Hamia kwenye habari

“Tendo Moja Dogo la Unyoofu”

“Tendo Moja Dogo la Unyoofu”

Danielle, Shahidi wa Yehova nchini Afrika Kusini, alipata mfuko ambao mteja alisahau mkahawani. Ndani ya mfuko huo kulikuwa na pochi yenye pesa na kadi za benki. Kwa kuwa Danielle alitaka sana kurudisha mfuko huo, alitafuta anwani au namba ya simu katika pochi hiyo lakini akapata tu jina la mwanamume fulani. Alijaribu kuwasiliana na mwanamume huyo kupitia benki yake lakini hakufanikiwa. Bila kukata tamaa, alipiga simu kwenye ofisi ya daktari ambaye namba yake ya simu ilikuwa kwenye risiti aliyopata katika mfuko huo. Karani aliyejibu simu alikubali kumpa mwanamume huyo namba ya Danielle.

Mwanamume huyo alishangaa kupokea simu kutoka kwenye ofisi ya daktari, ikimjulisha kwamba Danielle alikuwa amepata mfuko wake na alitaka kumrudishia. Alipoenda kuuchukua, alikutana na Danielle na baba yake. Walitumia nafasi hiyo kumweleza sababu iliyowafanya watie jitihada hizo zote ili kumpata. Walimweleza kwamba kwa kuwa wao ni Mashahidi wa Yehova, wanajaribu kuishi kupatana na kanuni za Biblia. Ndiyo sababu wao hujaribu kuwa wanyoofu sikuzote.—Waebrania 13:18.

Saa kadhaa baadaye, mwanamume huyo alimtumia Danielle na baba yake ujumbe, akiwashukuru tena kwa kurudisha mfuko na pochi yake. Aliandika hivi: “Ninathamini sana jitihada kubwa mliyofanya kunitafuta. Nilifurahi sana kukutana nawe na familia yako nami nitawakumbuka kwa uchangamfu na urafiki wenu. Ili kuonyesha shukrani, ningependa kutoa mchango. Najua kwamba mnajidhabihu ili kumtumikia Mungu. Matendo yenu ni wonyesho wa jinsi mlivyo, kama inavyoonekana kutokana na unyoofu na uaminifu ambao Danielle alionyesha. Kwa mara nyingine, nashukuru sana na Mungu abariki huduma yenu.”

Miezi kadhaa baadaye, baba ya Danielle alikutana tena na mwanamume huyo, ambaye alimsimulia kwamba muda mfupi uliopita alikuwa amepata pochi iliyopotea. Alipokuwa dukani, aliona pochi ardhini. Alipomkuta mwanamke aliyepoteza pochi hiyo na kumrudishia, alimweleza sababu iliyomchochea kuirudisha. Muda mfupi kabla ya hapo hata yeye alikuwa ametendewa kwa unyoofu. Alisema hivi: “Tendo moja dogo la unyoofu na fadhili linaongoza kwenye tendo lingine, na hivyo kuboresha maisha ya kila mtu katika jamii.