Hamia kwenye habari

Je, Mashahidi wa Yehova Huvunja Familia au Huziimarisha?

Je, Mashahidi wa Yehova Huvunja Familia au Huziimarisha?

 Sisi Mashahidi wa Yehova tunajitahidi kuimarisha familia zetu na za majirani wetu pia. Tunamheshimu Mungu ambaye ndiye Mwanzilishi wa familia zote. (Mwanzo 2:​21-​24; Waefeso 3:​14, 15) Katika Biblia, anatufundisha kanuni ambazo zimewasaidia watu ulimwenguni pote kuwa na ndoa imara zenye furaha.

Jinsi Ambavyo Mashahidi wa Yehova Huimarisha Familia

 Tunajitahidi kadiri tuwezavyo kufuata mashauri ya Biblia, kwa kuwa yanatusaidia kuwa waume, wake, na wazazi bora. (Methali 31:10-​31; Waefeso 5:22–​6:4; 1 Timotheo 5:8) Hekima inayopatikana katika Biblia husaidia familia zenye watu walio katika dini tofauti. (1 Petro 3:​1, 2) Fikiria maelezo haya ya watu wasio Mashahidi ambao wenzi wao wa ndoa waliamua kuwa Mashahidi wa Yehova:

  •   “Miaka sita ya kwanza ya ndoa yetu ilijaa ugomvi na hasira. Hata hivyo, Ivete alipoamua kuwa Shahidi wa Yehova, alianza kunipenda na kunionyesha subira zaidi. Mabadiliko aliyofanya yaliokoa ndoa yetu.”​—Clauir, nchini Brazili.

  •   “Mume wangu Chansa alipoanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, nilimpinga kwa sababu nilifikiri wao huvunja familia za watu. Tangu wakati huo, nimejionea jinsi ambavyo Biblia imeisaidia ndoa yetu.”​—Agness, nchini Zambia.

 Katika huduma yetu, tunawaonyesha majirani wetu jinsi kutumia hekima inayopatikana katika Biblia kunavyoweza kuwasaidia

Je, kubadili dini kunasababisha mizozo katika ndoa?

 Kwa kweli, nyakati nyingine kubadili dini husababisha mizozo. Kwa mfano, ripoti iliyotolewa mwaka wa 1998 na kampuni ya kufanya utafiti inayoitwa Sofres ilisema kwamba ndoa 1 kati ya ndoa 20 ilikuwa na matatizo makubwa wakati mwenzi mmoja alipokuwa Shahidi.

 Yesu alitabiri kwamba wale wanaofuata mafundisho yake nyakati nyingine wangepingwa na watu wa familia zao. (Mathayo 10:32-​36) Mwanahistoria Will Durant aliandika kwamba chini ya Utawala wa Roma, “Ukristo ulishutumiwa kwamba unavunja familia za watu,” * na baadhi ya Mashahidi wa Yehova wanakabili hali kama hiyo leo. Hata hivyo, je, hilo linamaanisha kwamba Shahidi ndiye anayesababisha matatizo hayo?

Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu

 Ilipokuwa ikitoa uamuzi kuhusu kesi ambayo Mashahidi wa Yehova walishtakiwa kwa kuvunja familia za watu, Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu ilisema kwamba mara nyingi watu wa familia ambao si Mashahidi ndio husababisha kutoelewana kwa kukataa “kukubali na kuheshimu uhuru wa mtu wa ukoo wa kujichagulia dini.” Mahakama hiyo iliongezea hivi: “Hii ni hali ya kawaida katika ndoa zote ambazo wenzi wana dini tofauti, na si kwa Mashahidi peke yao.” * Hata hivyo, wanapobaguliwa kwa sababu ya imani yao, Mashahidi wa Yehova hufuata shauri hili la Biblia: “Msimlipe yeyote uovu kwa uovu. . . . Ikiwezekana, kwa kadiri inavyowategemea ninyi, iweni wenye kufanya amani na watu wote.”​—Waroma 12:17, 18.

Kwa nini Mashahidi wa Yehova huamini kwamba wanapaswa kuoa au kuolewa na watu wa dini yao tu?

 Mashahidi hutii agizo la Biblia la kuoa au kuolewa “katika Bwana tu,” yaani, kuoa au kuolewa na mtu mwenye imani sawa na yako. (1 Wakorintho 7:​39) Hiyo ni amri ya Biblia na inafaa. Kwa mfano, makala moja ya mwaka wa 2010 katika jarida liitwalo Journal of Marriage and Family ilisema kwamba “wenzi wa ndoa walio katika dini moja, wanaoabudu pamoja na kuamini mambo yaleyale” wana uhusiano bora zaidi. *

 Hata hivyo, Mashahidi hawachochei waabudu wenzao kutengana na mwenzi wa ndoa asiye Shahidi. Biblia inasema hivi: “Ikiwa ndugu yeyote ana mke asiyeamini, na bado mke huyo anakubali kukaa pamoja naye, basi asimwache; na mwanamke aliye na mume asiyeamini, na bado mume huyo anakubali kukaa pamoja naye, basi asimwache mume wake.” (1 Wakorintho 7:​12, 13) Mashahidi wa Yehova hutii amri hiyo.

^ Tazama kitabu Caesar and Christ, ukurasa wa 647.

^ Tazama uamuzi uliotolewa katika kesi ya Mashahidi wa Yehova wa Urusi na Wengine dhidi ya Serikali ya Urusi ukurasa wa 26-​27, fungu la 111.

^ Tazama jarida Journal of Marriage and Family, Buku la 72, Namba 4, (Agosti 2010), ukurasa wa 963.