Hamia kwenye habari

Waliendelea Kuhubiri Licha ya Janga

Waliendelea Kuhubiri Licha ya Janga

 Tangu janga la corona (COVID-19) lilipoanza, ndugu na dada zetu wamebadili njia zao za kushiriki na wengine ujumbe unaofariji wa Biblia. Badala ya kuhubiri hadharani au kutembelea watu nyumbani, wamekuwa wakiwahubiria hasa kwa kutumia simu na kuandika barua. a Watu wengi walifurahi kufikiwa kwa njia hii, na ni wazi kwamba Yehova amebariki jitihada za wahubiri hao. (Methali 16:3, 4) Ifuatayo ni mifano kadhaa ya mambo yaliyoonwa katika kisiwa kimoja.

 Kabla ya janga hili kuanza, Helen alikuwa akimtembelea mwanamke mmoja na alimwalika ajifunze Biblia pamoja naye. Kila mara, mwanamke huyo alikataa kujifunza. Lakini, siku moja kabla ya kutolewa sheria ya kukataza watu kutoka nyumbani kwa sababu ya corona, Helen alimpa Biblia na kitabu Biblia Inatufundisha Nini? Baada ya muda, Helen alimwalika mwanamke huyo tena kujifunza Biblia kwa njia ya simu na awamu hiyo, alikubali. Alifurahia sana mazungumzo yao, na akamwomba Helen wajifunze kila siku! Mwanamke huyo alianza kuhudhuria mikutano kwa ukawaida kwa njia ya simu. Na jambo la kuvutia hata zaidi ni kwamba, anatumia mafundisho ya Biblia maishani mwake na pia kuwaeleza watu wengine mambo anayojifunza.

 Mashahidi katika kutaniko fulani, walipokuwa katika huduma waliwaandikia barua polisi ili kuwashukuru kwa kazi yao yenye thamani kubwa. Polisi hao walishangaa kupata barua hizo. Ofisa mmoja alimwambia mzee wa kutaniko anayeitwa Jefferson hivi: “Nilifikiri kwamba Mashahidi wa Yehova wanachukia polisi.” Jefferson alimwelezea kwamba hilo si kweli. Maofisa hao walivutiwa sana na ujumbe mzuri wa barua hizo hivi kwamba walizibandika kwenye mwingilio wa jengo lao. Ofisa mwingine alisema hivi: “Huenda hili litawasaidia watu wengine watuone kwa njia nzuri pia.”

 Edna na Ednalyn ni mapainia wa kawaida. b Kwa kuwa hawana Intaneti nyumbani kwao, hawakuweza kujiunga na mikutano ya kutaniko lao mtandaoni. Hivyo, walimpigia simu jirani yao ambaye si Shahidi na kumwomba ikiwa wanaweza kutumia Wi-Fi yake kisha wachangie pesa za kulipia gharama. Kwa fadhili, mwanamke huyo aliwaruhusu kutumia Intaneti yake bila malipo. Edna na Ednalyn walimwalika ahudhurie mikutano, na alifanya hivyo. Sasa, jirani huyo, mtoto wake mmoja, na wajukuu wake wawili wanajifunza Biblia na Mashahidi na kuhudhuria mikutano kwa ukawaida.

 Akina ndugu na dada waliwaalika jirani zao, wafanyakazi wenzao, na watu wengine wasikilize hotuba ya pekee ambayo ingetolewa kupitia mtandao. Mwanzoni, Ellaine, anayefanya kazi kwenye hospitali katika eneo hilo, alisita kuwaalika wafanyakazi wenzake. Hata hivyo, aliwaalika madaktari kupitia ujumbe mfupi wa simu. Ellaine aliogopa hasa kuwaalika madaktari wawili ambao ni wenzi wa ndoa. Baada ya kufikiria kuhusu jambo hilo na kusali, aliwatumia mwaliko. Mwanamke huyo alimwuliza: “Kwa hiyo, unataka mimi niwe Shahidi wa Yehova?” Ellaine alimwambia kwamba watu wote wanaweza kuhudhuria, si Mashahidi wa Yehova tu. Siku iliyofuata, Ellaine, alishangaa wenzi hao walipojiunga kwenye mkutano mapema. Anasema hivi: “Kabla ya mkutano kuisha, nilipata ujumbe huu kutoka kwa mwanamke huyo: ‘Hii ni mara yangu ya kwanza kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova. Ulikuwa mzuri. Nimefurahia. Asante kwa kunialika.’”

Ellaine

 Ellaine aliwaalika madaktari 20 wahudhurie mkutano na alifurahi kujua kwamba madaktari 16 walihudhuria. Alinukuu maneno ya mtume Paulo na kusema hivi: “Ninafurahi kwamba ‘nilijipa ujasiri’ wa kushiriki ‘habari njema ya Mungu’ pamoja na wafanyakazi wenzangu.”​—1 Wathesalonike 2:2.

 Kipindi hiki cha janga kimekuwa kigumu kwa kila mtu. Ndugu na dada zetu katika kisiwa hiki na kwingineko wamefaulu kudumisha shangwe yao na mtazamo wao mzuri kwa kuendelea kufanya yote wawezayo kuwafariji na kuwasaidia wengine.​—Matendo 20:35.

a Mashahidi wa Yehova wanafanya utumishi wao kwa kuzingatia sheria za kulinda taarifa.

b Mapainia ni wahubiri wa wakati wote wa Kikristo.