Hamia kwenye habari

Inamaanisha Nini “Kuwapenda Adui” Zetu?

Inamaanisha Nini “Kuwapenda Adui” Zetu?

Jibu la Biblia

 Katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu alisema hivi: “Endeleeni kuwapenda adui zenu.” (Mathayo 5:44; Luka 6:27, 35) Maneno haya yanamaanisha tunapaswa kuwatendea kwa upendo wale wanaotuchukia au kututendea kwa ukosefu wa haki.

 Yesu aliwaonyesha upendo maadui wake kwa kuwasamehe wale waliomtendea kwa njia isiyofaa. (Luka 23:33, 34) Mafundisho yake kuhusu kuwapenda maadui wetu yanapatana na mambo yanayozungumziwa katika Maandiko ya Kiebrania, ambayo kwa kawaida yanajulikana kama Agano la Kale.​—Kutoka 23:4, 5; Methali 24:17; 25:21.

 “Endeleeni kuwapenda adui zenu na kusali kwa ajili ya wale wanaowatesa ninyi.”​—Mathayo 5:43, 44.

Katika makala hii

 Kwa nini uwapende adui zako?

  •   Mungu anatuwekea mfano. Mungu “huwaonyesha fadhili hata watu wasio na shukrani na waovu.” (Luka 6:35) Yeye “huwaangazia jua lake waovu.”​—Mathayo 5:45.

  •   Upendo unaweza kumchochea adui kubadilika. Biblia inapendekeza kwamba tumtendee adui kwa fadhili, na inasema tunapofanya hivyo, ‘tutakuwa tunakusanya makaa ya mawe yanayowaka juu ya kichwa chake.’ (Methali 25:22) Maneno hayo ya mfano yanarejelea kazi ya kupitisha chuma kwenye moto ili kupata madini. Vivyo hivyo, tukimwonyesha fadhili mtu anayetuchukia, huenda tukayeyusha hasira yake na kutokeza sifa zake nzuri.

 Ni zipi baadhi ya njia za kuwapenda adui zako?

  •   ‘Watendee mema wale wanaokuchukia.’ (Luka 6:27) Biblia inasema hivi: “Ikiwa adui yako ana njaa, mlishe; ikiwa ana kiu, mpe kitu anywe.” (Waroma 12:20) Huenda ukapata njia nyingine za kuonyesha unampenda adui yako kwa kutumia ile inayoitwa Kanuni Bora, inayosema: “Kama vile mnavyotaka watu wawatendee ninyi, watendeeni vivyo hivyo.”​—Luka 6:31.

  •   “Wabariki wale wanaokulaani.” (Luka 6:28) Tunawabariki adui zetu kwa kuzungumza nao kwa fadhili na ufikirio hata wanapotutukana. Biblia inasema hivi: “Msilipe . . . matukano kwa matukano. Badala yake, lipeni kwa baraka.” (1 Petro 3:9) Ushauri huo unaweza kutusaidia kushinda chuki.

  •   ‘Sali kwa ajili ya wale wanaokutukana.’ (Luka 6:28) Mtu anapokutukana, usimlipe “uovu kwa uovu.” (Waroma 12:17) Badala yake, mwombe Mungu amsamehe mtu huyo. (Luka 23:34; Matendo 7:59, 60) Badala ya kulipiza kisasi, mwachie Mungu ashughulikie mtu huyo kulingana na kiwango Chake kikamilifu cha haki.​—Mambo ya Walawi 19:18; Waroma 12:19.

 “Endeleeni kuwapenda adui zenu na kuwatendea mema wale wanaowachukia, kuwabariki wale wanaowalaani, na kusali kwa ajili ya wale wanaowatukana.”​—Luka 6:27, 28.

  •   Uwe mwenye “subira na fadhili.” (1 Wakorintho 13:4) Katika ufafanuzi wake unaofahamika sana kuhusu upendo, mtume Paulo alitumia aina fulani ya neno hilo la Kigiriki (a·gaʹpe) ambalo tunapata katika maneno ya Mathayo 5:44 na Luka 6:27, 35. Tunaonyesha upendo kama huo wa Kikristo hata kuelekea adui zetu tunapowaonyesha subira na fadhili, bila kuwa na wivu, kiburi, au ukaidi.

 Upendo ni wenye subira na fadhili. Upendo hauna wivu. Haujigambi, haujivuni, haujiendeshi bila adabu, hautafuti faida zake wenyewe, hauchokozeki. Hauweki hesabu ya ubaya. Haushangilii ukosefu wa uadilifu, bali hushangilia pamoja na kweli. Huhimili mambo yote, huamini mambo yote, hutumaini mambo yote, huvumilia mambo yote. Upendo haushindwi kamwe.”​—1 Wakorintho 13:4-8.

 Je, unapaswa kujihusisha katika vita dhidi ya adui zako?

 Hapana, kwa sababu Yesu aliwafundisha wafuasi wake wasipigane kuhusu maadui wao. Kwa mfano, alipowaonya kuhusu shambulizi dhidi ya Yerusalemu, hakuwaambia wakae na kupigana, badala yake walipaswa kukimbia. (Luka 21:20, 21) Yesu pia alimwambia mtume Petro: “Rudisha upanga wako mahali pake, kwa maana wote wanaochukua upanga wataangamia kwa upanga.” (Mathayo 26:52) Historia ya Biblia na ya wanahistoria wa ulimwengu inaonyesha kwamba wafuasi wa Yesu katika karne ya kwanza hawakwenda vitani kupigana dhidi ya adui zao. a2 Timotheo 2:24.

 Maoni yasiyo sahihi kuhusu kuwapenda adui zako

 Maoni yasiyo sahihi: Sheria ya Mungu ilitaka Waisraeli wawachukie adui zao.

 Ukweli: Sheria haikuwa na amri kama hiyo. Badala yake iliwaagiza Waisraeli kuwapenda jirani zao. (Mambo ya Walawi 19:18) Ingawa neno “jirani” lilimaanisha wanadamu wengine, baadhi ya Wayahudi walipunguza upana wa maana hiyo ili kumaanisha Wayahudi tu, na waliamini kwamba watu wasio Wayahudi walikuwa maadui waliopaswa kuchukiwa. (Mathayo 5:43, 44) Yesu alisahihisha maoni hayo yenye kasoro kwa kusimulia mfano wa Msamaria mwema, au mwenye ujirani.​—Luka 10:29-37.

 Maoni yasiyo sahihi: Kuwapenda adui zako kunamaanisha kukubali mwenendo wao usiofaa.

 Ukweli: Biblia inaonyesha kwamba unaweza kumpenda mtu bila kukubaliana na mwenendo wake usiofaa. Kwa mfano, Yesu alishutumu jeuri lakini alisali kwa ajili ya wale waliomuua. (Luka 23:34) Na alichukia uasi-sheria, au dhambi, lakini akatoa uhai wake kwa ajili ya watenda-dhambi.​—Yohana 3:16; Waroma 6:23.

a Kitabu The Rise of Christianity cha E. W. Barnes kinasema hivi: “Uchunguzi wa makini wa habari yote inayopatikana unaonyesha kwamba hadi wakati wa Marcus Aurelius [maliki wa Roma kuanzia 161 W.K. hadi 180 W.K.], hakuna Mkristo aliyekuwa mwanajeshi; na hakuna mwanajeshi, baada ya kuwa Mkristo, aliyeendelea na utumishi wa kijeshi.”