Hamia kwenye habari

MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | KULEA WATOTO

Jinsi ya Kuwa Baba Mzuri

Jinsi ya Kuwa Baba Mzuri

 Baba ana jukumu gani?

  •   Kabla ya mtoto wako kuzaliwa. Jinsi unavyomtendea mke wako sasa, kunafunua jinsi utakavyowatendea watoto wako baadaye. Kitabu Do Fathers Matter? kinasema hivi:

     “Ikiwa mwanamume atamsaidia mwenzi wake mjamzito kufanya ununuzi, atamsindikiza hospitalini kumwona daktari, na atamwona mtoto wake akiwa bado kijusi tumboni au hata kusikiliza mapigo ya moyo wake, kuna uwezekano mkubwa kwamba atajihusisha na kushirikiana zaidi na mwenzi wake katika malezi ya mtoto wao.”

     “Sikutaka mke wangu ahisi kana kwamba anapitia kipindi cha ujauzito peke yake, kwa hiyo nilimsaidia kwa njia yoyote niliyoweza. Hata tulipanga chumba cha mtoto wetu pamoja. Tulikuwa na wakati mzuri tulipokuwa tukifanya matayarisho huku tukimsubiri mtoto wetu.”​—James.

     Kanuni ya Biblia: “Mkiangalia, si faida zenu wenyewe, bali pia faida za wengine.”​—Wafilipi 2:4.

  •   Baada ya mtoto wako kuzaliwa. Unaweza kujenga uhusiano mzuri na mtoto wako kwa kucheza naye na pia kumbeba. Ni muhimu kwako kushiriki katika kazi ya kumtunza mtoto. Kujihusisha katika kazi hiyo ukiwa baba kutachangia maendeleo na ukuzi wa mtoto wako. Unapojenga uhusiano mzuri na mtoto wako unaonyesha kwamba unamthamini sana.

     “Jishushe. Cheza naye. Mchekeshe. Ukifanya mambo hayo hujidhalilishi. Kumbuka kwamba masomo ya kwanza ambayo mtoto wako anapata kuhusu upendo ni kupitia upendo unaomwonyesha ukiwa mzazi.”​—Richard.

     Kanuni ya Biblia: “Watoto ni urithi kutoka kwa Yehova; uzao wa tumbo ni thawabu.”​—Zaburi 127:3.

  •   Kadiri mtoto wako anavyokua. Utafiti unaonyesha kwamba watoto ambao wana uhusiano wa karibu na baba zao wanafaulu zaidi shuleni, hawakabili matatizo mengi ya kihisia, na wanakuwa na uwezekano mdogo zaidi wa kutumia dawa za kulevya au kujihusisha katika uhalifu. Tenga muda wa kutosha ili kujenga uhusiano mzuri na mtoto wako.

     “Mtoto wangu wa kiume aliniambia kwamba atakapohama nyumbani kitu atakachokosa zaidi ni pindi tulizozungumza pamoja kwa muda mrefu kwenye gari au wakati wa mlo wa jioni. Wakati fulani tulijipata tu tukizungumza hata kuhusu mambo muhimu sana bila kutazamia. Tulifaulu kuzungumzia mambo hayo kwa sababu tulitumia muda mwingi pamoja.”​—Dennis.

     Kanuni ya Biblia: “Endeleeni kuangalia sana jinsi mnavyotembea, si kama watu wasio na hekima bali kama watu wenye hekima, mkiutumia vizuri kabisa wakati wenu.”​—Waefeso 5:15, 16.

 Kwa nini jukumu la baba ni la pekee?

 Kwa kawaida, watu wengi wanatazamia akina baba wataiandalia familia mahitaji ya kimwili na ulinzi, na akina mama wanatazamiwa kushughulikia hali ya kihisia ya washiriki wa familia. (Kumbukumbu la Torati 1:31; Isaya 49:15) Katika baadhi ya familia, mama anaweza kutimiza baadhi ya majukumu ya baba au baba anaweza kutimiza baadhi ya majukumu ya mama. Hata hivyo, watafiti wanasema kwamba wazazi wote wawili wanachangia kwa njia ya pekee katika malezi ya watoto wao. a

 Mtafiti mmoja wa masuala ya kifamilia anayeitwa Judith Wallerstein alisema amejionea ukweli wa jambo hilo maishani mwake. Aliandika hivi: “Binti yangu mwenye umri wa miaka kumi na miwili alipogongwa na gari, alitaka baba yake awe pamoja naye katika ambulansi kwa sababu alikuwa na uhakika kwamba baba yake anaweza kumlinda katika hali hiyo. Baadaye, alipokuwa amelazwa hospitalini, alitaka mimi nikae karibu naye muda wote ili kumfariji.” b

 “Baba ana uwezo wa kulinda familia na kuifanya iwe imara lakini huenda ikawa vigumu kwa mama kufanya hivyo akiwa peke yake. Kwa upande mwingine, mama ana uwezo wa kuwafanya watoto wahisi wanapendwa kwa jinsi anavyowasikiliza na kuwaonyesha hisia-mwenzi. Wazazi wote wawili hushirikiana kujenga familia.”​—Daniel.

 Kanuni ya Biblia: “Mwanangu, sikiliza nidhamu ya baba yako, wala usiyaache mafundisho ya mama yako.”​—Methali 1:8.

 Akina baba na binti zao

 Mfano ambao unamwekea binti yako ukiwa baba utamfundisha anapaswa kutarajia kutendewa jinsi gani na wanaume. Atajifunza hilo kupitia njia hizi mbili:

  •   Kwa kutazama jinsi unavyomtendea mama yake. Unapompenda na kumheshimu mke wako, binti yako anajifunza sifa ambazo anapaswa kutafuta atakapochagua mume baadaye.​—1 Petro 3:7.

  •   Kwa kutazama jinsi unavyomtendea. Unapoonyesha kwamba unamheshimu binti yako, unamfundisha kujiheshimu yeye mwenyewe. Isitoshe, anajifunza kwamba wanaume wengine wanapaswa kumtendea kwa njia hiyo.

     Kinyume na hilo, baba anapomkosoa binti yake kila mara, binti huyo anaweza kuhisi kuwa hana thamani na hilo linaweza kumchochea kutafuta upendo kutoka kwa wanaume wengine, na huenda wanaume hao wakawa na nia mbaya.

     “Kuna uwezekano mdogo sana kwa binti anayeona jinsi baba yake anavyompenda na kumjali kuvutiwa na mwanamume ambaye hana sifa za kuwa mume mzuri.”​—Wayne.

a Mama wengi wamewalea watoto wao bila msaada wa mume.

b Kutoka kwenye kitabu The Unexpected Legacy of Divorce.