali 22:6

 Methali sura ya 22 imefanyizwa na sentensi fupifupi zinazotusaidia kutumia hekima ya Mungu katika hali mbalimbali maishani. Maneno hayo yanakazia umuhimu wa kuwa na jina jema mbele za Yehova, a jambo ambalo mtu anaweza kujipatia kwa kuonyesha unyenyekevu, ukarimu, na bidii. (Methali 22:1, 4, 9, 29) Tofauti na hilo, mistari mingine inaonyesha kwamba wale wanaopuuza viwango vya Mungu na kuwadhulumu maskini watapatwa na madhara.​—Methali 22:8, 16, 22-27.

 Ingawa mistari mingi katika Methali sura ya 22 hairejelei kumzoeza mtoto, inafafanua njia ya maisha inayoongoza kwenye kibali cha Mungu na furaha ya kweli. (Methali 22:17-19) Wazazi wanapowazoeza watoto wao kuifuata njia hiyo ya maisha, wanaonyesha kwamba wanawatakia watoto wao maisha bora kabisa.​—Waefeso 6:1-3.

 Tazama video hii fupi ili upate habari zaidi kuhusu kitabu cha Methali.

a Yehova ni jina la kibinafsi la Mungu. (Zaburi 83:18) Ona makala yenye kichwa “Yehova Ni Nani?