Hamia kwenye habari

Je, Yesu Alikuwa na Mke? Je, Alikuwa na Ndugu na Dada?

Je, Yesu Alikuwa na Mke? Je, Alikuwa na Ndugu na Dada?

Jibu la Biblia

 Biblia inaonyesha wazi kwamba Yesu hakuwahi kufunga ndoa, ingawa haisemi kuhusu jambo hilo moja kwa moja. a Fikiria mambo yafuatayo.

  1.   TMara nyingi Biblia hutaja kuhusu familia ya Yesu na vilevile wanawake walioandamana naye alipokuwa akihubiri na ambao walisimama kando yake alipokuwa akiuawa, hata hivyo haisemi kwamba alikuwa na mke. (Mathayo 12:46, 47; Marko 3:​31, 32; 15:40; Luka 8:​2, 3, 19, 20; Yohana 19:25) Sababu ya msingi kwa nini Biblia haisemi lolote kuhusu jambo hilo ni kwa sababu hakuwahi kufunga ndoa.

  2.   Akizungumza kuhusu wale wanaobaki waseja kwa sababu wanataka kufanya mengi zaidi katika utumishi wa Mungu, Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake: ‘Yule anayeweza kuupa useja nafasi na aupe nafasi.’ (Mathayo 19:10-​12) Aliwawekea mfano wale wanaochagua kutofunga ndoa ili wajitoe kikamili zaidi kwa Mungu.​—Yohana 13:15; 1 Wakorintho 7:​32-​38.

  3.   Kabla tu ya kifo chake, Yesu alifanya mipango ya jinsi ambavyo mama yake angetunzwa. (Yohana 19:25-​27) Ikiwa Yesu angekuwa ameoa au kupata watoto, bila shaka angehakikisha kwamba familia yake inatunzwa vizuri pia.

  4.   Ingawa Biblia humrejezea Yesu kuwa kielelezo kwa waume, haizungumzii kamwe kuhusu alivyomtendea mke wake. Badala yake, inasema hivi: “Enyi waume, endeleeni kuwapenda wake zenu, kama vile Kristo pia alivyolipenda kutaniko na kujitoa mwenyewe kwa ajili yake.” (Waefeso 5:​25) Ikiwa kwa kweli Yesu alikuwa ameoa alipokuwa duniani, bila shaka kielelezo chake kikamilifu akiwa mume ndicho kingetajwa moja kwa moja katika mstari huo.

Je, Yesu alikuwa na ndugu na dada?

 Ndiyo, Yesu alikuwa na ndugu na dada sita. Ndugu hao walikuwa Yakobo, Yosefu, Simoni, na Yuda na pia dada wawili. (Mathayo 13:54-​56; Marko 6:3) Ndugu na dada hao walikuwa watoto halisi wa Maria mama ya Yesu, na mume wake Yosefu. (Mathayo 1:​25) Biblia humwita Yesu “mzaliwa wa kwanza” wa Maria, jambo linalodokeza kwamba Maria alikuwa na watoto wengine.​—Luka 2:7.

Maoni yasiyo sahihi kuhusu ndugu za Yesu

 Ili kuendeleza wazo la kwamba Maria alikuwa bikira maisha yake yote, wengine wamelifafanua neno “ndugu” katika njia tofauti tofauti. Kwa mfano, watu fulani wanahisi kwamba ndugu za Yesu walikuwa wana ambao Yosefu alipata katika ndoa yake ya kwanza. Hata hivyo, Biblia inaonyesha kwamba Yesu alirithi haki ya kisheria ya kuwa mtawala wa Ufalme ambao Daudi alikuwa ameahidiwa. (2 Samweli 7:​12, 13; Luka 1:​32) Ikiwa Yosefu alikuwa na wana wakubwa zaidi ya Yesu, bila shaka mwana wake mkubwa ndiye ambaye angekuwa na haki ya kumrithi na wala si Yesu.

 Je, huenda neno “ndugu” lilirejezea wanafunzi wa Yesu, au ndugu zake wa kiroho? Wazo hilo linapingana na Maandiko, kwa kuwa Biblia inasema kwamba wakati fulani “kwa kweli, ndugu zake walikuwa hawamwamini.” (Yohana 7:5) Biblia hutofautisha kati ya ndugu za Yesu na wanafunzi wake.​—Yohana 2:​12.

 Watu wengine wanasema kwamba ndugu za Yesu walikuwa binamu zake. Hata hivyo, Maandiko ya Kigiriki yanatumia maneno hususa yanapozungumza kuhusu “ndugu,” “jamaa,” na “binamu.” (Luka 21:16; Wakolosai 4:​10) Wasomi wengi wa Biblia wanakubali kwamba Yesu alikuwa na ndugu na dada halisi. Kwa mfano, kitabu The Expositor’s Bible Commentary kinasema hivi: “Njia ya kawaida kabisa ya kuelewa neno ‘ndugu’ . . . ni kwamba neno hilo linarejelea wana wa Maria na Yosefu na hivyo wao ni ndugu za Yesu waliozaliwa na mama mmoja.” b

a Ni kweli kwamba Biblia humtaja Kristo kuwa bwana-arusi, lakini muktadha unaonyesha kwamba yeye ni bwana-arusi kwa njia ya mfano.​—Yohana 3:​28, 29; 2 Wakorintho 11:2.

b Ona pia kitabu The Gospel According to St. Mark, Toleo la Pili, kilichoandikwa na Vincent Taylor, ukurasa wa 249, na kitabu A Marginal Jew​—Rethinking the Historical Jesus, kilichoandikwa na John P. Meier, Buku la 1, ukurasa wa 331-​332.