Hamia kwenye habari

IGENI IMANI YAO | MIRIAMU

“Mwimbieni Yehova”!

“Mwimbieni Yehova”!

Msichana mdogo alijificha mahali ambapo hangeonekana, macho yake yakiangalia sehemu hususa kati ya matete. Alikaa bila kusogea, akiwa na wasiwasi mwingi, huku Mto Nile ukiendelea kutiririka. Muda ulizidi kusonga, lakini alibaki palepale akitazama sehemu hiyo hususa, licha ya kwamba wadudu walirukaruka kumzunguka. Hapo alipokuwa akikazia fikira, kulikuwa na kikapu kisichoweza kupenyeza maji, na ndani ya kikapu hicho kulikuwa na ndugu yake mchanga. Alihuzunika alipofikiria kumhusu mdogo wake akiwa ndani ya kikapu hicho bila msaada wowote. Lakini alijua kwamba uamuzi wa wazazi wake ulifaa kabisa; hiyo tu ndiyo njia ambayo ndugu yake angeendelea kuwa hai wakati huo ambapo mambo mabaya yalikuwa yakitendeka.

Msichana huyo alikuwa akionyesha ujasiri kwa kukaa hapo, lakini baada ya muda mfupi angehitaji kuwa jasiri zaidi. Moyoni mwake sifa muhimu sana ilikuwa ikisitawi—imani. Tukio fulani lilikuwa karibu sana kutokea ambalo lingeathiri maisha yake yote. Miaka mingi baadaye, alipozeeka, imani yake ingemwongoza katika kipindi muhimu zaidi katika historia ya watu wake. Pindi nyingine, sifa hiyohiyo ingemsaidia tena alipofanya kosa zito. Msichana huyo alikuwa nani? Na imani yake inaweza kutufundisha nini?

Miriamu Binti ya Watumwa

Biblia haituambii jina la msichana huyo, lakini hatuwezi kuwa na shaka alikuwa nani. Alikuwa Miriamu, mzaliwa wa kwanza wa Amramu na Yokebedi, watumwa Waebrania waliokuwa katika nchi ya Misri. (Hesabu 26:59) Ndugu yake mdogo baadaye aliitwa Musa. Haruni, aliyekuwa mkubwa kidogo kuliko Musa alikuwa na umri wa miaka mitatu hivi wakati huo. Haijulikani Miriamu alikuwa na umri gani, lakini inapatana na akili kusema kwamba huenda hakuwa amefikisha umri wa miaka kumi.

Miriamu aliishi katika nyakati ngumu kwa ajili ya watu wake. Wamisri waliwaona watu wake, Waebrania, kuwa tishio kubwa kwa hiyo wakawafanya kuwa watumwa na kuwatesa. Licha ya hilo, watumwa hao walivumilia na kuendelea kuongezeka idadi, kwa hiyo, Wamisri wakaamua kutumia mbinu yenye ukatili hata zaidi. Farao aliamuru kwamba watoto wote wa kiume wa Waebrania wauawe walipozaliwa. Bila shaka Miriamu alijua kuhusu imani ya wakunga wawili walioitwa Shifra na Pua, ambao hawakutii amri hiyo ya mfalme.—Kutoka 1:8-22.

Miriamu aliona pia imani ambayo wazazi wake walikuwa nayo. Baada ya mtoto wao wa tatu kuzaliwa, Amramu na Yokebedi walimficha kwa miezi mitatu ya kwanza. Hawakuacha woga wa agizo la mfalme liwafanye wamuue mtoto wao. (Waebrania 11:23) Lakini si rahisi kumficha mtoto, na walihitaji kufanya uamuzi mgumu sana. Yokebedi alijua kwamba alihitaji kumficha mtoto huyo mahali ambapo angepatikana tu na mtu ambaye angeweza kumlinda na kumtunza. Wazia sala nyingi ambazo mama huyo alitoa alipokuwa akishona kikapu kwa mafunjo, kukipaka lami na bereu ili kuzuia maji yasipenye, kisha kumwacha mtoto wake aliyempenda kwenye Mto Nile! Si ajabu kwamba alimwambia Miriamu akae hapo na kuangalia ni nini ambacho kingetokea.—Kutoka 2:1-4.

Miriamu Alikuwa Mkombozi

Kwa hiyo Miriamu akasubiri. Baada ya muda, aliona watu wakija. Wanawake kadhaa walifika hapo. Hawakuwa Wamisri wa kawaida. Alikuwa binti ya Farao na watumishi wake wa kike, na walikuja kwenye Mto Nile kuoga. Unaweza kuwazia jinsi Miriamu alivyoshuka moyo. Kwa kweli, haikupatana na akili kutarajia kwamba binti ya Farao mwenyewe angevunja amri ya mfalme na kumlinda mtoto Mwebrania. Lazima Miriamu awe alisali kwa bidii katika pindi hiyo.

Binti ya Farao ndiye aliyekuwa wa kwanza kutambua kulikuwa na kikapu katikati ya matete. Kwa hiyo, akamtuma mtumishi wake akilete. Simulizi hilo linasema hivi kumhusu binti ya mfalme: “Alipokifungua, alimwona mwana huyo akilia.” Mara moja alitambua kinachoendelea: Mama Mwebrania alikuwa akijaribu kumwokoa mtoto wake. Binti ya Farao alijawa na huruma kumwelekea yule mtoto. (Kutoka 2:5, 6) Bila shaka, Miriamu aliyekuwa akitazama kwa makini aliona uso wa mwanamke huyo ulionyesha hisia gani. Alijua kwamba wakati wake wa kuonyesha imani katika Yehova ulikuwa umefika. Alijipa ujasiri na kumkaribia binti ya Farao na watumishi wake.

Hatujui ni nini ambacho kwa kawaida kilitokea msichana mtumwa Mwebrania alipoamua kuzungumza na mtu wa familia ya mfalme. Hata hivyo, Miriamu alimuuliza binti ya mfalme swali la moja kwa moja: “Je, niende nikamwite mwanamke mlezi Mwebrania akunyonyeshee mtoto huyu?” Hilo lilikuwa swali lenye akili sana. Binti ya Farao alijua kwamba asingeweza kumnyonyesha mtoto. Huenda alihisi kwamba lingekuwa jambo la busara ikiwa mvulana huyo angelelewa na watu wake; kisha baadaye angemleta nyumbani kwake akiwa mwana wake wa kambo, halafu angemlea na kumwelimisha. Lazima Miriamu alishangilia binti ya mfalme alipomjibu kwa neno moja tu: “Nenda!”—Kutoka 2:7, 8.

Kwa ujasiri Miriamu alihakikisha kwamba ndugu yake alikuwa salama

Miriamu alikimbia kwenda nyumbani kwa wazazi wake waliokuwa na wasiwasi. Wazia jinsi alivyosisimka alipokuwa akimweleza mama yake mambo yaliyotokea. Inawezekana kwamba Yokebedi alitambua Yehova alikuwa akielekeza mambo, kwa hiyo, alienda na Miriamu hadi kwa binti ya Farao. Huenda Yokebedi alijaribu kujizuia asionyeshe kuwa amefurahi wakati ambapo binti ya mfalme alimwagiza hivi: “Mchukue mtoto huyu uninyonyeshee, nami nitakulipa.”—Kutoka 2:9.

Siku hiyo, Miriamu alijifunza mengi kumhusu Mungu wake, Yehova. Alijifunza kwamba anawajali watu wake na anasikiliza sala zao. Na alijifunza kwamba si watu wazima na wanaume tu ambao wanaweza kuonyesha ujasiri na imani. Yehova anawasikiliza watumishi wake wote waaminifu. (Zaburi 65:2) Sisi sote leo—vijana kwa wazee, wanaume kwa wanawake—tunahitaji kukumbuka jambo hilo katika siku hizi ngumu.

Miriamu Alikuwa Dada Mwenye Subira

Yokebedi alimnyonyesha na kumtunza mtoto huyo. Tunaweza kuwazia jinsi Miriamu alivyompenda sana ndugu yake ambaye alikuwa amemwokoa. Huenda alimsaidia kujifunza kuzungumza na alifurahi alipomsikia akisema jina la Mungu wake, Yehova kwa mara ya kwanza. Mtoto huyo alipokuwa mkubwa, wakati ulifika wa kumpeleka kwa binti ya Farao. (Kutoka 2:10) Lazima iwe familia yote ilihuzunika. Hata hivyo, lazima Miriamu awe alikuwa na hamu ya kuona Musa, kama alivyoitwa na binti ya Farao, angekuja kuwa mwanamume wa aina gani! Je, bado angeendelea kumpenda Yehova alipozidi kukua katika familia ya kifalme ya Misri?

Baada ya muda, jibu likawa wazi. Lazima Miriamu awe alijivunia kwamba ndugu yake ndogo alikuja kuwa mwanamume aliyechagua kumtumikia Mungu wake badala ya kujifaidi na nafasi zote alizopata katika familia ya kifalme ya Farao! Musa alipokuwa na umri wa miaka 40, aliwatetea watu wake. Alimuua Mmisri kwa kumdhulumu mtumwa Mwebrania. K wa kuwa Musa alijua angeuawa kwa kufanya hivyo, alikimbia kutoka Misri.—Kutoka 2:11-15; Matendo 7:23-29; Waebrania 11:24-26.

Huenda Miriamu hakusikia jambo lolote kumhusu ndugu yake kwa miaka 40 iliyofuata alipokuwa akiishi mbali Midiani, huku akichunga kondoo. (Kutoka 3:1; Matendo 7:29, 30) Muda ulipita na Miriamu aliendelea kuzeeka huku akitazama jinsi kuteseka kwa watu wake kulivyozidi kuongezeka.

Miriamu Nabii wa Kike

Huenda Miriamu alikuwa na zaidi ya miaka 80 Musa aliporudi, akiwa ametumwa na Mungu kuwakomboa watu Wake. Haruni alikuwa msemaji wa Musa, na ndugu wawili wa Miriamu wakamwendea Farao ili kumwomba awaruhusu watu wa Mungu waondoke. Bila shaka, alifanya yote aliyoweza kuwaunga mkono na kuwatia moyo kila mara waliporudi baada ya Farao kukataa kuwasikiliza huku Yehova akileta mapigo kumi kuwaonya Wamisri. Hatimaye, baada ya pigo la mwisho—kuuawa kwa mzaliwa wa kwanza wa wana wa Misri—wakati ulifika wa Waisraeli Kutoka Misri! Mwazie Miriamu akiwasaidia watu wake walipokuwa wakiondoka huku Musa akiwaongoza.—Kutoka 4:14-16, 27-31; 7:1–12:51.

Baadaye, ilipoonekana kwamba Waisraeli wamenaswa na jeshi la Wamisri lililokuwa linawafuatilia na Bahari Nyekundu ikiwa mbele yao, Miriamu alimwona Musa ndugu yake akisimama mbele ya bahari na kuinua fimbo yake. Bahari ikagawanyika! Alipomtazama ndugu yake akiwavusha watu kwenye sakafu ya bahari, lazima imani ya Miriamu iwe iliimarishwa kuliko wakati mwingine wowote. Alikuwa na uhakika kwamba Mungu wake angeweza kufanya chochote, na kutimiza ahadi yoyote ile anayotoa!—Kutoka 14:1-31.

Baadaye, watu walipovuka salama na bahari ikarudi na kumzamisha Farao na jeshi lake, Miriamu aliona kwamba Yehova alikuwa mwenye nguvu zaidi kuliko jeshi lenye nguvu zaidi ulimwenguni. Watu walichochewa kumwimbia Yehova wimbo. Miriamu aliwaongoza wanawake kuimba maneno haya: “Mwimbieni Yehova, kwa maana amekwezwa sana. Farasi na mpandaji wake amewavurumisha baharini.”—Kutoka 15:20, 21; Zaburi 136:15.

Miriamu alichochewa kuwaongoza wanawake Waisraeli kuimba wimbo wa ushindi kwenye Bahari Nyekundu

Hiyo ilikuwa mojawapo ya pindi bora zaidi maishani mwa Miriamu, pindi ambapo hangesahau kamwe. Hapo ndipo Biblia inamwita Miriamu nabii. Miriamu ndiye aliyekuwa mwanamke wa kwanza kuitwa nabii. Yeye ni mmoja kati ya wanawake wachache tu waliomtumikia Yehova katika njia hiyo ya pekee.—Waamuzi 4:4; 2 Wafalme 22:14; Isaya 8:3; Luka 2:36.

Hivyo, Biblia inatukumbusha kwamba Yehova anatutazama na ana hamu ya kutubariki kwa jitihada zetu za unyenyekevu, subira, na tamaa yetu ya kumsifu. Vijana kwa wazee, wanaume kwa wanawake, sikuzote na tuwe na imani katika Yehova. Imani kama hiyo inamfurahisha; hasahau kamwe imani ya aina hiyo naye yuko tayari kututhawabisha kwa sababu ya kuionyesha. (Waebrania 6:10; 11:6) Hiyo inatupa sababu nzuri ya kuiga imani ya Miriamu!

Miriamu Mwenye Kiburi

Mapendeleo na umashuhuri huleta baraka na pia hatari. Waisraeli walipokombolewa kutoka utumwani, huenda Miriamu ndiye aliyekuwa mwanamke aliyejulikana zaidi katika taifa lote. Je, angekuwa na kiburi na kujitakia umashuhuri? (Methali 16:18) Inasikitisha kwamba kuna wakati ambapo alifanya hivyo.

Miezi kadhaa baada ya Kutoka Misri, Musa alitembelewa na kikundi kilichosafiri kutoka mbali—Yethro, baba-mkwe wake, ambaye alimletea Musa mke wake, aliyeitwa Sipora na wana wao wawili. Musa alikuwa ameoa alipokuwa akiishi Midiani kwa miaka 40. Mapema Sipora alikuwa amerudi nyumbani kule Midiani, huenda ili kutembea, na sasa baba yake alikuwa akimrudisha kwenye kambi ya Waisraeli. (Kutoka 18:1-5) Wazia jinsi Waebrania walivyosisimka Sipora alipofika! Huenda wengi walikuwa na hamu ya kumwona mke wa mtu ambaye Mungu alikuwa amechagua kuwakomboa kutoka Misri.

Je, Miriamu alifurahi kumwona Sipora? Huenda mwanzoni alifurahi. Lakini inaonekana kamba baada ya muda aliruhusu kiburi kimdhibiti. Huenda aliona kwamba Sipora angekuwa maarufu kuliko yeye katika taifa lote. Vyovyote vile, Miriamu na Haruni walianza kusema mambo mabaya dhidi ya Musa. Na kama kawaida, mazungumzo kama hayo hugeuka kuwa yenye chuki. Mwanzoni walilalamika kumhusu Sipora; walilalamika kwamba yeye si Mwisraeli bali ni Mkushi. * Lakini mazungumzo hayo yalibadilika kuwa malalamiko dhidi ya Musa mwenyewe. Miriamu na Haruni walisema: “Je, Yehova amezungumza kupitia Musa peke yake? Je, hajazungumza kupitia sisi pia?”—Hesabu 12:1, 2.

Miriamu Apigwa na Ukoma

Maneno hayo yanatuonyesha kwamba sumu mbaya sana ilikuwa ikisitawi ndani ya Miriamu na Haruni. Kwa kuwa hawakuridhishwa na jinsi Yehova alivyokuwa akimtumia Musa, walitaka kuwa na mamlaka na uvutano mkubwa. Je, ni kwamba Musa alikuwa akitumia mamlaka yake vibaya na kujaribu kujitafutia makuu? Ni kweli kwamba hakuwa mkamilifu, lakini Musa hakujitafutia makuu wala hakuwa na kiburi. Maandiko yaliyoongozwa na roho yanasema: “Musa alikuwa mtu mpole zaidi kuliko watu wote duniani.” Vyovyote vile, Miriamu na Haruni walikosea kulalamika kwa njia hiyo dhidi ya Musa, na walikuwa hatarini. Simulizi hilo linasema, “Yehova alikuwa akisikiliza.”—Hesabu 12:2, 3.

Ghafla, Yehova akawaita wote watatu kwenye hema la mkutano. Ile nguzo kubwa ya wingu, iliyowakilisha kuwepo kwa Yehova, ilishuka na kusimama kwenye mlango. Kisha Yehova akazungumza. Aliwashutumu Miriamu na Haruni, akiwakumbusha kuhusu uhusiano wa pekee ambao Yeye na Musa walikuwa nao na jinsi alivyomwamini kabisa. Yehova akawauliza: “Kwa nini, basi, hamkuogopa kusema vibaya kumhusu Musa, mtumishi wangu?” Lazima Miriamu na Haruni walitetemeka. Yehova aliona kwamba kukosa kumheshimu Musa kulikuwa sawa na kukosa kumheshimu Yehova mwenyewe.—Hesabu 12:4-8.

Inaonekana kwamba Miriamu ndiye aliyekuwa mchochezi wa jambo hilo, na kumfanya ndugu yake mdogo ajiunge naye kumpinga wifi yao. Hiyo inaweza kutusaidia kueleza kwa nini Miriamu ndiye aliyeadhibiwa. Yehova alimpiga kwa ukoma. Ugonjwa huo wenye kuogopesha ulifanya ngozi yake iwe ‘nyeupe kama theluji.’ Mara moja Haruni akajinyenyekeza mbele ya Musa, akamsihi amwombe Yehova awasamehe, akisema: “Tumetenda kwa upumbavu.” Musa, aliyekuwa mpole, akamlilia Yehova: “Ee Mungu, tafadhali mponye! Tafadhali!” (Hesabu 12:9-13) Musa na Haruni walihuzunika sana kwa sababu ya hali ya dada yao kwa sababu walimpenda sana, licha ya udhaifu wake.

Miriamu Aponywa

Yehova alitenda kwa rehema. Alimponya Miriamu alipotubu. Hata hivyo, Yehova alisema kwamba Miriamu atengwe kwa siku saba nje ya kambi ya Israeli. Lazima Miriamu aliaibika kutii agizo hilo kwa sababu wote katika kambi wangejua alikuwa ametiwa nidhamu. Lakini imani yake ilimwokoa. Moyoni mwake alijua kwamba Baba yake, Yehova, alikuwa mwenye haki na alikuwa akimtia nidhamu kwa sababu alimpenda. Kwa hiyo, alifanya kama alivyoagizwa. Siku saba zilipita huku Waebrania katika kambi wakisubiri. Kisha Miriamu alionyesha imani tena—kwa kukubali kwa unyenyekevu ‘kurudishwa kambini.’—Hesabu 12:14, 15.

Yehova huwatia nidhamu wale anaowapenda. (Waebrania 12:5, 6) Alimpenda Miriamu sana hivi kwamba asingemruhusu aendelee kuwa na kiburi. Miriamu aliumia aliporekebishwa, lakini kufanya hivyo kulimwokoa. Kwa sababu alikubali nidhamu kwa imani, alipata tena kibali cha Mungu. Aliendelea kuishi hadi karibu na mwisho wa safari ya Waisraeli nyikani. Huenda alikuwa anakaribia umri wa miaka 130 alipokufa huko Kadeshi katika nyika ya Zini. * (Hesabu 20:1) Karne nyingi baadaye, kwa upendo Yehova alimsifu Miriamu kwa utumishi wake mwaminifu. Kupitia nabii wake Mika, aliwakumbusha watu wake hivi: “Kutoka katika nyumba ya utumwa niliwakomboa; nilimtuma Musa, Haruni, na Miriamu mbele yenu.”—Mika 6:4.

Imani ya Miriamu ilimwezesha kuendelea kuwa mnyenyekevu Yehova alipomtia nidhamu

Tunaweza kujifunza mengi kutokana na maisha ya Miriamu. Tunahitaji kuwalinda wale ambao hawawezi kujilinda na kuzungumza kwa ujasiri ili kutetea kilicho sawa, kama Miriamu alivyofanya alipokuwa mdogo. (Yakobo 1:27) Kama yeye, tunahitaji kuwafundisha wengine ujumbe wa Mungu kwa shangwe. (Waroma 10:15) Kama Miriamu, tunapaswa kuepuka sifa mbaya za wivu na uchungu. (Methali 14:30) Na kama yeye, tunahitaji kuwa wanyenyekevu na kubali kurekebishwa na Yehova. (Waebrania 12:5) Tunapofanya mambo hayo, tutaiga imani ya Miriamu.

^ fu. 21 Katika kisa cha Sipora, ni wazi kwamba neno “Mkushi” lilimaanisha kwamba ametoka Arabia, kama Wamidiani wengine, na si kutoka Ethiopia.

^ fu. 26 Wote watatu walikufa kwa mfuatano waliozaliwa—kwanza Miriamu, kisha Haruni, halafu Musa—inaonekana ndani ya mwaka uleule.