Hamia kwenye habari

Mashahidi wa Yehova Ni Wangapi Ulimwenguni Pote?

Mashahidi wa Yehova Ni Wangapi Ulimwenguni Pote?

2023 Ripoti

Idadi ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote

8,816,562

Makutaniko

118,177

Nchi ambamo Mashahidi wa Yehova wanahubiri

239

2023 Jumla Kuu

2023 Ripoti ya Nchi na Eneo

Idadi ya Mashahidi wa Yehova inahesabiwa jinsi gani?

 Tunawahesabu wale tu wanaohubiri kila mwezi habari njema ya Ufalme wa Mungu kuwa ni Mashahidi wa Yehova. (Mathayo 24:14) Hesabu hiyo inatia ndani wale ambao wamebatizwa wakawa Mashahidi kutia ndani wale ambao, ingawa bado hawajabatizwa, wanastahili kushiriki katika kazi ya kuhubiri.

Je, ni lazima mtu atoe mchango ili awe mmoja wa Mashahidi wa Yehova?

 Hapana. Michango haina uhusiano na mtu kuhesabiwa kuwa Shahidi wala haifanyi mtu apewe mgawo au pendeleo lolote katika tengenezo letu. (Matendo 8:​18-20) Kwa kweli, karibu michango yote inatolewa bila mtoaji kujulikana. Kila Shahidi hutoa wakati, nguvu, na mali zake kwa ajili ya kazi yetu ya ulimwenguni pote kwa hiari na kulingana na hali zake.​—2 Wakorintho 9:7.

Mnajuaje idadi ya wanaohubiri kwa ukawaida?

 Kila mwezi, Mashahidi hutoa ripoti ya kazi yao ya kuhubiri kwenye makutaniko yao. Ripoti hiyo hutolewa kwa hiari.

 Ripoti za kutaniko hujumlishwa, na jumla hutumwa kwenye ofisi ya tawi ya kutaniko. Ofisi ya tawi hutuma jumla ya ripoti ya kila nchi au eneo lililo chini ya usimamizi wake kwenye makao makuu ya ulimwenguni pote.

 Mwishoni mwa kila mwaka wa utumishi, * kilele cha Mashahidi kwenye kila nchi katika mwaka huo hupatikana. Idadi hizo hujumlishwa ili kujua kuna Mashahidi wangapi ulimwenguni. Ripoti ya kila nchi, kutia ndani mambo yaliyoonwa ya kazi ya kuhubiri, hupatikana kwenye sehemu ya “Ulimwenguni Pote” katika tovuti yetu. Ripoti hizo hututia moyo, kama tu Wakristo wa mapema walivyotiwa moyo na ripoti walizopokea.?—Matendo 2:​41; 4:4; 15:3.

Je, mnawahesabu watu wanaoshirikiana na tengenezo lenu ambao hawahubiri?

 Ingawa hatuwahesabu katika idadi yetu ya Mashahidi, tunawakaribisha kwenye makutaniko yetu. Wengi wao huhudhuria Ukumbusho wa kila mwaka wa kifo cha Kristo, kwa hiyo makadirio ya idadi ya watu hao inaweza kutambuliwa kwa kutoa idadi ya Mashahidi kutoka kwenye hudhurio la mkutano huo. Katika mwaka wa 2023, hudhurio la Ukumbusho lilikuwa 20,461,767.

 Watu wengi ambao hawahudhurii mikutano yetu hufaidika kutokana na programu yetu ya kujifunza Biblia bila malipo. Katika mwaka wa 2023, tulijifunza Biblia kila mwezi na watu 7,281,212 hivi kwa wastani, idadi hiyo inatia ndani mafunzo yaliyofanywa na watu kadhaa kwa wakati mmoja.

Kwa nini idadi ya Mashahidi inayotolewa na serikali ni kubwa kuliko idadi mnazoonyesha?

 Mara nyingi idadi inayotolewa na serikali hupatikana kwa kuwauliza watu wanajitambulisha kuwa wa dini gani. Kwa mfano, Idara ya Sensa ya Marekani inasema kwamba uchunguzi wao “ulikusudia kujua ikiwa watu wanajitambulisha kuwa washiriki wa kikundi fulani cha kidini,” na ikaongeza kusema kwamba idadi zao “zinategemea maoni ya mtu, si mambo hakika.” Tofauti na hilo, sisi tunamhesabu mtu kuwa Shahidi wa Yehova ikiwa tu anawahubiria wengine na kutoa ripoti ya utendaji wake, si wale wanaojitambulisha tu kuwa Mashahidi.

^ Mwaka wa utumishi unahesabiwa kuanzia Septemba 1 hadi Agosti 31 ya mwaka unaofuata. Kwa mfano, mwaka wa utumishi wa 2015 ulianza Septemba 1, 2014 hadi Agosti 31, 2015.