Hamia kwenye habari

Je, Dunia Itaharibiwa?

Je, Dunia Itaharibiwa?

Jibu la Biblia

 Hapana, Dunia haitawahi kamwe kuharibiwa, kuteketezwa, au kubadilishwa na sayari nyingine. Biblia inafundisha kwamba Mungu aliiumba dunia ili ikaliwe milele.

  •   “Waadilifu wataimiliki dunia, nao wataishi humo milele.”​—Zaburi 37:29.

  •   “[Mungu] ameiimarisha dunia juu ya misingi yake; haitasogezwa kutoka mahali pake milele na milele.”​—Zaburi 104:5.

  •   “Dunia inadumu milele.”​—Mhubiri 1:4.

  •   “Aliyeiumba dunia, Yule aliyeitengeneza na kuifanya imara kabisa, . . . hakuiumba tu bila sababu, lakini aliiumba ili ikaliwe.”​—Isaya 45:18.

Je, wanadamu wataiharibu dunia?

 Mungu hatawaruhusu wanadamu waiharibu kabisa dunia kupitia uchafuzi, vita, au njia nyingine yoyote. Badala yake, ‘atawaharibu wale wanaoiharibu dunia.’ (Ufunuo 11:18) Atafanyaje hivyo?

 Mungu ataondoa serikali za wanadamu, ambazo zimeshindwa kuilinda dunia, na kusimamisha Ufalme wa mbinguni ulio mkamilifu. (Danieli 2:​44; Mathayo 6:​9, 10) Ufalme huo utatawaliwa na Mwana wa Mungu, Yesu Kristo. (Isaya 9:​6, 7) Alipokuwa duniani, Yesu alionyesha nguvu za kufanya miujiza kwa kudhibiti nguvu za asili. (Marko 4:​35-​41) Akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu, Yesu atadhibiti kikamili dunia na nguvu zake za asili. Ataumba upya, au kutokeza hali mpya duniani, na hivyo kutokeza hali kama zile zilizokuwepo katika bustani ya Edeni.​—Mathayo 19:28; Luka 23:43.

Je, Biblia haifundishi kwamba dunia itateketezwa kwa moto?

 Hapana, haifundishi hivyo. Maoni hayo yasiyo sahihi mara nyingi hutokea kwa sababu ya kuelewa vibaya andiko la 2 Petro 3:7, linalosema: “Mbingu na dunia zilizopo sasa zimewekwa akiba kwa ajili ya moto.” Fikiria mambo mawili muhimu yanayotusaidia kuelewa maana ya maneno hayo:

  1.   Biblia hutumia maneno “mbingu,” “dunia,” na “moto” kumaanisha mambo mengi tofauti. Kwa mfano, Mwanzo 11:1 inasema hivi: “Dunia yote iliendelea kuwa na lugha moja.” Katika mstari huo, “dunia” inarejelea jamii ya wanadamu.

  2.   Muktadha wa 2 Petro 3:7 unaonyesha maana ya mbingu, dunia, na moto unaotajwa hapo. Mstari wa 5 na 6 unaonyesha mambo yanayofanana na Gharika ya siku za Noa. Wakati huo, ulimwengu wa kale uliangamizwa, hata hivyo, sayari yetu haikutoweka. Badala yake, Gharika ilifutilia mbali jamii ya wanadamu, au “dunia,” iliyokuwa imejaa ukatili. (Mwanzo 6:​11) Pia, iliharibu aina fulani ya “mbingu”​—watu waliotawala jamii hiyo. Hivyo, watu waovu waliharibiwa, si sayari yetu. Noa na familia yake waliokoka uharibifu wa ulimwengu huo na wakaishi duniani baada ya Gharika.​—Mwanzo 8:​15-​18.

 Kama tu maji hayo ya Gharika, uharibifu, au “moto,” unaotajwa katika 2 Petro 3:7 utaleta mwisho wa wanadamu waovu, si wa sayari Dunia. Mungu anaahidi kutakuwa na “mbingu mpya na dunia mpya, na humo uadilifu utakaa.” (2 Petro 3:​13) “Dunia mpya,” au jamii mpya ya wanadamu, itatawaliwa na “mbingu mpya,” au utawala mpya​—Ufalme wa Mungu. Chini ya utawala wa Ufalme huo, dunia itakuwa paradiso yenye amani.​—Ufunuo 21:​1-4.