Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

IGENI IMANI YAO | DEBORA

‘Nilisimama kama Mama katika Israeli’

‘Nilisimama kama Mama katika Israeli’

DEBORA aliwatazama wanajeshi waliokuwa wamekusanyika juu ya Mlima Tabori. Alitiwa moyo sana kuwaona. Asubuhi na mapema alikuwa akitafakari kuhusu ujasiri na imani ya kiongozi wao, Baraka. Ijapokuwa walikuwa wanaume 10,000 wenye nguvu, imani na ujasiri wao ungejaribiwa kwa kiasi kikubwa siku hiyo. Walikuwa wakipambana na adui hatari, aliyekuwa na wanajeshi wengi na silaha nyingi. Hata hivyo, wamekuja kupigana kwa sababu ya kutiwa moyo na mwanamke huyo.

Wazia nguo ya Debora, ikipepea huku na huku kutokana na upepo, huku yeye na Baraka wakitazama mandhari yenye kuvutia. Umbo la Mlima Tabori ni kama pia kubwa isiyo na makali katika ncha yake. Kilele chake kilicho tambarare kinafanya iwe rahisi kuona Uwanda wa Esdraeloni, ulio meta 400 chini na kusambaa upande wa kusini-magharibi. Mto Kishoni unapita katikati ya eneo lenye nyasi na kumwaga maji yake kwenye Bahari Kuu kupitia Mlima Karmeli. Huenda bonde la mto huo halikuwa na maji asubuhi hiyo, lakini kitu fulani chenye kung’aa kilionekana kikitokea kwa mbali. Jeshi la Sisera lilikuwa likikaribia, likiwa na vyombo vya chuma vinavyong’aa. Sisera alijivunia jeshi lake lililokuwa na magari ya vita 900, ambayo huenda yalikuwa na miundu ya chuma iliyotokeza katika ekseli zake. Sisera alikusudia kuwaangamiza Waisraeli hao wasiokuwa na zana za kutosha za kivita, kama vile mtu anavyovuna shayiri!

Debora alijua kwamba Baraka na watu wake walikuwa wanangojea ishara au neno kutoka kwake. Je, Debora alikuwa mwanamke pekee mahali hapo? Alihisije kubeba jukumu hilo katika pindi hiyo? Je, hakujua kusudi la kuwa hapo? Hapana! Yehova, Mungu wake, alikuwa amemwambia aanzishe vita hiyo; na alimwambia pia kwamba angetumia mwanamke kushinda vita hiyo. (Waamuzi 4:9) Tunaweza kujifunza nini kuhusu imani kutokana na mfano wa Debora na wapiganaji jasiri?

“NENDA USAMBAE KATIKA MLIMA TABORI”

Biblia inapomtaja kwa mara ya kwanza Debora, inamrejelea kuwa “nabii wa kike.” Cheo hicho kinamfanya Debora awe wa pekee katika masimulizi ya Biblia ingawa haimaanishi kwamba ni yeye tu aliyekuwa na cheo kama hicho. * Debora alikuwa na daraka lingine pia. Inaonekana kwamba alitatua migogoro kwa kutoa majibu ya Yehova, matatizo yalipotokea.—Waamuzi 4:4, 5.

Debora aliishi katika eneo lenye milima la Efraimu, lililokuwa kati ya mji wa Betheli na Rama. Alikuwa na kawaida ya kukaa chini ya mtende na kutumikia watu kulingana na mwongozo wa Yehova. Ni wazi kwamba mgawo wake ulikuwa na changamoto, hata hivyo, Debora hakuruhusu hilo limvunje moyo. Kazi yake ilikuwa muhimu sana. Alishiriki kutunga wimbo ulioandikwa kwa mwongozo wa roho ya Mungu ambao ulitia ndani maneno haya kuhusu watu wake waliokosa kuwa waaminifu: “Wakaanza kuchagua miungu mipya. Ndipo kukawa na vita malangoni.” (Waamuzi 5:8) Kwa kuwa Waisraeli walimwacha Yehova na kutumikia miungu mingine, Yehova aliacha washambuliwe na adui zao. Mfalme wa Kanaani, Yabini, aliwatawala kupitia Sisera, mkuu wa majeshi mwenye nguvu.

Sisera! Jina hilo lilipotajwa katika Israeli lilifanya watu waogope na kushtuka. Dini na utamaduni wa Wakanaani ulikuwa wenye ukatili, kwa kuwa walitoa watoto wao kuwa dhabihu na walifanya ukahaba hekaluni. Hali ilikuwaje mkuu huyo wa jeshi la Kanaani na jeshi lake walipotawala nchi hiyo? Wimbo wa Debora unaonyesha kwamba ilikuwa vigumu kusafiri nchini na maisha katika maeneo ya vijijini yalikuwa magumu, hivyo watu walihama. (Waamuzi 5:6, 7) Tunaweza kuwazia jinsi ambavyo watu walikuwa wakiogopa na kujificha katika mapori na vilima, wakiogopa kulima au kuishi katika vijiji ambavyo havikuwa na ukuta na wakiogopa sana kushambuliwa kwa sababu ya kusafiri barabarani, watoto wao kutekwa, na wanawake wao kubakwa. *

Hofu ilitawala nchini kwa miaka 20 mpaka Yehova alipoona wazi kwamba watu wake wakaidi walikuwa tayari kubadilika au, kama wimbo ulioandikwa na Debora na Baraka kwa mwongozo wa roho ya Mungu unavyosema, “Mpaka mimi, Debora, niliposimama, mpaka niliposimama kama mama katika Israeli.” Hatujui ikiwa Debora, mke wa Lapidothi, alikuwa na watoto, lakini usemi huo ulikuwa lugha ya mfano. Ni kana kwamba Yehova alimpa Debora mgawo wa kulinda taifa hilo kama vile mama angefanya kwa watoto wake. Alimwagiza amwambie Mwamuzi Baraka, mwanamume mwenye imani yenye nguvu, aende kupigana na Sisera.—Waamuzi 4:3, 6, 7; 5:7.

Debora alimtia moyo Baraka awaokoe watu wa Mungu

Yehova alitoa agizo hili kupitia Debora: “Nenda, usambae katika Mlima Tabori.” Baraka alipaswa kukusanya wanaume 10,000 kutoka makabila mawili ya Israeli. Debora alitaja ahadi ya Mungu kwamba wanaume hao wangemshinda Sisera mwenye nguvu na magari yake 900 ya vita! Bila shaka ahadi hiyo ilimfanya Baraka astaajabu. Waisraeli hawakuwa na jeshi wala silaha. Licha ya hali hiyo, Baraka alikubali kwenda vitani ikiwa tu Debora angeenda pamoja naye katika Mlima Tabori.—Waamuzi 4:6-8; 5:6-8.

Kwa sababu ya ombi hilo, watu fulani hudai kwamba Baraka hakuwa na imani, lakini jambo hilo si kweli. Baraka hakumwomba Mungu ampe silaha zaidi. Akiwa mwanamume mwenye imani, Baraka aliona umuhimu wa kuandamana na mwakilishi wa Yehova ili kumwimarisha na kuimarisha watu wake. (Waebrania 11:32, 33) Yehova alikubali ombi lake. Alimruhusu Debora kwenda na Baraka kama alivyoomba. Hata hivyo, Yehova alimwezesha Debora kutabiri kwamba ushindi wa pigano hilo usingetokana na mwanamume. (Waamuzi 4:9) Mungu aliamua kwamba mwanamke ndiye atakayemuua Sisera aliyekuwa mwovu!

Katika ulimwengu wa leo, wanawake wanakabili matendo mengi ya ukosefu wa haki, jeuri, na kutendewa vibaya. Ni mara chache sana wanatendewa kwa heshima kama Mungu anavyotaka watendewe. Hata hivyo, machoni pa Mungu, wanawake na wanaume wana haki sawa na wanaweza kupata kibali chake. (Waroma 2:11; Wagalatia 3:28) Mfano wa Debora unatukumbusha kwamba Mungu huwabariki wanawake kwa kuwapa mapendeleo na hilo linaonyesha kwamba anawatumaini na kuwapa kibali chake. Ni muhimu kwamba tuepuke kuwa na maoni yasiyofaa kuelekea wanawake yaliyoenea ulimwenguni leo.

“DUNIA ILITIKISIKA, MBINGU PIA ZIKATIRIRIKA MAJI”

Baraka alikusanya jeshi lake. Alikusanya wanaume 10,000 jasiri ili kupambana na jeshi la Sisera lenye kutisha. Baraka alipokuwa akiongoza watu wake kuelekea Mlima Tabori alithamini sana kwamba alikuwa na uwezo wa kuchochea ujasiri wao. Tunasoma hivi: “Debora akapanda pamoja naye.” (Waamuzi 4:10) Wazia jinsi wanajeshi hao walivyotiwa moyo walipomwona mwanamke huyo jasiri akiambatana nao kuelekea Mlima Tabori, akiwa tayari kuhatarisha maisha yake kwa kuwa pamoja nao kwa sababu ya imani yake kwa Yehova Mungu!

Sisera alichukua hatua mara moja alipojua kwamba jeshi la Israeli limejikusanya ili kupigana naye. Wafalme kadhaa wa Kanaani walimuunga mkono Mfalme Yabini ambaye huenda alikuwa na nguvu zaidi kati yao. Kisha, magari ya kivita ya Sisera yalitikisa ardhi yalipoenda pamoja katika eneo tambarare. Wakanaani walikuwa na uhakika kabisa kwamba wangelishinda jeshi la Israeli.—Waamuzi 4:12, 13; 5:19.

Baraka na Debora wangefanya nini adui anapokaribia? Ikiwa wangebaki katika miteremko ya Mlima Tabori, huenda ingekuwa rahisi kwao kushinda majeshi ya Kanaani kwa kuwa magari yao ya vita yalihitaji eneo tambarare ili kushambulia vizuri. Hata hivyo, Baraka alitaka kupigana kulingana na maagizo ya Yehova, hivyo alisubiri mwelekezo kutoka kwa Debora. Hatimaye, mwelekezo ukatolewa. Debora alisema hivi: “Simama, kwa maana hii ndiyo siku ambayo Yehova hakika atamtia Sisera mkononi mwako. Je, Yehova siye ambaye ameenda mbele yako?” Kisha tunasoma hivi: “Baraka akashuka kutoka Mlima Tabori akiwa na wanaume elfu kumi nyuma yake.”—Waamuzi 4:14. *

Jeshi la Israeli lilisonga kwa kasi na kushuka mlimani mpaka eneo la wazi, tambarare, kuelekea magari hayo ya kivita yenye kutisha. Je, Yehova alienda mbele yao kama Debora alivyoahidi? Jibu lilipatikana baada ya muda mfupi. Tunasoma hivi: “Dunia ilitikisika, mbingu pia zikatiririka maji.” Jeshi la Sisera lenye kiburi halikujua la kufanya. Mvua ikaanza kunyesha. Inaonekana kwamba mvua hiyo ilikuwa kubwa sana hivi kwamba ikasababisha mafuriko makubwa katika bonde hilo. Hivyo, magari hayo ya kivita yaliyotengenezwa kwa chuma hayakufaa kitu. Yalizama kwenye matope kwa sababu ya mvua hiyo.—Waamuzi 4:14, 15; 5:4.

Baraka na wapiganaji wake hawakuathiriwa na dhoruba hiyo. Walijua chanzo chake. Waliyafuatilia majeshi ya Wakanaani. Wakitekeleza hukumu ya Mungu, Waisraeli waliua wanajeshi wote wa Sisera. Mto Kishoni ulifurika na kufagilia mbali maiti zote mpaka Bahari Kuu.—Waamuzi 4:16; 5:21.

Kama Debora alivyotabiri, Yehova alipigania watu wake na kushinda majeshi ya Sisera

Leo, Yehova hatumii watumishi wake kupigana vita halisi. Hata hivyo, anahimiza watu wake kupigana vita vya kiroho. (Mathayo 26:52; 2 Wakorintho 10:4) Tukijitahidi kumtii Mungu katika ulimwengu wa leo, tunaonyesha kwamba tunapigana vita hivyo. Tunahitaji ujasiri kwa kuwa wale wanaomtii Mungu leo wanaweza kukabili upinzani mkali. Hata hivyo, Yehova hajabadilika. Bado anawalinda wale wenye imani na wanaomtegemea kama Debora, Baraka, na wanajeshi jasiri wa taifa la Israeli walivyofanya.

“ATABARIKIWA ZAIDI KATI YA WANAWAKE”

Adui mkubwa zaidi Mkanaani alitoroka! Sisera, mkandamizaji mkuu wa watu wa Mungu, alikimbia kwa miguu kutoka katika uwanja wa vita. Akiwaacha watu wake wakifa kwenye matope, Sisera alifanikiwa kupita katikati ya wanajeshi Waisraeli na kukimbilia eneo kavu, akiwa na lengo la kukimbilia eneo lenye wafalme waliomuunga mkono. Aliteremka katika nyanda tambarare, huku akiwa na hofu kubwa kwamba huenda wanajeshi wa Israeli wangemkamata, alielekea katika mahema ya Heberi, Mkeni aliyetengana na watu wake wahamaji upande wa kusini na kufanya mkataba wa amani na Mfalme Yabini.—Waamuzi 4:11, 17.

Sisera alifika katika kambi ya Heberi akiwa amechoka. Hakumkuta Heberi nyumbani kwake. Hata hivyo, mke wake, Yaeli alikuwapo. Yawezekana kwamba Sisera alifikiri Yaeli angetenda kulingana na mkataba wa amani aliofanya mume wake na Mfalme Yabini. Huenda hakufikiri kwamba mwanamke huyo angetenda tofauti na mume wake. Ni wazi kwamba Sisera hakumjua Yaeli! Hata hivyo, Yaeli aliona wazi uovu aliofanya mkandamizaji huyo Mkanaani kuelekea Israeli; na yawezekana hilo lilifanya aone kwamba alipaswa kuchukua hatua. Alihitaji kuamua ama kumsaidia mwanamume huyo mwovu au kumtegemea Yehova na kumuua adui huyo wa Watu wake. Angefanya nini? Mwanamke atawezaje kumuua mpiganaji mwenye nguvu na uzoefu?

Yaeli alihitaji kufikiria haraka jambo la kufanya. Alimwonyesha Sisera mahali pa kupumzika. Sisera akamwamuru amfiche ili mwanamume yeyote atakayekuja kumtafuta asimpate. Yaeli akamfunika, na alipomwomba maji, akampa maziwa. Baada ya muda mfupi, Sisera alilala usingizi mzito. Kisha Yaeli akachukua kigingi cha hema, chombo ambacho wanawake wanaoishi katika mahema mara nyingi walitumia kwa ustadi. Akiwa amechuchumaa karibu na kichwa cha Sisera, Yaeli alikabili kazi ngumu ya kutenda akiwa mtekelezaji wa hukumu kwa niaba ya Yehova. Kusita au kutokuwa na uhakika wa jambo la kufanya kungesababisha madhara makubwa. Je, Yaeli alikumbuka watu wa Mungu na jinsi mwanamume huyo alivyowatesa kwa miaka mingi? Au je, alifikiria pendeleo alilokuwa nalo la kuchukua msimamo upande wa Yehova? Masimulizi hayatoi majibu. Tunajua tu kwamba Yaeli alichukua hatua. Sisera alikufa!—Waamuzi 4:18-21; 5:24-27.

Baadaye, Baraka alifika ili kumtafuta adui yake. Yaeli alipomwonyesha maiti ikiwa imepigiliwa kigingi katika kipaji cha uso, Baraka akajua kwamba unabii wa Debora umetimia. Mwanamke alimuua Sisera, shujaa mwenye nguvu! Wachambuzi wa mambo wa siku hizi wamemwita Yaeli majina mengi yasiyofaa, lakini Baraka na Debora walijua vizuri alichofanya Yaeli. Katika wimbo wao ulioongozwa na roho takatifu, walimsifu Yaeli kwa kusema kwamba “atabarikiwa zaidi kati ya wanawake” kwa sababu ya tendo lake la ujasiri. (Waamuzi 4:22; 5:24) Ni wazi kwamba Debora alikuwa mkarimu. Hakumsifu Yaeli huku akiwa na wivu; badala yake alikazia zaidi kutimizwa kwa neno la Yehova.

Nguvu za Mfalme Yabini mtawala aliyekuwa tishio kwa taifa la Israeli zilikoma Sisera alipouawa. Ukandamizaji wa Wakanaani ulikoma. Kukawa na amani kwa miaka 40. (Waamuzi 4:24; 5:31) Debora, Baraka na Yaeli walibarikiwa sana kwa sababu ya kudhihirisha imani katika Yehova Mungu. Tukiiga imani ya Debora, tukichukua kwa ujasiri msimamo thabiti upande wa Yehova, na kuwachochea wengine wafanye vivyo hivyo, Yehova atatubariki na kutusaidia kushinda na kutupatia amani ya kudumu.

^ fu. 7 Manabii wengine wa kike ni Miriamu, Hulda, na mke wa Isaya.—Kutoka 15:20; 2 Wafalme 22:14; Isaya 8:3.

^ fu. 9 Wimbo wa Debora unaonyesha kwamba mara nyingi Sisera alirudi kutoka katika uvamizi wa kijeshi akiwa na mali alizopata zilizotia ndani wasichana, na pindi fulani alimpa kila mwanajeshi msichana zaidi ya mmoja. (Waamuzi 5:30) Usemi ‘tumbo la uzazi,’ lililotumika katika mstari huo linaonyesha kwamba wanawake hao walithaminiwa tu kwa sababu ya viungo vyao vya uzazi. Inaonekana kwamba lilikuwa jambo la kawaida kwa wasichana kubakwa.

^ fu. 17 Pigano hilo linatajwa mara mbili katika Biblia, kwanza katika masimulizi ya historia yanayopatikana katika Waamuzi sura ya  4 na katika wimbo alioimba Debora na Baraka katika sura ya 5. Kila simulizi linategemeza lingine kwa kutaja mambo ambayo simulizi lingine halitaji na hivyo kukamilisha vizuri simulizi.