Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

BIBLIA INABADILISHA MAISHA YA WATU

“Mwishowe, Nimepata Uhuru wa Kweli”

“Mwishowe, Nimepata Uhuru wa Kweli”
  • ALIZALIWA MWAKA WA 1981

  • ALIZALIWA KATIKA INCHI YA ÉTATS-UNIS

  • ALIKUWA MWANA MUPOTEVU

MAISHA YANGU YA ZAMANI: Nilizaliwa huko Moundsville, muji mutulivu ulio pembeni ya Mutoni Ohio kaskazini Mangaribi mwa Virginia, huko États-Unis. Nilikuwa mutoto wa pili katika familia ya watoto ine, watoto watatu ni wanaume, ndiyo maana familia yetu ilikuwa moto-moto. Wazazi wangu walikuwa wafanyakazi wenye bidii, waaminifu na walipenda watu. Hatukuwa na feza nyingi, lakini sikuzote tulipata vitu vyote tulivyohitaji. Kwa sababu wazazi wangu walikuwa Mashahidi wa Yehova, walifanya yote waliyoweza ili kutufundisha kanuni za Biblia tulipokuwa watoto wachanga.

 

Hata hivyo, wakati nilipokuwa kijana, moyo wangu ulikuwa tayari umeanza kukengeuka na nikaacha mambo niliyofundishwa tangu utoto. Nilianza kuwa na mashaka na kujiuliza ikiwa kwa kweli maisha yenye kuongozwa na kanuni za Biblia yanaweza kuleta furaha na kurizisha. Nilianza kufikiri kwamba ninaweza kuwa na furaha ikiwa tu nina uhuru wa kufanya kila kitu ninachotaka. Muda mufupi kisha hapo, nikaacha kuhuzuria mikutano ya kutaniko. Ndugu yangu mukubwa na dada yangu mudogo wakaasi pia kama mimi. Wazazi wangu walifanya yote waliyoweza ili kutusaidia, lakini hatukubadilika.

Muda mufupi baadaye, nilitambua kwamba ule niliowazia kuwa uhuru ungeniongoza katika mazoea yenye kuharibu. Siku moja nilipokuwa nikirudi nyumbani nikitoka kwenye masomo, rafiki yangu mumoja alinipa tumbaku na nikaikubali. Tangu siku hiyo na kuendelea, nilikubali mazoea mengine yenye kuharibu. Na kisha hapo, nikaanza kutumia sana dawa za kulewesha, kunywa pombe sana, na kuishi maisha mabaya sana. Kwa muda wa miaka mingi iliyofuata, hatua kwa hatua nilianza kutumia dawa za kulewesha zenye nguvu zaidi na nikakuwa mutumwa wa nyingi kati ya dawa hizo. Kwa kuwa sasa nilikuwa mutumwa wa dawa hizo, nilianza kuziuzisha ili kuendeleza maisha yangu mabaya.

Kwa kadiri nilivyojaribu kupuuza zamiri yangu, ndivyo iliendelea kunikumbusha kwamba namna yangu ya kuishi ilikuwa mbaya. Lakini, nilijisikia kuwa nilikuwa tayari nimeharibu maisha yangu na singeweza tena kubadilika. Ijapokuwa nilizungukwa na watu wengi kwenye karamu na maonyesho ya muziki, mara nyingi nilijisikia kuwa peke yangu na mwenye kuvunjika moyo. Nyakati nyingine, nilifikiria namna wazazi wangu walivyokuwa watu wazuri na wenye kujiendesha vizuri na nilijiuliza sababu gani nimeharibika.

BIBLIA ILIBADILISHA MAISHA YANGU: Hata ikiwa sikuwa tena na tumaini kama ninaweza kubadilika, watu wengine hawakupoteza tumaini. Katika mwaka wa 2000, wazazi wangu walinialika kuhuzuria mukusanyiko wa wilaya wa Mashahidi wa Yehova. Nilienda tu bila kutaka. Nilishangaa kuona kwamba ndugu yangu mukubwa na dada yangu mudogo waliokuwa waasi kama mimi walikuja pia.

 

Nilipokuwa kwenye mukusanyiko huo, nilikumbuka kwamba nilikuwa mahali hapo kwa ajili ya maonyesho ya muziki kulikuwa kumepita mwaka mumoja hivi. Tofauti niliyoona ilinigusa moyo sana. Kwenye maonyesho hayo ya muziki, mahali hapo palijaa uchafu na moshi wa tumbaku. Wengi kati ya watu waliokuwa kwenye maonyesho hayo hawakuwa wenye urafiki, na ujumbe wa muziki haukuwa wenye kujenga. Lakini kwenye mukusanyiko wa wilaya, nilikuwa nimezungukwa na watu wenye furaha kwelikweli, ambao walinikaribisha kwa shauku hata kama hatukuonana kwa muda wa miaka mingi. Mahali hapo palikuwa safi, na ujumbe uliotolewa ulikuwa wenye kutoa tumaini. Nilipoona namna kweli ya Biblia inavyosaidia watu maishani, nilijiuliza sababu gani niliacha kweli!​—Isaya 48:17, 18.

“Biblia ilinipatia nguvu ya kuacha kutumia dawa za kulewesha na kuziuzisha na pia ilinisaidia kuishi vizuri na watu wengine”

Kisha tu mukusanyiko huo, niliamua kurudi katika kutaniko la Kikristo. Ndugu yangu mukubwa na dada yangu mudogo, waliguswa pia moyo na mambo waliyosikia kwenye mukusanyiko huo, na wakaamua pia kurudi katika kutaniko. Sisi wote watatu tulikubali kujifunza Biblia.

Andiko la Biblia lililonigusa moyo sana ni Yakobo 4:8, ambalo linasema hivi: ‘Mukaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.’ Nilielewa kwamba ikiwa ninapenda kumukaribia Mungu, nilipaswa kufanya mabadiliko katika maisha yangu. Kati ya mabadiliko hayo, nilihitaji kuacha kuvuta tumbaku, kutumia dawa za kulewesha, na kunywa pombe sana.​—2 Wakorintho 7:1.

Niliachana na marafiki wangu wa zamani na nikatafuta marafiki wapya kati ya Mashahidi wa Yehova. Muzee wa kutaniko aliyenifundisha Biblia alinisaidia kabisa. Alikuwa ananiita kwa ukawaida kwenye telefone na kunitembelea ili kujua hali yangu. Leo, yeye ni mumoja wa marafiki wangu ambao ninapendana nao sana.

Katika mwaka wa 2001, nilijitoa kwa Mungu na kubatizwa katika maji, ndugu yangu mukubwa na dada yangu mudogo walibatizwa pia. Wazazi wangu na ndugu yangu aliyekuwa mwaminifu walifurahi sana familia yetu ilipoungana mwishowe katika ibada ya Yehova.

FAIDA AMBAYO NIMEPATA: Zamani nilikuwa ninafikiri kwamba kanuni za Biblia zinamunyima mutu uhuru, lakini sasa ninaziona kuwa ni ulinzi muzuri sana. Biblia ilinisaidia kuacha kutumia dawa za kulewesha na kuziuzisha na pia ilinisaidia kuishi vizuri na watu wengine.

 

Nina pendeleo la kuwa katika familia ya ndugu na dada wa ulimwenguni pote wanaomuabudu Yehova. Watu hao wanapendana kwelikweli, na wanamutumikia Mungu kwa umoja. (Yohana 13:34, 35) Baraka nyingine ya pekee ambayo nimepata ni bibi yangu Adrianne, ambaye ninamupenda sana na kumuona kuwa wa maana sana. Kumutumikia Muumbaji wetu pamoja kunatuletea furaha kubwa.

Kuliko kufuatilia maisha ya uchoyo, sasa mimi ni muhubiri wa wakati wote anayefundisha watu namna wao pia wanaweza kufaidika na Neno la Mungu. Kazi hiyo inaniletea furaha kubwa zaidi kuliko kazi nyingine yoyote. Ninaweza kusema kwa usadikisho mukubwa zaidi kwamba Biblia imebadilisha maisha yangu. Mwishowe, nimepata uhuru wa kweli.