Hamia kwenye habari

Matokeo Aliyopata Yalimshangaza

Matokeo Aliyopata Yalimshangaza

 Desicar alitamani sana kupanua utumishi wake na kuwa painia wa kawaida. Yeye ni mama ambaye hana mwenzi. Anaishi nchini Venezuela ambako kuna matatizo mengi ya kiuchumi. Hata hivyo, alikuwa ameazimia kuanza upainia naye alifanikiwa. Alifurahi sana alipotimiza lengo lake lakini janga la COVID-19 likaanza.

 Mwanzoni mwa janga, ilikuwa vigumu kwa Desicar kutumia njia mpya za kuhubiri ambazo tulikuwa tukitumia wakati huo. Ilikuwa vigumu kwake kuandika barua. Isitoshe, hangeweza kutumia video kwenye mtandao kwa sababu huduma ya Intaneti ni ghali sana katika eneo analoishi. Desicar anasema: “Nilivunjika moyo. Nisingeweza kuhubiri kama nilivyofanya zamani. Nilihisi sikuwa painia wa kawaida mwenye matokeo.”

 Kisha, Januari 2021, ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova nchini Venezuela ilianzisha kampeni ya pekee ya kuhubiri. Mipango ilifanywa ili vituo 60 vya redio na vituo 7 vya televisheni vipeperushe hotuba za watu wote kila mwisho juma. Mwezi huo kulikuwa na miisho juma mitano. Mashahidi walitiwa moyo wawaalike watu watazame au kusikiliza hotuba hizo. Pia, ofisi ya tawi iliandaa maswali na maandiko yaliyohusiana na kila hotuba, na ndugu na dada zetu wakayatia ndani ya barua walizoandika na pia katika mazungumzo ya simu. Kwa kuongezea, ofisi ya tawi iliwatia moyo akina ndugu na dada kutumia njia mpya ya kuhubiri, yaani, kutuma ujumbe wa simu. Ndugu na dada wengi nchini Venezuela hawakuwa wametumia njia hiyo hapo awali.

 Desicar alitazamia kwa hamu kushiriki katika kampeni hiyo. Ingawa ilikuwa mara yake ya kwanza kuhubiri kwa kuandika ujumbe wa simu, aliamua kujaribu. Hata hivyo, alihitaji msaada. Desicar amesema, “Mimi sijui sana mambo ya teknolojia.” Kwa hiyo, alimwomba binti yake amfundishe na punde si punde, Desicar alikuwa tayari kushiriki katika kampeni hiyo.

Desicar

 Desicar aliwatumia ujumbe watu wengi aliowafahamu na akawaalika wasikilize hotuba hizo zilizorekodiwa mapema. Matokeo aliyopata yalimshangaza. Wengi kati ya watu aliowaalika walisikiliza hotuba hizo na hata walimwuliza maswali. Wale ambao hawakufaulu walimwuliza Desicar mambo yaliyokuwa yamezungumziwa kwenye hotuba hizo. Desicar anasema: “Nilitumia mambo makuu ambayo nilikuwa nimeandika kuwafafanulia hotuba hizo. Kabla ya hapo sikuwa nimeripoti ziara 5 za kurudia kwa mwezi, lakini kufikia mwisho wa kampeni hiyo, nilikuwa na ziara 112 za kurudia!” a

 Desicar alimwalika dada yake ambaye si Shahidi na ambaye ni jirani yake asikilize hotuba hizo kwenye redio. Desicar anasema: “Nilishangaa sana dada yangu alipokubali mwaliko huo. Kila Jumapili, nilienda kwake saa mbili asubuhi na tukasikiliza hotuba hizo pamoja. Aliniuliza maswali mengi wakati wa programu na hata baadaye.” Pia, dada yake alihudhuria ukumbusho wa kifo cha Yesu kupitia Intaneti na hata alimruhusu Desicar atumie Intaneti yake katika huduma.

 Desicar anasema: “Ninamshukuru sana Yehova, na pia ninawashukuru wazee wa kutaniko letu kwa kunitia moyo. Walinisaidia kupata tena shangwe katika huduma.” (Yeremia 15:16) Desicar anaendelea kufanya upainia na kuwafundisha watu aliowapata kupitia jumbe alizotuma.

a Mashahidi wa Yehova huhubiri kwa kuzingatia sheria za kulinda taarifa.