Hamia kwenye habari

Biblia Inasema Nini Kuhusu Kulipiza Kisasi?

Biblia Inasema Nini Kuhusu Kulipiza Kisasi?

Jibu la Biblia 

 Hata ingawa mtu anaweza kuhisi kuwa ana haki ya kulipiza kisasi, kufanya hivyo ni kinyume na ushauri wa Biblia: “Usiseme: ‘Nitamtendea kama tu alivyonitendea; nitamlipiza kwa sababu ya mambo aliyonitendea.’” (Methali 24:29) Biblia ina ushauri ambao umewasaidia wengi kushinda tamaa ya kulipiza kisasi. 

Katika makala hii 

 Kuna ubaya gani kulipiza kisasi? 

 Mtu akikukosea au kukuumiza, ni jambo la kawaida kukasirika na kutaka mtu yule mwingine aadhibiwe kwa sababu ya alichofanya. Hata hivyo, kujilipizia kisasi hakupatani na ujumbe wa Biblia. Kwa nini? 

 Mungu hafurahi wanadamu wanapojilipizia kisasi. Katika Biblia, Yehova a Mungu anasema hivi: “Kisasi ni changu; mimi nitalipa.” (Waroma 12:19) Biblia inawatia moyo wale ambao wamekosewa kutafuta njia zenye amani kutatua hali inapowezekana badala ya kulipiza kisasi. (Waroma 12:18) Lakini vipi ikiwa mtu amejaribu njia zote kutatua jambo kwa njia ya amani au vipi ikiwa hakuna njia yenye amani ya kutatua tatizo? Maandiko yanatuhimiza tutumaini kwamba Yehova atashughulikia ukosefu wote wa haki.—Zaburi 42:10, 11

 Mungu hutoa adhabu kwa njia gani? 

 Kwa sasa, Mungu ameruhusu mamlaka za serikali kuwaadhibu watu wanaotenda mabaya. (Waroma 13:1-4) Wakati utafika ambapo atawaadhibu wote ambao wana hatia ya kutenda kwa ukatili na ataondoa kuteseka milele.—Isaya 11:4

 Ninaweza kushindaje tamaa ya kulipiza kisasi? 

  •    Usitende bila kufikiri. (Methali 17:27) Mara nyingi watu wanaofanya mambo wakiwa wamekasirika hujuta baadaye. Lakini wale wanaochukua muda kufikiri kabla ya kutenda hufanya maamuzi mazuri zaidi.—Methali 29:11

  •    Chunguza ukweli wa mambo. (Methali 18:13) Mtu ambaye amekosewa anapaswa kujiuliza hivi, ‘Je, kuna mambo ambayo sijui yanayoweza kunisaidia kuelewa kwa nini mtu huyu alinikosea kwa njia hii? Je, alikuwa chini ya mkazo fulani? Au ametenda bila kujua?’ Nyakati nyingine huenda tukafikiri mtu alitaka kutukosea kimakusudi lakini ukweli ni kwamba alikosea bila kukusudia. 

 Maoni yasiyo sahihi kuhusu kulipiza kisasi 

 Maoni yasiyo sahihi: Biblia inaunga mkono kulipiza kisasi inaposema “jicho kwa jicho.”—Mambo ya Walawi 24:20

 Ukweli: Sheria ya “jicho kwa jicho” katika Israeli la kale ilikusudiwa kuwazuia watu kulipiza kisasi. Kwa ujumla, sheria hiyo iliwasaidia mahakimu kutoa adhabu inayofaa. bKumbukumbu la Torati 19:15-21

 Maoni yasiyo sahihi: Kwa kuwa Biblia haiungi mkono watu kulipiza kisasi, hatuwezi kujilinda tunaposhambuliwa. 

 Ukweli: Mtu anaposhambuliwa ana haki ya kujilinda au kutafuta msaada kutoka kwa wenye mamlaka. Hata hivyo, Biblia inasema tunapaswa kuepuka ugomvi kadiri tuwezavyo.—Methali 17:14

a Yehova ni jina la Mungu kama linavyoonyeshwa katika Biblia. 

b Kwa habari zaidi kuhusu sheria hii, ona makala yenye kichwa “Ni Nini Maana ya ‘Jicho kwa Jicho’?”