Hamia kwenye habari

IGENI IMANI YAO | YONATHANI

“Wakashikamana na Kuwa Marafiki wa Karibu Sana”

“Wakashikamana na Kuwa Marafiki wa Karibu Sana”

Vita vilikuwa vimekwisha, na kimya kikatanda juu ya Bonde la Ela. Upepo wa alasiri ulipokuwa ukipiga mahema kwenye kambi ya jeshi, Mfalme Sauli alikuwa na mkutano pamoja na wanaume wake. Mwana wake wa kwanza, Yonathani, alikuwepo huku kijana mchungaji akisimulia hadithi yake kwa msisimuko. Kijana huyo alikuwa Daudi, na alikuwa amechachawa kwa bidii na msisimuko. Sauli alimsikiliza Daudi kwa makini ili asipitwe na neno hata moja. Hata hivyo, Yonathani alihisije? Alikuwa ameshinda vita vingi katika utumishi wake wa miaka mingi katika jeshi la Yehova. Lakini ushindi wa leo haukuwa wa Yonathani; ulikuwa wa kijana huyu. Daudi alikuwa ameliua lile jitu Goliathi! Je, Yonathani alikuwa na wivu kwa sababu ya sifa nyingi ambazo Daudi alikuwa akipewa?

Huenda ukashangazwa na itikio la Yonathani. Tunasoma hivi: “Baada tu ya Daudi kumaliza kuzungumza na Sauli, Yonathani na Daudi wakashikamana na kuwa marafiki wa karibu sana, na Yonathani akaanza kumpenda kama alivyojipenda mwenyewe.” Yonathani alimpa Daudi mavazi yake ya vita, kutia ndani upinde wake, na kwa kweli hiyo ilikuwa zawadi ya pekee kwa kuwa Yonathani alikuwa na sifa ya kuwa bingwa wa kurusha mishale. Mbali na hilo, Yonathani na Daudi wakafanya agano, mkataba wa pekee, ambao ungewaunganisha na kuwafanya marafiki ambao wangetegemezana.​—1 Samweli 18:1-5.

Huo ndio mwanzo wa mojawapo ya urafiki wa karibu sana unaofafanuliwa katika Biblia. Urafiki ni muhimu kati ya watu wenye imani. Tukichagua marafiki kwa hekima na kuwa rafiki anayetegemeza na mshikamanifu kwa wengine, tunaweza kuimarisha imani yetu katika nyakati hizi zisizo na upendo. (Methali 27:17) Acheni tuone tunaweza kujifunza nini kuhusu urafiki kutoka kwa Yonathani.

Msingi wa Urafiki

Urafiki kama huo unawezaje kusitawi upesi hivyo? Jibu linapatikana tunapochunguza msingi wa urafiki huo. Fikiria mambo machache. Yonathani alikuwa akikabili hali ngumu. Baba yake, Mfalme Sauli, alikuwa akibadilika kadiri miaka ilivyosonga, na utu wake ulizidi kuzorota. Ingawa zamani alikuwa mwanamume mnyenyekevu, mtiifu, na mwenye imani, Sauli alibadilika na kuwa mfalme mkaidi na asiyetii.​—1 Samweli 15:17-​19, 26.

Lazima Yonathani awe alihuzunishwa sana na mabadiliko katika maisha ya Sauli, kwa sababu alikuwa na uhusiano wa karibu na baba yake. (1 Samweli 20:2) Inaelekea kwamba Yonathani alijiuliza Sauli ataleta madhara gani juu ya taifa lililochaguliwa na Yehova. Je, kukosa kutii kwa mfalme kungewafanya raia watende kwa njia isiyofaa na kuwafanya wapoteze kibali cha Yehova? Bila shaka, hizo zilikuwa nyakati ngumu kwa mwanamume mwenye imani kama Yonathani.

Huenda mambo hayo yakatusaidia kuelewa ni nini kilichomfanya Yonathani avutiwe na kijana Daudi. Yonathani aliona imani kubwa ya Daudi. Kumbuka, tofauti na wote katika jeshi la Sauli, Daudi hakumwogopa Goliathi ingawa alikuwa na umbo kubwa sana. Alijiambia kwamba kwenda kupigana akiwa na jina la Yehova kulimfanya awe na nguvu zaidi kuliko Goliathi na silaha zake zote.​—1 Samweli 17:45-​47.

Miaka kadhaa mapema, Yonathani alikuwa amesema maneno kama hayo. Alikuwa na uhakika kwamba wanaume wawili, yaani, yeye na mtumishi wake aliyembebea silaha, wangeweza kushambulia na kushinda kikosi kizima cha askari wenye silaha. Kwa nini? Yonathani alisema: “Hakuna kitu chochote kinachoweza kumzuia Yehova.” (1 Samweli 14:6) Kwa hiyo, Yonathani na Daudi walifanana kwa njia nyingi: walikuwa na imani yenye nguvu katika Yehova na walimpenda sana. Huo ulikuwa msingi unaofaa kabisa kwa wanaume hao kuanzisha na kudumisha urafiki. Hata ingawa Yonathani alikuwa mwana mwenye nguvu wa mfalme, na alikuwa anakaribia umri wa miaka 50, huku Daudi akiwa mchungaji wa hali ya chini ambaye hata hajatimia miaka 20, tofauti hizo hazikuwa muhimu kwao. *

Agano walilofanya lililinda urafiki wao sana. Jinsi gani? Fikiria kwamba Daudi alijua Yehova alitaka awe mfalme anayefuata wa Israeli! Je, alimficha Yonathani habari hiyo? Hapana! Urafiki mzuri unasitawi na kudumishwa kupitia mawasiliano ya wazi, si kupitia siri na uwongo. Kufahamu kwamba Daudi ndiye atakayekuwa mfalme kungeweza kumwathirije Yonathani? Vipi ikiwa Yonathani alikuwa anatamani kuwa mfalme siku moja ili asahihishe makosa ambayo baba yake alifanya? Biblia haituelezi kwamba Yonathani alikuwa na hisia zisizofaa moyoni; inatuambia tu kuhusu kile kilichokuwa muhimu, yaani, ushikamanifu na imani ya Yonathani. Aliona wazi kwamba roho ya Yehova ilikuwa ikitenda juu ya Daudi. (1 Samweli 16:​1, 11-​13) Kwa hiyo, Yonathani alitimiza kiapo chake na akaendelea kumwona Daudi, si kama mpinzani wake, bali kama rafiki. Yonathani alitaka kuona mapenzi ya Yehova yakitendeka.

Yonathani na Daudi walikuwa na imani yenye nguvu katika Yehova na walimpenda sana

Urafiki huo ulikuwa baraka kubwa. Tunaweza kujifunza nini kutoka kwa imani ya Yonathani? Mtumishi yeyote wa Mungu anapaswa kutambua thamani ya urafiki. Si lazima marafiki wetu wawe na umri au malezi kama yetu, lakini wanaweza kutusaidia sana ikiwa wana imani ya kweli. Yonathani na Daudi walifaulu kuimarishana na kutiana moyo mara nyingi. Na wote wangehitaji msaada kama huo, kwa kuwa urafiki wao ungekabili majaribu makubwa zaidi.

Changamoto ya Kuamua Utakuwa Mshikamanifu kwa Nani

Mwanzoni, Sauli alimpenda sana Daudi na kumweka asimamie jeshi lake. Hata hivyo, baada ya muda mfupi, Sauli alishindwa na adui ambaye Yonathani alikuwa amemshinda​—wivu. Daudi alishinda vita moja baada ya nyingine dhidi ya Wafilisti waliokuwa maadui wa Waisraeli. Kwa sababu hiyo, Daudi alisifiwa na kuheshimiwa. Hata wanawake fulani wa Israeli waliimba hivi: “Sauli ameua maelfu yake, na Daudi makumi yake ya maelfu.” Wimbo huo ulimchukiza Sauli. Tunasoma hivi: “Kuanzia siku hiyo na kuendelea, Sauli alikuwa akimtilia shaka Daudi.” (1 Samweli 18:7, 9) Aliogopa kwamba Daudi angejaribu kujinyakulia ufalme. Huo ulikuwa upumbavu kwa upande wa Sauli. Ni kweli kwamba Daudi alijua angekuwa mfalme baada ya Sauli, lakini hakuna wakati ambapo hata alifikiria kumng’oa mfalme mtiwa-mafuta wa Yehova kutoka kwenye kiti chake!

Sauli akapanga njama za kumfanya Daudi afe vitani, lakini hakuna kitu kilichofaulu. Daudi aliendelea kushinda vita na watu walizidi kumpenda na kumheshimu. Sauli akajaribu kuifanya familia yake kwa pamoja​—watumishi wake wote pamoja na mwana wake wa kwanza​—wajiunge katika njama ya kumuua Daudi! Wazia jinsi Yonathani alivyochukizwa kumwona baba yake akitenda kwa njia hiyo! (1 Samweli 18:25-​30; 19:1) Yonathani alikuwa mwana mshikamanifu, lakini alikuwa pia rafiki mshikamanifu. Sasa kwa kuwa ushikamanifu huo ulipingana, ni upi ungeshinda?

Yonathani akazungumza: “Mfalme, usimtendee dhambi mtumishi wako Daudi kwa sababu yeye hajakutendea dhambi na mambo aliyokufanyia yamekunufaisha. Alihatarisha uhai wake alipomuua yule Mfilisti, na Yehova akawapa Waisraeli wote ushindi mkubwa. Uliona jambo hilo, ukashangilia sana. Basi kwa nini uitendee dhambi damu isiyo na hatia kwa kuagiza Daudi auawe bila sababu?” Kwa ajabu katika pindi hii moja Sauli alitenda kwa usawaziko na kumsikiliza Yonathani hivi kwamba akaapa hatamuumiza Daudi. Lakini Sauli hakutimiza ahadi yake. Baada ya Daudi kupata ushindi mwingine, Sauli alijawa na hasira hivi kwamba akamtupia mkuki! (1 Samweli 19:4-6, 9, 10) Lakini Daudi akaponyoka na kukimbia kutoka nyumbani kwa Sauli.

Je, umewahi kukabili changamoto ya ushikamanifu unaopingana? Inaweza kuwa hali ngumu sana. Katika pindi kama hizo, huenda watu fulani wakakushauri kwamba sikuzote unapaswa kuwa mshikamanifu kwa familia yako. Lakini Yonathani alijua jambo linalofaa ni lipi. Angewezaje kumuunga mkono baba yake wakati ambapo Daudi alikuwa mtumishi mshikamanifu na mtiifu wa Yehova? Kwa hiyo, Yonathani aliruhusu ushikamanifu wake kwa Yehova uongoze uamuzi wake. Hiyo ndiyo sababu alimtetea Daudi waziwazi. Ingawa Yonathani alitanguliza ushikamanifu wake kwa Mungu, bado alionyesha kwamba yeye ni mshikamanifu kwa baba yake kwa kumshauri kwa unyoofu badala ya kumwambia alichotaka kusikia. Kila mmoja wetu anaweza kunufaika kwa kuiga njia ambayo Yonathani alionyesha ushikamanifu.

Ushikamanifu Unaleta Wajibu

Yonathani alijaribu tena kumsaidia Sauli afanye amani na Daudi, lakini Sauli hata hakumsikiliza. Daudi akakutana na Yonathani kisiri na kumweleza kwamba anahofia uhai wake uko hatarini. Alimwambia rafiki yake mwenye umri mkubwa hivi: “Kuna hatua moja tu kati yangu na kifo!” Yonathani alikubali kuchunguza hisia za baba yake kisha amjulishe Daudi hali ikoje. Daudi angejificha, naye Yonathani angempasha habari kwa kutumia upinde na mishale. Yonathani alimwomba Daudi aape kuhusu jambo moja tu: “Usiache kamwe kuitendea nyumba yangu kwa upendo mshikamanifu, hata Yehova atakapowafagilia mbali maadui wote wa Daudi duniani pote.” Daudi alikubali kwamba sikuzote angewatunza na kuwalinda watu wa nyumba ya Yonathani.​—1 Samweli 20:​3, 13-​27.

Yonathani alijaribu kumsifu Daudi mbele ya Sauli, lakini mfalme akakasirika! Akamwita Yonathani “mwana wa mwanamke mwasi” na akamwambia kwamba ushikamanifu wake kwa Daudi uliiaibisha familia yao. Akajaribu kumchochea Yonathani ajifikirie: “Maadamu mwana wa Yese anaishi duniani, wewe wala ufalme wako hautadumu.” Bila kuyumbishwa, Yonathani akamsihi tena baba yake: “Kwa nini auawe? Amefanya nini?” Sauli akalipuka kwa jeuri! Ingawa alikuwa amezeeka, bado Sauli alikuwa shujaa mwenye nguvu. Akamrushia mwana wake mkuki! Ingawa alikuwa na ustadi wa kutupa mikuki, mkuki huo ulimkosa. Akiwa amehuzunishwa na kuaibishwa, Yonathani akaondoka kwa hasira.​—1 Samweli 20:24-34.

Yonathani alishinda jaribu la kuwa mwenye ubinafsi

Asubuhi iliyofuata, Yonathani akaenda kwenye uwanja karibu na mahali ambapo Daudi alikuwa amejificha. Alirusha mshale kama walivyokuwa wamekubaliana, na kumjulisha Daudi kwamba Sauli alikuwa amekusudia kumuua. Kisha Yonathani akamwambia mtumishi wake arudi jijini. Yeye na Daudi wakaachwa peke yao, hivyo wakawa na muda mfupi wa kuzungumza. Wote wawili wakalia, na kwa huzuni Yonathani akamuaga Daudi, rafiki yake mwenye umri mdogo ambaye sasa angeanza maisha mapya akiwa mkimbizi.​—1 Samweli 20:35-​42.

Licha ya kukabili hali ngumu, Yonathani alithibitika kuwa mshikamanifu na si mwenye ubinafsi. Shetani, adui ya watu waaminifu, angalipenda sana kumwona Yonathani akimwiga Sauli na kutanguliza tamaa ya kupata ukuu au kusifiwa. Kumbuka, Shetani anapenda kuchochea mwelekeo wenye dhambi wa wanadamu. Alifaulu kufanya hivyo katika kisa cha Adamu na Hawa, wazazi wetu wa kwanza. (Mwanzo 3:1-6) Hata hivyo, hakufaulu kumchochea Yonathani. Lazima Shetani awe alikasirika sana. Je, wewe pia utamshinda anapokujaribu? Tunaishi wakati ambapo ubinafsi unawaathiri watu kila mahali. (2 Timotheo 3:1-5) Je, tutajifunza kutokana na roho ya ushikamanifu na isiyo na ubinafsi ya Yonathani?

Kwa kuwa alikuwa rafiki mshikamanifu, Yonathani alimtolea ishara rafiki yake Daudi ili kumwepusha na hatari

“Nilikupenda Sana”

Kadiri muda ulivyopita, chuki ya Sauli kumwelekea Daudi ikatawala kabisa kufikiri kwake na hisia zake. Yonathani hakuwa na la kufanya ila tu kumtazama baba yake akitenda kama mtu mwenye wazimu, akikusanya jeshi lake na kuliongoza nchi nzima ili kumtafuta na kumuua mtu mmoja tu ambaye hakuwa na hatia. (1 Samweli 24:​1, 2, 12-​15; 26:20) Je, Yonathani alihusika? Kwa kupendeza, Maandiko hayamtaji popote wakati wa kampeni hizo zisizofaa. Ushikamanifu wa Yonathani kwa Yehova, Daudi, na kiapo chake cha urafiki ulimzuia kufanya hivyo.

Hisia zake kuelekea rafiki yake mwenye umri mdogo hazikuwahi kubadilika. Baada ya muda, alitafuta njia ya kukutana na Daudi tena. Walikutania Horeshi, jina linalomaanisha “Eneo Lenye Miti.” Horeshi lilikuwa eneo la mlimani la porini, ambalo huenda liko kilomita kadhaa hivi kutoka Hebroni. Kwa nini Yonathani alihatarisha uhai wake kumwona mkimbizi huyo? Biblia inatuambia kwamba nia yake ilikuwa kumsaidia Daudi “kupata nguvu katika Yehova.” (1 Samweli 23:16) Yonathani alifanyaje hivyo?

Yonathani alimwambia rafiki yake kijana hivi: “Usiogope.” Kisha akaongezea uhakikisho huu: “Sauli baba yangu hatakupata.” Uhakika huo ulitegemea nini? Ulitegemea imani yenye nguvu ya Yonathani kwamba kusudi la Yehova litatimia. Aliendelea kusema hivi: “Utakuwa mfalme wa Israeli.” Nabii Samweli alikuwa ametumwa kusema maneno hayo miaka mingi mapema, na sasa Yonathani alimkumbusha Daudi kwamba sikuzote neno la Yehova linategemeka. Naye Yonathani alifikiri hali itakuwaje kwake wakati ujao? “Nitakuwa wa pili baada yako.” Huo ulikuwa unyenyekevu mkubwa kama nini! Angeridhika kutumikia chini ya uongozi wa mwanamume huyo ambaye alimzidi kwa miaka 30, na kumuunga mkono! Yonathani alimalizia kwa kusema: “Sauli baba yangu anajua jambo hilo.” (1 Samweli 23:17, 18) Moyoni mwake, Sauli alijua kwamba asingeweza kumshinda mwanamume ambaye Yehova alikuwa amemchagua kuwa mfalme anayefuata!

Yonathani alimtia moyo Daudi alipokuwa na uhitaji

Katika miaka iliyofuata, bila shaka Daudi alifurahia kutafakari pindi hiyo ambayo walikutana. Hiyo ndiyo iliyokuwa mara yao ya mwisho kukutana. Kwa kusikitisha, tamaa ya Yonathani ya kuwa wa pili baada ya Daudi haikutimizwa.

Yonathani aliandamana na baba yake kwenda vitani dhidi ya Wafilisti waliokuwa wamejitangaza wazi kuwa maadui wa Waisraeli. Angeweza kupigana kando ya baba yake akiwa na dhamiri safi, kwa sababu hakuruhusu makosa ya baba yake yaingilie utumishi wake kwa Yehova. Alipigana kwa uhodari na kwa ushikamanifu kama kawaida, lakini Waisraeli hawakushinda pigano hilo. Uovu wa Sauli ulikuwa mbaya sana hivi kwamba akahusika katika kuwasiliana na pepo, kosa ambalo lilistahili kifo chini ya Sheria ya Mungu, kwa hiyo Yehova hakuendelea kumbariki Sauli. Wana watatu wa Sauli, kutia ndani Yonathani, waliuawa vitani. Sauli alijeruhiwa, kisha akajiua.​—1 Samweli 28:​6-​14; 31:​2-6.

Yonathani alisema, “Utakuwa mfalme wa Israeli, nami nitakuwa wa pili baada yako.”—1 Samweli 23:17

Daudi alihuzunika sana. Mwanamume huyo mwenye fadhili na mwenye kusamehe hata alimwombolezea Sauli, ambaye alikuwa amemtesa na kufanya maisha yake yawe magumu! Daudi aliandika wimbo wa maombolezo kwa ajili ya Sauli na Yonathani. Huenda maneno yenye kugusa moyo zaidi ni yale ambayo aliandika kumhusu rafiki yake: “Nimehuzunika kwa ajili yako, ndugu yangu Yonathani; nilikupenda sana. Upendo wako kwangu ulikuwa mzuri sana kuliko upendo wa wanawake.”​—2 Samweli 1:​26.

Daudi hakusahau kamwe kiapo chake kwa Yonathani. Miaka mingi baadaye alimtafuta na kumtunza Mefiboshethi, mwana wa Yonathani aliyekuwa mlemavu. (2 Samweli 9:​1-​13) Ni wazi kwamba Daudi alikuwa amejifunza mengi kutokana na ushikamanifu na heshima ya Yonathani na utayari wake wa kushikamana kwa ushikamanifu na rafiki yake hata ikiwa angelazimika kukabiliana na hali ngumu ili kudumisha ushikamanifu huo. Je, sisi tutajifunza masomo kama hayo pia? Je, tunaweza kuwatafuta marafiki kama Yonathani? Je, tunaweza kuwa marafiki wa aina hiyo? Tukiwasaidia marafiki wetu kujenga na kuimarisha imani yao katika Yehova, tukitanguliza ushikamanifu kwa Mungu, na tukidumisha ushikamanifu wetu badala ya kutanguliza faida zetu, tutakuwa marafiki wa kweli kama Yonathani alivyokuwa. Nasi tutaiga imani yake.

^ fu. 7 Yonathani anapotajwa kwa mara ya kwanza katika simulizi la Biblia, mwanzoni mwa utawala wa Sauli, alikuwa kamanda wa jeshi, hivyo, lazima awe alikuwa na umri wa zaidi ya miaka 20. (Hesabu 1:3; 1 Samweli 13:2) Sauli alitawala kwa miaka 40. Kwa hiyo, kufikia wakati ambapo Sauli anakufa, Yonathani alikuwa na umri wa miaka 60 hivi. Daudi alikuwa na umri wa miaka 30 Sauli alipokufa. (1 Samweli 31:2; 2 Samweli 5:4) Kwa hiyo, ni wazi kwamba Yonathani alimzidi Daudi umri kwa miaka 30.