Hamia kwenye habari

Je, Mashahidi wa Yehova Ni Dhehebu?

Je, Mashahidi wa Yehova Ni Dhehebu?

 La, Mashahidi wa Yehova si dhehebu. Sisi ni Wakristo wanaojitahidi kufuata mfano uliowekwa na Yesu Kristo na kuishi kupatana na mafundisho yake.

Dhehebu ni nini?

 Watu wanaelewa neno “dhehebu” katika njia mbalimbali. Hata hivyo, fikiria maoni mawili ambayo watu huwa nayo kuhusu dhehebu na kwa nini maoni hayo hayatuhusu sisi.

  •   Watu fulani hudhani kwamba dhehebu ni dini mpya au isiyo ya kawaida. Mashahidi wa Yehova hawajaanzisha dini mpya. Badala yake, ibada yetu inafuata kielelezo kilichowekwa na Wakristo wa karne ya kwanza, ambao mifano na mafundisho yao yameandikwa katika Biblia. (2 Timotheo 3:​16, 17) Tunaamini kwamba Maandiko Matakatifu ndiyo yanayopaswa kutumiwa kuamua ibada inayokubaliwa.

  •   Watu fulani hudhani kwamba dhehebu ni dini hatari inayoongozwa na mwanadamu. Mashahidi wa Yehova hawamtambui mtu yeyote kuwa kiongozi wao. Badala yake, tunafuata kiwango ambacho Yesu aliwawekea wafuasi wake aliposema: “Kiongozi wenu ni mmoja, Kristo.”​—Mathayo 23:10.

 Mashahidi wa Yehova si dhehebu hatari bali dini yao huwanufaisha wafuasi wake na watu wengine katika jamii. Kwa mfano, kupitia kazi yetu ya kuhubiri, tumewasaidia watu wengi kuacha mazoea yenye uraibu kama vile kutumia dawa za kulevya na kileo. Isitoshe, sisi huwa na madarasa ya kuwafunza watu kusoma na kuandika ulimwengu pote. Madarasa hayo yamewasaidia maelfu ya watu. Pia sisi hushiriki katika kutoa misaada wakati wa misiba. Tunajitahidi sana kuwa mfano mzuri kwa wengine, kama Yesu alivyowaamuru wafuasi wake wawe.​—Mathayo 5:​13-16.