Hamia kwenye habari

Ninaweza Kufanyaje Maamuzi Mazuri?

Ninaweza Kufanyaje Maamuzi Mazuri?

Jibu la Biblia

 Biblia inatupa mwongozo bora zaidi kuhusu kufanya maamuzi mazuri. Inaweza kutusaidia ‘kujipatia hekima na uelewaji.’ (Methali 4:5) Katika hali fulani, inatueleza uamuzi unaofaa zaidi. Na katika hali nyingine, inatupa mwongozo ambao unaweza kutusaidia kufanya maamuzi ya hekima.

Katika makala hii

 Madokezo yatakayokusaidia kufanya uamuzi mzuri

  •   Usifanye uamuzi muhimu upesi. Biblia inasema: “Mwerevu hutafakari kila hatua.” (Methali 14:15) Ukifanya uamuzi wako haraka, unaweza kupuuza habari nyingine muhimu. Fikiria kwa uangalifu mambo yote yanayohusika.—1 Wathesalonike 5:21.

  •   Usifanye maamuzi kwa kutegemea hisia zako tu. Biblia inatuonya kwamba si vizuri kuutumaini moyo wetu. (Methali 28:26; Yeremia 17:9) Kwa mfano, ni vigumu kufanya maamuzi mazuri tunapokuwa na hasira, tunaposhuka au kuvunjika moyo, tunapokosa subira, au hata tunapokuwa tumechoka sana.—Methali 24:10; 29:22.

  •   Sali upate hekima. (Yakobo 1:5) Mungu anapendezwa kujibu sala kama hizo. Yeye ni mzazi anayetujali, Baba anayetaka watoto wake waepuke matatizo inapowezekana. “Yehova mwenyewe hutoa hekima; na kinywani mwake hutoka ujuzi na utambuzi.”  a (Methali 2:6) Anatupa hekima hiyo kupitia Neno lake, Biblia.—2 Timotheo 3:16, 17.

  •   Fanya utafiti. Ili kufanya uamuzi mzuri, unahitaji kuwa na habari zinazotegemeka. Biblia inasema hivi: “Mtu mwenye hekima husikiliza na kujifunza zaidi.” (Methali 1:5) Unaweza kupata wapi habari zinazotegemeka na zinazoweza kukusaidia?

     Kwanza, chunguza Biblia inasemaje kuhusu suala hilo. Kwa kuwa Muumba wetu anajua vizuri zaidi kinachotufaa, Neno lake lina ushauri unaotegemeka kuliko ushauri wowote mwingine. (Zaburi 25:12) Nyakati fulani, Biblia inatueleza moja kwa moja uamuzi tunaopaswa kufanya, labda kupitia sheria au amri. (Isaya 48:17, 18) Lakini katika mambo mengine, Biblia haituelezi moja kwa moja uamuzi tunaopaswa kufanya. Badala yake, inatupatia mwongozo kupitia kanuni mbalimbali. Hivyo, tunaweza kufanya uamuzi mzuri, hata ikiwa uamuzi tuliofanya haufanani na wa watu wengine. Ili kupata sehemu za Biblia zinazozungumzia hali hususa, fanya utafiti katika makala au machapisho, kama yanayopatikana katika tovuti hii bila malipo. b

     Kwa maamuzi fulani, itabidi ufanye utafiti katika vyanzo vingine vinavyotegemeka. Kwa mfano, kabla ya kufanya ununuzi—hasa wa kifaa cha bei ghali—utatenda kwa hekima ikiwa utafanya utafiti kuhusu bidhaa hiyo na pia mtengenezaji wake, sera zozote zinazohusika kuhusiana na udhamini kutia ndani unachopaswa kufanya ikiwa kitu hicho kitaharibika au utahitaji kukirudisha. Ni vizuri kuhakikisha kwamba kifaa hicho kinatimiza mahitaji yako.

     Biblia inasema hivi: “Mipango huvunjika watu wasiposhauriana.” (Methali 15:22) Kwa hiyo, kabla ya kufanya uamuzi, shauriana na watu wanaotegemeka. Kwa mfano, utakuwa umetenda kwa hekima ukimwomba daktari ushauri kabla ya kufanya uamuzi fulani unaohusiana na afya yako. (Mathayo 9:12) Nyakati nyingine, unaweza kuzungumza na watu ambao wamewahi kupitia hali kama yako. Kumbuka kwamba, ni wewe—si watu uliowaomba ushauri—utakayefanya uamuzi na kupambana na matokeo ya uamuzi huo.—Wagalatia 6:4, 5.

  •   Elewa mambo yote yanayohusika. Kwa kutegemea habari ulizokusanya, unaweza kutegeneza orodha ya mambo mbalimbali unayoweza kufanya, na pia faida na hasara za kila jambo. Na tafakari matokeo ya uamuzi wako kwa unyoofu. (Kumbukumbu la Torati 32:29) Kwa mfano, uamuzi wako unaweza kukuathirije wewe, familia yako, au wengine? (Methali 22:3; Waroma 14:19) Kutafakari maswali kama hayo, ukiwa na kanuni za Biblia akilini kutakusaidia kufanya uamuzi wa hekima na wenye upendo.

  •   Fanya uamuzi wako. Nyakati nyingine, tunaweza kusita kufanya uamuzi fulani kwa sababu hatuna uhakika. Lakini tusipofanya uamuzi huenda tukakosa fursa ama tukajipata katika hali mbaya. Kwa maneno mengine, kutofanya uamuzi ni sawasawa na kufanya uamuzi mbaya. Biblia inatusaidia kuelewa jambo hilo kwa kulilinganisha na ukulima inaposema hivi: “Anayengoja upepo hatapanda mbegu, anayesubiri mawingu yatoweke, hatavuna kitu.”—Mhubiri 11:4. Biblia Habari Njema.

 Kumbuka kwamba hata uamuzi bora zaidi si mkamilifu. Mara nyingi, tunapochagua kitu kimoja, huenda tunahitaji kudhabihu kingine. Pia, matukio yasiotarajiwa yanaweza kutokea. (Mhubiri 9:11) Kwa hiyo, tumia vizuri habari bora zaidi unazoweza kupata, na uchague jambo ambalo kuna uwezekano mkubwa zaidi wa kufaulu.

 Je, nibadili uamuzi ambao nilikuwa nimefanya?

 Tunaweza kubadili maamuzi fulani tuliyofanya. Hali yako inaweza kubadilika au ukaona kwamba uamuzi uliofanya awali ulikuwa na matokeo ambayo hukutarajia. Kwa hiyo, inaweza kuwa jambo la busara kufikiria hali tena na kufanya uamuzi mwingine ili kutimiza malengo yako.

 Lakini maamuzi fulani hayapaswi kubadilishwa. (Zaburi 15:4) Kwa mfano, Mungu anatarajia wenzi wa ndoa kuweka nadhiri zao za ndoa. c (Malaki 2:16; Mathayo 19:6) Matatizo yanapotokea katika ndoa, wenzi wa ndoa wanapaswa kujitahidi kuyatatua na si kuvunja ndoa yao.

 Itakuaje ikiwa nilifanya uamuzi mbaya ambao siwezi kubadili?

 Kila mtu hufanya maamuzi mabaya wakati fulani. (Yakobo 3:2, maelezo ya chini) Tunaweza hata kujuta au kuhisi hatia, jambo ambalo ni la kawaida. (Zaburi 69:5) Kwa kweli, kuwa na hisia hizo kunaweza kuwa jambo zuri ikiwa kutatuzuia kurudia makosa tena! (Methali 14:9) Hata hivyo, Biblia inatuonya dhidi ya kuhisi hatia kupita kiasi kwa sababu tunaweza kuvunjika moyo sana na kushindwa kufanya maamuzi mazuri. (2 Wakorintho 2:7) d Biblia inasema hivi: “Yehova ni mwenye rehema na mwenye huruma.” (Zaburi 103:8-13) Kwa hiyo, jaribu kujifunza kutokana na uamuzi mbaya ambao huwezi kubadili na ufanye yote uwezayo ili kuboresha mambo.

a Yehova ni jina la Mungu kama linavyofunuliwa katika Biblia.—Zaburi 83:18.

b Pia, unaweza kufanya utafiti katika tovuti ya jw.org kwa kuandika neno au maneno kadhaa katika sehemu ya tafuta yanayohusiana na uamuzi unaotaka kufanya. Tovuti hiyo ina ushauri mwingi wa Kimaandiko kuhusu mambo mbalimbali. Zaidi ya hilo, unaweza kutafuta maneno hususa katika “Fahirisi ya Maneno ya Biblia” ya Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

c Mapenzi ya Mungu ni kwamba wenzi wa ndoa waishi pamoja muda wote wa maisha yao. Anaruhusu watalikiane na kuweza kuoa au kuolewa tena ikiwa mmoja wao amefanya uasherati. (Mathayo 19:9) Ikiwa unakabili matatizo katika ndoa yako, Biblia inaweza kukusaidia kuyatatua kwa njia ya upendo na yenye hekima.

d Ili kupata habari zaidi, ona makala yenye kichwa “Ninahisi Nina Hatia—Je, Biblia Inaweza Kunisaidia Nijihisi Vizuri?