Hamia kwenye habari

IGENI IMANI YAO | YONATHANI

“Hakuna Kitu Chochote Kinachoweza Kumzuia Yehova

“Hakuna Kitu Chochote Kinachoweza Kumzuia Yehova

Wazia kituo cha ulinzi kilicho katika eneo la mbali kikitazama eneo kame na lenye miamba. Ghafla askari Wafilisti waliokuwa hapo wanajionea kitu kinachovuta uangalifu wao: Wanaume wawili, Waisraeli, wanasimama mbele yao upande ule mwingine wa bonde. Askari hao wanacheka—hawawaoni kuwa tisho lolote. Kwa muda mrefu Wafilisti wamewakandamiza Waisraeli ambao hawawezi hata kunoa vifaa vya chuma wanavyotumia katika mashamba yao bila kuwaendea maadui wao Wafilisti ili kupata msaada. Kwa sababu hiyo, askari wa Israeli hawana silaha. Isitoshe, hawa ni wanaume wawili tu! Hata ikiwa wangekuwa na silaha, wanaweza kutokeza madhara gani? Kwa dhihaka, Wafilisti wakasema: “Njooni hapa juu tulipo, nasi tutawafunza somo!”​—1 Samweli 13:19-23; 14:11, 12.

Kwa kweli, somo lilikuwepo, lakini Wafilisti hao ndio wangejifunza somo hilo. Waisraeli hao wawili wakakimbia na kuvuka bonde hilo kisha wakaanza kupanda mwamba uliokuwa mbele yao. Ulikuwa mwinuko mkali hivi kwamba walihitaji kutumia mikono na miguu, lakini walizidi kusonga, kupanda, na kuelekea moja kwa moja kwenye kituo hicho! (1 Samweli 14:13) Sasa Wafilisti wangeweza kuona kwamba mwanamume aliyekuwa mbele alikuwa na silaha; alifuatiwa na mtumishi aliyembebea silaha. Lakini je, alikuwa akiongoza shambulizi la watu wawili dhidi ya kikosi kizima? Je, alikuwa amerukwa na akili?

La, akili zake zilikuwa timamu; alikuwa mtu mwenye imani kubwa. Jina lake Yonathani pamoja na hadithi yake inawafundisha Wakristo wa kweli leo masomo mengi sana. Ingawa hatujihusishi katika vita halisi, tunaweza kujifunza mengi kutoka kwa Yonathani kuhusu ujasiri, ushikamanifu, na kutenda bila ubinafsi, sifa ambazo tunahitaji ili kusitawisha imani ya kweli.​—Isaya 2:4; Mathayo 26:51, 52.

Mwana Mshikamanifu na Askari Mwenye Ujasiri

Ili kuelewa sababu iliyomfanya Yonathani ashambulie kituo hicho cha ulinzi, tunahitaji kuchunguza malezi yake. Yonathani alikuwa mwana wa kwanza wa Sauli, mfalme wa kwanza wa Israeli. Sauli alipowekwa rasmi kuwa mfalme, tayari Yonathani alikuwa mwanamume, huenda mwenye umri wa miaka 20 au zaidi. Inaonekana kwamba Yonathani alidumisha uhusiano wa karibu na baba yake, ambaye mara nyingi angemweleza mwana wake mambo ya siri. Katika miaka hiyo ya mapema, Yonathani alijua kwamba mbali na kuwa mwanamume mrefu, mwenye sura nzuri, na shujaa wa vita mwenye ujasiri, baba yake alikuwa na sifa nyingine muhimu zaidi​—alikuwa mwanamume mwenye imani na mnyenyekevu. Yonathani angeweza kuona sababu iliyomfanya Yehova amchague Sauli kuwa mfalme. Hata nabii Samweli alisema kwamba hakukuwa na mtu yeyote mwingine kama Sauli katika nchi yote!—1 Samweli 9:1, 2, 21; 10:20-24; 20:2.

Lazima Yonathani awe aliona ni pendeleo kuwa chini ya uongozi wa baba yake walipopigana dhidi ya maadui wa watu wa Yehova. Vita hivyo havikuwa kama vita vya kizalendo vinavyopiganwa leo. Wakati huo, Yehova alichagua taifa la Israeli kumwakilisha, na lilishambuliwa mara nyingi na mataifa yaliyoabudu miungu ya uwongo. Wafilisti, waliochafuliwa na ibada ya miungu kama vile Dagoni, mara nyingi walijaribu kuwanyanyasa na hata kuwaangamiza watu ambao Yehova alikuwa amewachagua.

Kwa hiyo, kwa wanaume kama vile Yonathani, kupigana kulikuwa utumishi mshikamanifu kwa Yehova Mungu. Na Yehova alibariki jitihada za Yonathani. Punde baada ya Sauli kuwa mfalme, alimweka rasmi mwana wake kusimamia askari 1,000, na Yonathani aliwaongoza kushambulia kambi ya kijeshi ya Wafilisti iliyokuwa Geba. Ingawa wanaume wake hawakuwa na silaha zinazofaa, kwa msaada wa Yehova, Yonathani alishinda. Hata hivyo, Wafilisti walikusanya jeshi kubwa ili kulipiza kisasi. Askari wengi wa Sauli waliogopa sana. Wengine walitoroka na kujificha, na wachache hata walivuka na kujiunga na Wafilisti! Lakini Yonathani alidumisha ujasiri wake.​—1 Samweli 13:​2-7; 14:21.

Kama ilivyosimuliwa kwenye utangulizi, siku moja Yonathani aliamua kuondoka akiwa tu na mtumishi aliyembebea silaha. Walipokaribia kituo cha ulinzi cha Wafilisti kilichokuwa Mikmashi, Yonathani alimfunulia mtumishi wake aliyembebea silaha mbinu yake. Wangetokea ili waonekane na askari Wafilisti. Iwapo Wafilisti wangewajaribu kwa kuwaambia wapande na kuwashambulia, hiyo ingekuwa ishara kwamba Yehova atawasaidia watumishi wake. Mtumishi aliyembebea silaha alikubali upesi, labda kwa sababu alichochewa na maneno haya ya Yonathani yenye nguvu: “Hakuna kitu chochote kinachoweza kumzuia Yehova kuokoa kwa kutumia watu wengi au wachache.” (1 Samweli 14:6-10) Alimaanisha nini?

Ni wazi kwamba Yonathani alimfahamu Mungu vizuri. Bila shaka alijua kwamba zamani, Yehova alikuwa amewasaidia watu wake kuwaangamiza maadui waliowazidi sana. Nyakati nyingine, Yehova alikuwa ametumia mtu mmoja tu kuleta ushindi. (Waamuzi 3:31; 4:1-23; 16:23-30) Kwa hiyo, Yonathani alijua jambo muhimu halikuwa idadi, nguvu, au silaha za watumishi wa Mungu; jambo muhimu lilikuwa imani yao. Basi, kwa imani Yonathani alimruhusu Yehova aamue ikiwa yeye na mtumishi wake aliyembebea silaha wanapaswa kushambulia kituo hicho cha ulinzi; alichagua ishara ambayo Yehova angetumia kumwonyesha kuwa anakubaliana na mbinu yake. Kibali kilipotolewa, Yonathani alisonga mbele bila woga.

Ona mambo mawili yanayoonyesha imani ya Yonathani. Kwanza, alimwogopa sana Mungu wake, Yehova. Alijua kwamba Mungu Mweza-Yote hategemei nguvu za mwanadamu ili kutimiza makusudi yake, lakini Yehova anafurahi kuwabariki wanadamu waaminifu wanaomtumikia. (2 Mambo ya Nyakati 16:9) Pili, kabla ya kutenda Yonathani alitafuta uthibitisho wa kibali cha Yehova. Leo, hatutafuti ishara za kimuujiza kutoka kwa Mungu wetu ili kuthibitisha ikiwa anakubaliana na jambo tunalotaka kufanya. Kwa kuwa tayari tuna Neno la Mungu lililoongozwa na roho, tuna kila kitu tunachohitaji ili kutambua mapenzi ya Mungu. (2 Timotheo 3:16, 17) Je, tunachunguza Biblia kwa makini kabla ya kufanya maamuzi muhimu? Ikiwa ndivyo, basi tunaonyesha kwamba tunajali mapenzi ya Mungu zaidi ya mapenzi yetu​—kama Yonathani alivyofanya.

Kwa hiyo, wanaume hao wawili, shujaa na mtumishi wake aliyembebea silaha, wakapanda mwinuko huo mkali kwenda kwenye kituo hicho cha ulinzi. Wafilisti, walipotambua kwamba wanashambuliwa, waliwatuma watu wakawashambulie wavamizi hao wawili. Kwa kuwa Wafilisti walikuwa wengi na pia walikuwa upande wa juu wa mwinuko huo, wangaliweza kuwamaliza washambuliaji hao wawili kwa urahisi. Lakini Yonathani aliwapiga askari Wafilisti na kuwaangusha chini mmoja baada ya mwingine. Na mtumishi wake aliyembebea silaha alikuwa akiwaua nyuma yake. Katika eneo hilo dogo, wanaume hao wawili waliwaua askari 20 Wafilisti! Kisha Yehova akafanya jambo lingine. Tunasoma hivi: “Ndipo hofu ikaenea katika kambi iliyo shambani na miongoni mwa watu wote waliokuwa katika kituo cha ulinzi, na hata makundi ya wavamizi yakashikwa na hofu. Dunia ikaanza kutetemeka, kukawa na hofu kubwa kutoka kwa Mungu.”​—1 Samweli 14:15.

Yonathani aliongoza shambulizi la watu wawili dhidi ya kituo kizima cha maadui walio na silaha

Kwa mbali, Sauli na wanaume wake waliona machafuko na hofu ikienea kati ya Wafilisti, ambao walianza kushambuliana wenyewe kwa wenyewe! (1 Samweli 14:16, 20) Waisraeli wakajipa ujasiri na kushambulia, labda wakichukua silaha kutoka kwa Wafilisti waliokuwa wamekufa. Siku hiyo Yehova aliwapa watu wake ushindi mkubwa. Naye hajabadilika tangu nyakati hizo zenye kusisimua. Ikiwa leo tutamwamini, kama Yonathani na mtumishi aliyembebea silaha, hatutawahi kukata tamaa.​—Malaki 3:6; Waroma 10:11.

“Alitenda Pamoja na Mungu”

Kwa Sauli, ushindi huo haukuwa na matokeo mazuri kwake kama ilivyokuwa kwa Yonathani. Sauli alikuwa amefanya makosa makubwa. Alikosa kumtii nabii Samweli aliyewekwa rasmi na Yehova kwa kutoa dhabihu ambayo nabii huyo, aliyekuwa Mlawi, ndiye aliyepaswa kuitoa. Samweli alipowasili, alimwambia Sauli kwamba kwa sababu ya kutotii kwake, ufalme wake hautadumu. Kisha, Sauli alipowatuma wanaume wake vitani, bila kufikiri aliwaapisha hivi kabla ya kuondoka: “Alaaniwe mtu yeyote atakayekula chakula chochote kabla ya jioni na kabla sijalipiza kisasi dhidi ya maadui wangu!”​—1 Samweli 13:10-14; 14:24.

Maneno ya Sauli yanamwonyesha kuwa mwanamume aliyebadilika sana. Je, mwanamume mnyenyekevu na mwenye hali nzuri ya kiroho alikuwa akibadilika kuwa mwenye kiburi na kujitakia makuu? Yehova hakuwahi kuelekeza kwamba askari hao jasiri na wenye bidii wawekewe sheria kama hiyo isiyo na usawaziko. Namna gani kuhusu maneno haya ya Sauli, “kabla sijalipiza kisasi dhidi ya maadui wangu? Je, yanaonyesha kwamba Sauli alifikiri vita hivyo vilikuwa vyake? Je, alikuwa amesahau kwamba haki ya Yehova ndiyo iliyokuwa jambo kuu na si tamaa ya Sauli ya kulipiza kisasi, kujipatia utukufu, au ushindi?

Yonathani hakujua lolote kuhusu kiapo hicho cha baba yake kisichofaa. Akiwa amechoka kwa sababu ya vita hivyo vikali, alichovya fimbo yake ndani ya mzinga na kuonja asali; mara moja alipata nguvu tena. Ndipo mtu mmoja akamwambia kwamba baba yake alikuwa amewakataza kula. Yonathani akasema: “Baba yangu ameleta shida kubwa nchini. Angalieni jinsi macho yangu yalivyong’aa nilipoonja asali hii kidogo. Hali ingekuwa bora zaidi ikiwa watu wangekula kwa uhuru leo baadhi ya nyara walizopata kutoka kwa maadui wao! Kwa maana Wafilisti wengi hata zaidi wangeuawa.” (1 Samweli 14:25-30) Alisema kweli. Yonathani alikuwa mwana mshikamanifu, lakini ushikamanifu wake haukumpofusha. Hakukubaliana bila kufikiri na kila kitu ambacho baba yake alisema na kufanya, na maoni hayo yenye usawaziko yalimfanya aheshimiwe na wengine.

Sauli alipogundua kwamba Yonathani alikuwa amekosa kutii kiapo alichoweka, bado alikataa kukubali kwamba amri yake ilikuwa ya kipumbavu. Badala yake, aliamini kwamba mwana wake anapaswa kuuawa! Yonathani hakubisha wala hakuomba aonyeshwe rehema. Hebu ona jibu lake lenye kupendeza. Alisema hivi bila ubinafsi: “Nipo hapa! Niko tayari kufa!” Hata hivyo, Waisraeli wakamtetea wakisema: “Je, Yonathani afe, ambaye ameleta ushindi huu mkubwa katika Israeli? Ni jambo lisiloweza kuwaziwa kamwe! Kwa hakika kama anavyoishi Yehova, hakuna unywele hata mmoja wa kichwa chake unaopaswa kuanguka ardhini, kwa maana alitenda pamoja na Mungu leo.” Matokeo yakawaje? Sauli alisikiliza maneno hayo. Simulizi linasema: “Hivyo watu wakamwokoa Yonathani, naye hakufa.”​—1 Samweli 14:43-45.

“Nipo hapa! Niko tayari kufa!”

Kupitia ujasiri, bidii, na roho ya kujidhabihu, Yonathani alikuwa amejitengenezea sifa. Alipokuwa hatarini, sifa yake ilimtetea. Ni vizuri kwetu pia kufikiria tunajitengenezea jina, au sifa, ya aina gani siku baada ya siku. Biblia inatuambia kwamba jina zuri ni lenye thamani sana. (Mhubiri 7:1) Ikiwa sisi, kama Yonathani, tunajitahidi kujifanyia jina zuri pamoja na Yehova, sifa yetu itakuwa hazina yenye thamani kubwa.

Giza Lililozidi Kuongezeka

Licha ya makosa ya Sauli, Yonathani aliendelea kupigana kwa ushikamanifu kando yake kwa miaka mingi. Tunaweza kuwazia jinsi alivyohuzunika kumwona baba yake akisitawisha roho ya kutotii na yenye kiburi. Wingu lenye giza lilikuwa likijitokeza ndani ya baba yake, na Yonathani hakuwa na uwezo wa kulizuia.

Tatizo liliongezeka Yehova alipompa Sauli mgawo wa kupigana na Waamaleki, watu ambao katika siku za Musa walikuwa wamejihusisha sana katika uovu hivi kwamba Yehova alitabiri kuangamizwa kwa taifa hilo lote. (Kutoka 17:14) Sauli aliambiwa aangamize mifugo yao yote na kumuua mfalme wao, Agagi. Sauli alishinda vita hivyo, na bila shaka kama kawaida Yonathani alipigana kwa ujasiri chini ya uongozi wa baba yake. Lakini Sauli alikosa kutii amri ya Yehova, akamwacha Agagi akiwa hai na kuchukua mali na mifugo. Nabii Samweli akatangaza hukumu ya mwisho ya Yehova dhidi ya Sauli: “Kwa kuwa umelikataa neno la Yehova, yeye pia amekukataa usiwe mfalme.”​—1 Samweli 15:2, 3, 9, 10, 23.

Muda mfupi baada ya hapo, Yehova akaondoa roho yake takatifu kutoka kwa Sauli. Bila uvutano wenye upendo wa Yehova, Sauli alianza kupatwa na hisia zinazobadilika-badilika sana, milipuko ya hasira, na woga mwingi kupita kiasi. Ilikuwa kana kwamba roho mbaya kutoka kwa Mungu ilikuwa imechukua mahali pa roho nzuri. (1 Samweli 16:14; 18:10-12) Lazima Yonathani awe alihuzunika sana kumwona baba yake ambaye wakati fulani alikuwa na sifa nzuri akiwa amebadilika sana. Hata hivyo, Yonathani hakuyumba kamwe na kuacha utumishi wake mshikamanifu kwa Yehova. Alimuunga mkono baba yake kwa kadiri aliyoweza, na hata pindi fulani alizungumza naye waziwazi, lakini sikuzote alimwelekezea fikira Yehova, Mungu wake na Baba yake ambaye habadiliki kamwe.​—1 Samweli 19:4, 5.

Je, umewahi kumtazama mtu unayempenda, labda mtu wa karibu wa familia, akibadilika na kuwa mbaya sana hatua kwa hatua? Jambo hilo linaweza kuleta maumivu mengi sana. Mfano wa Yonathani unatukumbusha maneno ambayo mtunga-zaburi aliandika baadaye: “Hata baba yangu na mama yangu wakiniacha, Yehova mwenyewe atanichukua.” (Zaburi 27:10) Yehova ni mshikamanifu. Atakuchukua pia na kuwa Baba bora zaidi kuliko unavyoweza kuwazia, hata wanadamu wasio wakamilifu wakifanya mambo yanayokuvunja moyo au kukukatisha tamaa.

Huenda Yonathani aligundua kwamba Yehova alikusudia kumnyang’anya Sauli ufalme. Yonathani alitendaje? Je, aliwahi kujiuliza yeye atakuwa mfalme wa aina gani? Je, alitumaini kwamba atarekebisha baadhi ya makosa ya baba yake, na kuweka mfano mzuri wa mfalme mshikamanifu na mtiifu? Hatujui mawazo yake ya ndani yalikuwaje; tunajua tu kwamba mambo hayo hayangetimizwa. Je, hilo linamaanisha kwamba Yehova alimwacha mwanamume huyo mwaminifu? Bila shaka la, badala yake alimtumia Yonathani kuweka mojawapo ya mifano bora zaidi kurekodiwa katika Biblia ya urafiki mshikamanifu! Urafiki huo utazungumziwa katika makala ya wakati ujao kumhusu Yonathani.