Hamia kwenye habari

“Mwamini Yesu”​—Je, Kumwamini Yesu Kunatosha Kupata Wokovu?

“Mwamini Yesu”​—Je, Kumwamini Yesu Kunatosha Kupata Wokovu?

Jibu la Biblia

 Wakristo wanaamini kwamba Yesu alikufa kwa ajili ya dhambi za wanadamu. (1 Petro 3:18) Hata hivyo, ili kupata wokovu unahitaji kufanya mengi zaidi ya kumwamini Yesu kuwa Mwokozi. Roho waovu wanajua kwamba Yesu ni “Mwana wa Mungu,” lakini hawatapata wokovu bali wataharibiwa.—Luka 4:41; Yuda 6.

 Nifanye nini ili niokolewe?

  •   Unapaswa kuamini kwamba Yesu alidhabihu uhai wake kwa ajili ya dhambi zetu. (Matendo 16:30, 31; 1 Yohana 2:2) Hilo linamaanisha kuamini kwamba Yesu alikuwa mtu halisi na kwamba mambo yote ambayo simulizi la Biblia linasema kumhusu ni sahihi.

  •   Jifunze kile ambacho Biblia inafundisha hasa. (2 Timotheo 3:15) Biblia inasema kwamba mtume Paulo na Sila walimwambia hivi mlinzi wa jela: “Mwamini Bwana Yesu, nawe utaokolewa, wewe na watu wa nyumba yako.” Kisha, baada ya hapo, walianza kumfundisha mlinzi huyo wa jela “neno la Yehova.” a (Matendo 16:31, 32) Hilo linaonyesha kwamba mlinzi huyo wa jela hangeweza kumwamini Yesu bila kuwa na ujuzi wa msingi wa Neno la Mungu. Alihitaji kuwa na ujuzi sahihi wa Maandiko.—1 Timotheo 2:3, 4.

  •   Tubu. (Matendo 3:19) Pia, lazima utubu, au uhuzunishwe sana, kuhusu mwenendo na mtazamo mbaya uliokuwa nao. Wengine wataona toba yako kadiri unavyoacha mazoea yanayomchukiza Mungu na unapofanya “matendo yanayoonyesha toba.”—Matendo 26:20.

  •   Ubatizo. (Mathayo 28:19) Yesu alisema kwamba wale ambao watakuwa wanafunzi wake wanapaswa kubatizwa. Mlinzi wa jela aliyetajwa hapo awali alibatizwa. (Matendo 16:33) Vivyo hivyo, baada ya mtume Petro kufundisha umati mkubwa ukweli kumhusu Yesu, “wale waliokubali neno lake kwa furaha wakabatizwa.”—Matendo 2:40, 41.

  •   Tii maagizo ya Yesu. (Waebrania 5:9) Wale ambao ‘wanashika mambo yote’ ambayo Yesu aliamuru wanaonyesha kupitia maisha yao kwamba wao ni wafuasi wake. (Mathayo 28:20) Wanakuwa “watendaji wa neno, na si wasikiaji tu.”—Yakobo 1:22.

  •   Vumilia mpaka mwisho. (Marko 13:13) Wanafunzi wa Yesu ‘wanahitaji uvumilivu’ ili waokolewe. (Waebrania 10:36) Kwa mfano, mtume Paulo aliendelea kutii mafundisho ya Yesu na kuwa mshikamanifu kwa Mungu, na alivumilia tangu alipokuwa Mkristo hadi alipokufa.—1 Wakorintho 9:27.

 Vipi kuhusu “Sala ya Mwenye Dhambi”?

 Katika dini fulani watu hutoa sala fulani kama vile “Sala ya Mwenye Dhambi” na “Sala ya Wokovu.” Wale wanaotoa sala hizo wanakubali kwamba wao ni wenye dhambi na wanaonyesha kwamba wanaamini kwamba Yesu alikufa kwa ajili ya dhambi zao. Pia wanamwomba Yesu aingie katika mioyo au maisha yao. Lakini Biblia haitaji wala haipendekezi kukariri sala kama “Sala ya Mwenye Dhambi.”

 Baadhi ya watu wanafikiri kwamba wanapotoa “Sala ya Mwenye Dhambi,” wamehakikishiwa wokovu wa milele. Lakini hakuna sala yoyote inayoweza kumhakikishia mtu kupata wokovu. Tukiwa wanadamu wasio wakamilifu, tunaendelea kufanya makosa. (1 Yohana 1:8) Ndiyo sababu Yesu aliwafundisha wafuasi wake wasali kwa ukawaida ili wasamehewe dhambi. (Luka 11:2, 4) Isitoshe, baadhi ya Wakristo ambao walikuwa na tumaini la kupata wokovu wa milele walipoteza tumaini hilo kwa sababu walianguka au kugeuka kutoka kwa Mungu.—Waebrania 6:4-6; 2 Petro 2:20, 21.

 “Sala ya Mwenye Dhambi” ilitoka wapi?

 Wanahistoria hawakubaliani kuhusu chanzo cha “Sala ya Mwenye Dhambi.” Baadhi yao husema kwamba desturi hiyo ilianza katika kile kipindi cha Marekebisho Makubwa ya Kiprotestanti. Wengine wanaamini kwamba watu walianza kutoa “Sala ya Mwenye Dhambi” wakati wa yale mapinduzi ya kidini katika karne ya 18 na 19. Vyovyote vile, desturi hiyo haipatani na Maandiko—badala yake inapingana na mafundisho ya Biblia.

a Yehova ni jina la Mungu kama linavyopatikana katika Biblia.