Hamia kwenye habari

MISTARI YA BIBLIA YAFAFANULIWA

Mathayo 6:33​—“Kuutafuta Kwanza Ufalme wa Mungu”

Mathayo 6:33​—“Kuutafuta Kwanza Ufalme wa Mungu”

 “Basi, endeleeni kuutafuta kwanza Ufalme na uadilifu wake, nanyi mtaongezewa hivi vitu vingine vyote.”—Mathayo 6:33, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

 “Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa.”—Mathayo 6:33, Union Version.

Maana ya Mathayo 6:33

 Ufalme wa Mungu ni serikali iliyo mbinguni ambayo itatimiza mapenzi ya Mungu duniani. (Mathayo 6:9, 10) Mtu huutafuta kwanza Ufalme kwa kuufanya kuwa jambo kuu maishani mwake. a Hilo linatia ndani si tu kuwa na hamu ya kujifunza kuhusu Ufalme wa Mungu bali pia kuwaambia wengine kuhusu mambo mazuri utakayotimiza. (Mathayo 24:14) Mtu anayetafuta Ufalme husali ili uje.—Luka 11:2.

 Uadilifu wa Mungu unatia ndani viwango vyake kuhusu mwenendo mzuri na mbaya. (Zaburi 119:172) Hivyo, mtu hutafuta uadilifu wa Mungu kwa kuishi kulingana na sheria za maadili zilizowekwa na Mungu, ambazo mara zote ni zenye faida.—Isaya 48:17.

 Maneno nanyi mtaongezewa hivi vitu vingine vyote, ni ahadi kutoka kwa Mungu kwamba atawapa mahitaji yao wale wote wanaoutanguliza Ufalme wa Mungu na viwango vyake maishani mwao.—Mathayo 6:31, 32.

Muktadha wa Mathayo 6:33

 Yesu alisema maneno hayo katika mahubiri yake ya Mlimani yanayopatikana katika Mathayo sura ya 5-7. Bila shaka, wasikilizaji wa Yesu walikuwa maskini. Huenda walihisi kwamba walihitaji hasa kutanguliza kutafuta riziki, na walitumia wakati mdogo kuutafuta Ufalme. Hata hivyo, Yesu aliwatia moyo wachunguze jinsi Mungu anavyotunza miti na wanyama aliowaumba. Mungu anaahidi kuwatunza vivyo hivyo wale wanaotafuta kwanza Ufalme wake.—Mathayo 6:25-30.

Maoni Yasiyo Sahihi Kuhusu Mathayo 6:33

 Maoni yasiyo sahihi: Mtu anayeutafuta Ufalme atakuwa tajiri.

 Ukweli: Yesu alisema kwamba wale wanaoutanguliza Ufalme wa Mungu watapata mahitaji yao, kama vile chakula na mavazi. (Mathayo 6:25, 31, 32) Hata hivyo, hakuahidi kwamba watapewa mali, au kuonyesha kwamba baraka za Mungu zinaweza kupimwa kupitia utajiri wa kimwili. Kwa kweli, Yesu hata aliwaonya wasikilizaji wake dhidi ya kutafuta utajiri, jambo linaloweza kufanya iwe vigumu zaidi kuutafuta kwanza Ufalme. (Mathayo 6:19, 20, 24) Ijapokuwa mtume Paulo alifanya kazi kwa bidii kwa ajili ya Ufalme wa Mungu, nyakati nyingine alipungukiwa na mahitaji ya kimwili. Kama Yesu, aliwaonya wengine kuhusu hatari ya kujitahidi kupata utajiri.—Wafilipi 4:11, 12; 1 Timotheo 6:6-10.

 Maoni yasiyo sahihi: Wakristo hawahitaji kufanya kazi ili kupata riziki.

 Ukweli: Biblia inasema kwamba Wakristo wanapaswa kufanya kazi kwa ajili ya kujitegemeza wao na familia zao. (1 Wathesalonike 4:11, 12; 2 Wathesalonike 3:10; 1 Timotheo 5:8) Yesu hakusema kwamba wafuasi wake wanapaswa kuutafuta tu Ufalme; badala yake alisema kwamba walipaswa kuutafuta kwanza Ufalme.

 Wale wanaoutafuta kwanza Ufalme wa Mungu na wanafanya kazi ili kujiruzuku, wanaweza kuwa na uhakika kwamba Mungu atawasaidia kupata mahitaji yao ya msingi.—1 Timotheo 6:17-19.

a Maneno “endeleeni kuutafuta” yametafsiriwa kutoka kitenzi cha Kigiriki kinachomaanisha tendo linaloendelea, na usemi huo unaweza kutafsiriwa “endelea kutafuta.” Hivyo, Ufalme unapaswa kuwa jambo la kwanza wala si upendezi wa muda mfupi au usiodumu.