Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

MAMBO YA KUFANYA ILI KUWA NA FURAHA KATIKA FAMILIA

Kushugulika na Wale Walio Inje ya Familia Yako Ambayo Bibi ao Bwana Ana Watoto

Kushugulika na Wale Walio Inje ya Familia Yako Ambayo Bibi ao Bwana Ana Watoto

MARGARET, * MAMA MUMOJA WA HUKO AUSTRALIE ALIYEOLEWA NA BWANA ALIYE NA WATOTO: “Bibi wa zamani wa bwana yangu aliwaambia watoto wake wasisikie kila neno ninalowaambia hata jambo ndogo kama vile ‘Usisahau kusafisha meno yako.’” Margaret anajisikia kuwa ndoa yake ina matatizo kwa sababu ya njia hiyo yenye kuleta mugawanyiko.

Familia ambazo bibi ao bwana ana watoto wake zina uhusiano wa pekee na pia mugumu pamoja na wale walio inje ya familia zao. * Wazazi wengi katika familia hizo wanapaswa kuzungumuza na baba ao mama muzazi wa mutoto kuhusu mambo kama vile mutoto kutembelea watu, namna ya kumuazibu mutoto, na namna ya kumutegemeza kifeza. Marafiki na watu wa jamaa pia wanaweza kuwa na magumu ya kuzoea washiriki wapya wa familia. Fikiria namna mashauri ya Biblia yanavyoweza kusaidia familia ambazo bibi ao bwana ana watoto wake ili kupambana na matatizo hayo.

UHUSIANO WA  1: KUSHUGULIKA NA BABA AO MAMA MUZAZI WA MUTOTO

Judith, mama mumoja wa huko Namibie aliyeolewa na bwana aliye na watoto anasema hivi: “Mama muzazi wa watoto wa bwana yangu aliwaambia siku moja kwamba mimi nilikuwa tu bibi mupya ya baba yao na kwamba mutoto yeyote ambaye tutazaa hangekuwa ndugu yao. Maneno yake yaliniumiza kwa sababu ninawapenda watoto wa bwana yangu kama watoto wangu mwenyewe.”

Watu waliojifunza mambo ya familia wanasema kwamba uhusiano pamoja na mama ao baba muzazi wa mutoto linaweza kuwa jambo ngumu sana, na hata lenye kuleta mugawanyiko. Mara nyingi, ni mama muzazi wa watoto ao mama aliyekuta watoto ndiye aliye na magumu zaidi. Ni nini kinachoweza kusaidia?

Siri: Weka mipaka yenye kiasi. Ikiwa haumuruhusu muzazi wa mutoto ajiingize katika maisha ya mutoto wake, mutoto anaweza kujisikia vibaya moyoni. * Wazazi wa mutoto, wale ambao ‘walimuzaa,’ wana nafasi ya pekee katika maisha yake. (Methali 23:22, 25) Kwa upande mwengine, ikiwa unamuacha bibi ao bwana yako wa zamani ajiingize sana katika mambo ya familia yako, unaweza kumuvunja moyo ao kumukasirisha bibi ao bwana yako mupya. Jaribu kuwa na usawaziko, kwa kuweka mipaka yenye kiasi ili kulinda ndoa yako, huku ukiendelea kuwa na uhusiano muzuri pamoja na bibi ao bwana yako wa zamani.

MASHAURI KWA WAZAZI

  • Unapozungumuza na bibi ao bwana yako wa zamani, zungumuzia sana mambo yanayohusu watoto wako na usizungumuzie sana mambo mengine. Kwa mufano, unaweza kumuuliza kwa busara ikiwa inawezekana apange wakati wa kuzungumuza na watoto kwenye telefone muchana. Kwa kawaida ni vizuri kufanya hivyo kuliko kuwaita wakati wowote ao usiku sana.

  • Ikiwa haukupewa haki ya kulea watoto wako, labda unaweza kuwaita kwenye telefone, kuwaandikia barua, kuwaandikia ujumbe kwenye telefone, ao kwenye Internete ili undelee kujua habari zao. (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7) Kupitia video, wengine hata wanazungumuza nao wakiwa wenye kuonana uso kwa uso. Unaweza hata kujua mahitaji na magumu ya watoto wako na kuwatolea mashauri mazuri yanayoweza kuwasaidia, kuliko unavyowazia.

MASHAURI KWA MAMA ALIYEOLEWA NA BWANA ALIYE NA WATOTO

  • Umuonyeshe “huruma” mama muzazi wa watoto kwa kumuonyesha waziwazi kwamba haujaribu kuchukua nafasi yake. (1 Petro 3:8La Sainte Bible en Swahili de la R.D. Congo) Umuelezee kwa ukawaida hali ya watoto wakati munapokuwa pamoja na watoto, ukazie zaidi mambo mema ya watoto. (Methali 16:24) Umuombe mashauri, na umushukuru anapokutolea mashauri hayo.

  • Usifanye sana alama za kuwaonyesha watoto upendo wakati mama yao muzazi iko hapo. Beverly, mama mumoja huko États-Unis, aliyeolewa na bwana aliye na watoto, anasema hivi: “Watoto wadogo wa bwana yangu walipenda kuniita Mama. Nilikubaliana nao kama ni sawa kufanya hivyo nyumbani kwetu lakini hawangepaswa kufanya hivyo wakati Jane, mama yao muzazi, iko pale ao wakati watu wa jamaa yake wako pale. Tangu wakati huo, mimi na Jane tunasikilizana. Mwishowe, tulitumika pamoja ili kusaidia watoto kuhusu michezo na matembezi ya masomo.”

Unaweza hata kuwatolea watoto wako mashauri mazuri yanayoweza kuwasaidia, kuliko unavyowazia

MASHAURI ILI KUSAIDIA BABA AO MAMA MUZAZI WA MUTOTO NA MUZAZI MWENGINE

    Adabu na heshima vinatembea pamoja

  • Usiseme vibaya juu ya baba ao mama muzazi wa mutoto na juu ya muzazi mwengine wakati mutoto iko pale. Ni vyepesi kufanya hivyo, lakini jambo hilo linaweza kumuhuzunisha sana mutoto. Na hauwezi kujua namna gani ao wakati gani maneno yako yatajulikana. (Mhubiri 10:20) Ikiwa mutoto anasema kama baba ao mama muzazi ao yule muzazi mwengine alikusema vibaya, kazia akili namna mutoto anavyojisikia moyoni. Unaweza kusema jambo fulani kama vile: “Ninasikitika kwamba umesikia hivyo. Mama yako ananikasirikia, na wakati fulani watu wanasema vibaya ikiwa wanakasirika.”

  • Jaribu kuwa na kanuni na azabu zilezile kuelekea watoto wote. Ikiwa jambo hilo haliwezekane, fasiria tofauti bila kumukosea heshima muzazi mwengine. Fikiria hali inayofuata:

    Mama aliyeolewa na bwana aliye na watoto: Tim, tafazali, anika nguo yako ya kujipanguza.

    Tim: Kwa mama yangu, tunaziacha chini kisha mama anazianika.

    Mama aliyeolewa na bwana aliye na watoto (mwenye hasira): Ee, anawafundisha kuwa wavivu.

    Je, hilo ni jibu nzuri?

    Mama aliyeolewa na bwana aliye na watoto (kwa utulivu): Sawa. Hapa tunazianika sisi wenyewe.

  • Epuka kuwapatia watoto kazi wakati ambao wamepanga kuenda kupitisha na mama ao baba yao muzazi. (Mathayo 7:12) Ikiwa hauwezi kubadilisha programe, omba ruhusa kwa baba ao mama muzazi wa mutoto mbele ya kumupangia mutoto kazi.

JARIBU KUFANYA HIVI: Fuata hatua hizi wakati utakutana na bibi ao bwana wa zamani wa mwenzi wako:

  1. Umutazame usoni na kucheka kidogo. Epuka kufunga sura ao kuangalia pembeni.

  2. Umusalimie kwa kutaja jina lake. Kwa mufano, sema, “Jambo Jane.”

  3. Umuhusishe katika mazungumuzo ikiwa muko katika kikundi.

UHUSIANO WA 2: WATOTO WENYE KUKOMAA

Kitabu kimoja kinachozungumuzia mambo ya vita (Step Wars) kinataja maneno ya mwanamuke mumoja akinungunika juu ya namna bwana yake alivyo na tabia ya kuwaunga mukono watoto wake wenye kukomaa na kukataa kukubali kwamba wanamutendea vibaya. Anasema hivi: “Hilo linanikasirisha sana.” Unaweza kufanya nini ili kuzuia uhusiano wako pamoja na watoto wako wenye kukomaa usiharibu ndoa yako?

Siri: Ujitie pa nafasi ya watoto. Biblia inasema hivi: ‘Kila mumoja na aendelee kutafuta, si faida yake mwenyewe, bali ile ya yule mutu mwengine.’ (1 Wakorintho 10:24) Jaribu kumuelewa mutu mwengine na kujisikia kama anavyojisikia. Watoto wa bibi ao bwana yako wenye kukomaa wanaweza kuogopa kwamba muzazi wao hatawapenda tena. Ao wanaweza kufikiri kwamba wakimukaribisha muzazi mwengine, watakosa uaminifu kuelekea familia yao ya zamani. Na wazazi pia wanaweza kuogopa kwamba kuwachambua​-chambua watoto wao kutawafanya wasiwakaribie tena.

Kuliko kujaribu kukaza urafiki pamoja na watoto wa bibi ao bwana yako, acha ujilete wenyewe. Kwa kawaida, si jambo la hekima kujaribu kumukaza mutu fulani akupende kabisa. (Wimbo wa Sulemani 8:4) Kwa hiyo, ujikaze kutazamia mambo mazuri kuhusu uhusiano na watoto wa bibi ao bwana yako.

Usiseme kila jambo ambalo unawaza, hata ikiwa unatendewa vibaya. (Methali 29:11) Inapokuwa vigumu kabisa kuzuia ulimi wako, sali kama Mufalme Daudi wa Israeli. Alisali hivi: ‘Uweke mulinzi, Ee Yehova, kwa ajili ya kinywa changu; uweke mwangalizi juu ya mulango wa midomo yangu.’​—Zaburi 141:3.

Ikiwa unaamua kuishi katika nyumba ambamo watoto walikomalia, unaweza kushangaa kuona kwamba wanaendelea kuipenda sana nyumba hiyo. Usifanye mabadiliko mengi katika nyumba hiyo, zaidi sana katika vyumba vyao vya zamani. Unaweza pia kufikiria kuhamia katika nyumba mupya.

JARIBU KUFANYA HIVI: Ikiwa watoto wa bibi ao bwana yako wanaendelea kukukosea adabu ao heshima, umuambie bibi ao bwana yako namna unavyojisikia na usikilize kwa uangalifu mawazo yake. Usimukaze bibi ao bwana yako awarekebishe watoto. Kuliko kufanya hivyo, ujikaze kusikilizana na bibi ao bwana yako. ‘Munapofikiri kwa upatano’ juu ya hali fulani, munaweza kuungana mukono ili kufanya hali hiyo iwe nzuri.​—2 Wakorintho 13:11.

Ujikaze kuwaonyesha upendo watoto wote katika familia

UHUSIANO WA 3: WATU WENGINE WA JAMAA NA MARAFIKI

Marion, mama mumoja huko Kanada aliyeolewa na bwana aliye na watoto, anasema hivi: “Mara nyingi wazazi wangu walikuwa wanamupatia mutoto wangu zawadi lakini hawakuwa wanawapatia watoto wa bwana yangu. Tulijikaza kuwanunulia zawadi, lakini wakati fulani hatukuweza kufanya hivyo.”

Siri: Tia familia yako mupya pa nafasi ya kwanza. Uwaambie watu wa jamaa yako na marafiki wako juu ya daraka lako kuelekea familia yako mupya. (1 Timotheo 5:8) Hata ikiwa hauwezi kutazamia kwamba watu wote wa jamaa yako watapenda mara moja washiriki wa familia yako mupya, unaweza kuwaomba wawe wenye adabu na bila ubaguzi. Eleza namna watoto wanavyoweza kuumizwa moyoni ikiwa hawahangaikiwe na kutendewa vizuri katika njia zingine.

Jaribu kuacha wazazi wa bibi ao bwana yako wa kwanza wawe na nafasi katika maisha ya watoto wako. Susan, mama mumoja huko Angleterre anasema hivi: “Niliolewa tena miezi 18 kisha kifo cha bwana yangu wa kwanza, na ilikuwa vigumu kwa wazazi wake kukubali bwana yangu mupya. Mambo yaliendeka vizuri wakati tuliwahusisha zaidi katika maisha yetu, tuliomba watoto wawe wanawaita, na tuliwashukuru kwa utegemezo wao.”

JARIBU KUFANYA HIVI: Tafuta kujua rafiki ao mutu wa jamaa ambaye ni vigumu kabisa kwako kufanya uhusiano muzuri naye, na kisha uzungumuze na bibi ao bwana yako juu ya namna ya kufanya uhusiano pamoja naye uwe muzuri zaidi.

Uhusiano pamoja na watu walio inje ya familia yako mupya unaweza kuleta matatizo katika familia yako. Lakini ukitumia mashauri ya Biblia, familia yako inaweza kupata baraka hii ambayo Biblia inaahidi: “Nyumba hujengwa kwa hekima, na kwa utambuzi itasimamishwa imara.”​—Methali 24:3.

^ Majina fulani yamebadilishwa.

^ Ili kupata habari kuhusu namna ya kushugulika na matatizo mengine, soma habari yenye kichwa “Jinsi Familia za Kambo Zinavyoweza Kufanikiwa,” katika Amukeni! ya Mwezi wa 4, 2012 iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ Bila shaka, ikiwa bibi ao bwana yako wa zamani ni mwenye kuhatarisha ao kuumiza familia yako, unaweza kuhitaji kuweka mipaka kali kwa ajili ya usalama wa familia yako.

UJIULIZE . . .

  • Namna gani ninaweza kuwa na uhusiano muzuri pamoja na bibi ao bwana wa mwenzi wangu wa zamani?

  • Namna gani ninaweza kuwasaidia watu wa jamaa yangu na marafiki wasiharibu familia yetu bila kukusudia?