Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

BIBLIA INABADILISHA MAISHA YA WATU

“Walitaka Mimi Mwenyewe Nivumbue Mambo Biblia Inasema Kabisa”

“Walitaka Mimi Mwenyewe Nivumbue Mambo Biblia Inasema Kabisa”
  • ALIZALIWA MWAKA WA 1982

  • ALIZALIWA KATIKA INCHI YA RÉPUBLIQUE DOMINICAINE

  • ALIKUWA KATIKA DINI YA MORMON

MAISHA YANGU YA ZAMANI: Nilizaliwa katika muji wa Santo Domingo, huko République Dominicaine. Mimi ni mutoto wa mwisho katika familia ya watoto ine. Wazazi wangu walisoma sana na walitaka tukomalie kati ya watu wazuri na wenye kuaminika. Miaka ine mbele ya kuzaliwa kwangu, wazazi wangu walikutana na wamisionere wa kanisa la Mormon. Walivutiwa sana na namna vijana hao wamisionere walivyokuwa wamekata nywele vizuri na namna walivyokuwa wenye adabu. Kwa hiyo, wazazi wangu waliamua kwamba familia yetu ingekuwa kati ya familia za kwanza katika kisiwa chetu kujiunga na Kanisa la Yesu Kristo la Watakatifu wa Siku za Mwisho, ao Kanisa la Mormon.

 

Nilipoendelea kukomaa, nilipenda kujifurahisha pamoja na marafiki kwenye kanisa na niliheshimu mambo ambayo kanisa la Mormon lilifundisha juu ya maisha ya familia na kanuni za mwenendo muzuri. Nilijivunia kuwa mushiriki wa kanisa la Mormon na nilijiwekea muradi wa kuwa misionere.

Nilipokuwa na miaka 18, familia yetu ilihamia huko États-Unis ili niweze kusomea kwenye masomo ya juu mazuri zaidi. Karibu mwaka mumoja kisha hapo, shangazi yangu na bwana yake, ambao ni Mashahidi wa Yehova, walikuja kututembelea huko Florida. Walitualika kuhuzuria pamoja nao mukusanyiko uliotegemea Biblia. Niliguswa sana moyo kuona kwamba kila mutu pembeni yangu alikuwa anatafuta maandiko katika Biblia na kuandika mawazo makubwa. Kwa hiyo, nikaomba kalamu na karatasi na mimi pia nikaanza kuandika mawazo makubwa.

Kisha mukusanyiko huo, shangazi yangu na bwana yake walisema kwamba kwa sababu nilipenda kuwa misionere, wangeweza kunisaidia kujifunza jambo fulani juu ya Biblia. Nilifikiri hilo lilikuwa wazo nzuri, kwa sababu wakati huo, nilikuwa ninasoma sana Kitabu cha Mormon kuliko Biblia.

BIBLIA ILIBADILISHA MAISHA YANGU: Tulipokuwa tukizungumuza juu ya Biblia kwenye telefone, sikuzote shangazi yangu na bwana yake walinitia moyo kulinganisha mambo ninayoamini na mafundisho ya Biblia. Walitaka mimi mwenyewe nivumbue mambo ambayo Biblia inasema kabisa.

 

Nilikuwa nimekubali mambo mengi juu ya mafundisho ya kanisa la Mormon, lakini sikuwa na uhakika kabisa ikiwa mafundisho hayo yanapatana na Biblia. Shangazi yangu alinitumia gazeti la Amkeni! la tarehe 8 Mwezi wa 11, 1995, lililochapishwa na Mashahidi wa Yehova, ambalo lilikuwa na habari fulani juu ya mafundisho ya kanisa la Mormon. Nilishangaa kuona kwamba gazeti hilo lilizungumuzia mafundisho mengi ya kanisa la Mormon ambayo sikuwa ninajua. Hilo lilinichochea kutafuta habari zaidi kwenye adresi ya Internete ya kanisa la Mormon ili kuhakikisha ikiwa mambo yaliyozungumuziwa katika gazeti hilo la Amkeni! yalikuwa ya kweli. Niliona kwamba yalikuwa ya kweli kabisa, na mambo hayo yalihakikishwa zaidi nilipotembelea majumba ya ukumbusho ya kanisa la Mormon huko Utah.

Sikuzote niliamini kwamba Kitabu cha Mormon na Biblia vilipatana. Lakini nilipoanza kusoma Biblia kwa uangalifu zaidi, nilitambua mambo yenye kupingana kati ya mafundisho ya kanisa la Mormon na mambo ambayo Biblia inasema. Kwa mufano, katika andiko la Ezekieli 18:4, Biblia inasema kama nafsi inakufa. Lakini, katika Kitabu cha Mormon, andiko la Alma 42:9 linasema hivi: “Nafsi haiwezi kufa hata kidogo.”

Zaidi ya kuvurugika kwa sababu ya mafundisho ya kanisa la Mormon, nilivurugika pia kwa sababu ya mawazo ya kanisa hilo ya kutukuza taifa. Kwa mufano, Wamormon wanafundishwa kwamba bustani ya Edeni ilikuwa katika Jimbo la Jackson, huko Missouri, États-Unis. Na manabii wa kanisa la Mormon wanafundisha kwamba wakati “Ufalme wa Mungu utaanza kutawala, bendera safi ya États-Unis itapepea juu ya mulingoti wa bendera ya uhuru na haki za sawa-sawa.”

Kulingana na mafundisho hayo ya Wamormon, nilijiuliza ni nini kitazipata inchi zingine, kama vile inchi yangu ya kuzaliwa. Mangaribi moja nilitokeza wazo hilo nilipozungumuza kwenye telefone na kijana mumoja wa kanisa la Mormon ambaye alikuwa anazoezwa ili kuwa misionere. Nilimuuliza waziwazi ikiwa angekuwa tayari kupigana na Wamormon wenzake ikiwa inchi yao na inchi yake zinapigana vita. Nilishangaa aliposema kwamba atakuwa tayari kupigana vita! Niliendelea kuchunguza kwa uangalifu mafundisho ya kanisa langu la Mormon na pia kuzungumuza na viongozi wa kanisa hilo. Niliambiwa kama majibu kwa maulizo yangu ni mafumbo na kwamba siku moja yangejibiwa kwa kadiri nuru inavyozidi kuongezeka.

Kwa sababu nilivunjwa moyo sana na maelezo yao, nilijichunguza kwa uangalifu na pia nilichunguza nia iliyonichochea nitake kuwa misionere wa kanisa la Mormon. Nilitambua kwamba nilivutiwa na wazo la kuwa misionere ili tu kuwasaidia watu wengine. Cheo ambacho ningepata kwa sababu ya kuwa misionere kilinivutia pia. Ukweli ni kwamba, sikujua mambo mengi juu ya Mungu. Hata ikiwa nilisoma Biblia mara nyingi wakati uliopita, sikuiona kabisa kuwa ya maana. Sikujua kusudi la Mungu kwa ajili ya dunia na wanadamu.

FAIDA AMBAYO NIMEPATA: Kupitia funzo langu la Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova, nilijifunza mambo mengi, kwa mufano jina la Mungu ni nani, inakuwa namna gani mutu anapokufa, na Yesu ana daraka gani katika kutimizwa kwa kusudi la Mungu. Mwishowe, nilianza kuelewa kitabu hicho kizuri sana, na nilifurahia kuwaelezea wengine mambo ambayo nilikuwa nikijifunza. Sikuzote nilijua kwamba kuna Mungu, lakini sasa ningeweza kuzungumuza naye katika sala kama Rafiki ninayependa sana. Nilibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova tarehe 12 Mwezi wa 7, 2004, na miezi sita kisha hapo nikakuwa muhubiri wa wakati wote.

 

Kwa muda wa miaka mitano, nilitumika kwenye makao makubwa ya Mashahidi wa Yehova huko Brooklyn, New York. Nilifurahi sana kusaidia katika kazi ya kuchapisha Biblia na vichapo vingine vinavyoeleza Biblia ambavyo vinawafaidi mamilioni ya watu duniani pote, na ninaendelea kufurahi kuwasaidia watu wengine wajifunze juu ya Mungu.