Hamia kwenye habari

Je, Maria Ni Mama ya Mungu?

Je, Maria Ni Mama ya Mungu?

Jibu la Biblia

 La, Biblia haifundishi kwamba Maria ni mama ya Mungu, wala hakuna mahali inapodokeza kwamba Wakristo wanapaswa kumwabudu Maria au kumpa heshima kupita kiasi. a Fikiria hili:

  •   Maria hakudai wakati wowote kwamba alikuwa mama ya Mungu. Biblia inaeleza kwamba alimzaa “Mwana wa Mungu,” si Mungu.​—Marko 1:1; Luka 1:32.

  •   Yesu Kristo hakusema kamwe kwamba Maria alikuwa mama ya Mungu au kwamba alipaswa kupewa heshima ya pekee. Yesu hata alimkosoa mwanamke ambaye alimpa Maria heshima ya pekee ya kuwa mama yake, akisema: “Hapana, badala yake, wenye furaha ni wale wanaolisikia neno la Mungu na kulishika!”​—Luka 11:27, 28.

  •   Maneno “Mama ya Mungu” na “Theotokos” (mzaa-Mungu) hayapatikani popote katika Biblia.

  •   Maneno “Malkia wa Mbinguni” yaliyo katika Biblia, hayarejelei Maria, bali yanarejelea mungu wa kike wa uwongo aliyeabudiwa na Waisraeli walioasi imani. (Yeremia 44:15-19) Huenda “Malkia wa Mbinguni” alikuwa Ishtari (Astarte), mungu wa kike wa Babiloni.

  •   Wakristo wa mapema hawakumwabudu Maria, wala hawakumtukuza kwa njia yoyote ya pekee. Mwanahistoria mmoja anasema kwamba Wakristo wa mapema “walipinga madhehebu na huenda waliogopa kwamba kumpa Maria uangalifu usiohitajika kungetokeza wazo la kwamba wanaabudu mungu wa kike.”​—In Quest of the Jewish Mary.

  •   Biblia inasema kwamba Mungu amekuwepo sikuzote. (Zaburi 90:1, 2; Isaya 40:28) Kwa kuwa hakuwa na mwanzo, hawezi kuwa na mama. Isitoshe, Maria hangeweza kumbeba Mungu katika tumbo lake la uzazi; Biblia inaonyesha wazi kwamba mbingu haziwezi kumtosha Mungu.​—1 Wafalme 8:​27.

Maria Alikuwa Mama ya Yesu Si “Mama ya Mungu”

 Maria alizaliwa katika taifa la Wayahudi, na alikuwa mzao wa ukoo wa Mfalme Daudi. (Luka 3:23-31) Alipendwa sana na Mungu kwa sababu ya imani na ujitoaji wake. (Luka 1:28) Mungu alimchagua awe mama ya Yesu. (Luka 1:31, 35) Maria alizaa watoto wengine ambao walikuwa wa Yosefu, mume wake.​—Marko 6:3.

 Ingawa Biblia inaonyesha kwamba Maria alikuja kuwa mwanafunzi wa Yesu, hakuna habari nyingi za ziada zinazotolewa kumhusu.​—Matendo 1:14.

a Dini kadhaa zinafundisha kwamba Maria ndiye mama ya Mungu. Huenda wakamwita “Malkia wa Mbinguni” au Theotokos, neno la Kigiriki linalomaanisha “mzaa-Mungu.”