Hamia kwenye habari

“Nilikuwa Nikisubiri Mnipigie Simu”

“Nilikuwa Nikisubiri Mnipigie Simu”

 Ed na mke wake, Jennie, walijaribu mahubiri ya simu kwa mara ya kwanza mwaka wa 2010. a Jennie anasema hivi: “Sikufurahia mahubiri hayo hata kidogo. Nilimwambia mume wangu, ‘Sitafanya mahubiri hayo tena!’” Ed pia alihisi hivyo. Alisema hivi: “Sipendi kupokea simu kutoka kwa watu wanaouza bidhaa kupitia simu, kwa hiyo sikuwazia jinsi ninavyoweza kuhubiri kupitia simu.”

 Hata hivyo, janga la COVID-19 lilipoanza, Mashahidi wa Yehova waliacha kuhubiri nyumba kwa nyumba. Ili kutii amri ya Yesu ya kutangaza habari njema, waliendelea na huduma yao, hasa kwa kuandika barua na kuhubiri kupitia simu. (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Wakati huohuo, mikutano ya Kikristo, kutia ndani mikutano ya utumishi wa shambani, ilifanywa kupitia mtandao. Ed alipohudhuria mkutano mmoja wa utumishi, alijipa ujasiri wa kuhubiri kupitia simu kwa mara nyingine. Alihisije kabla ya kupiga simu yake ya kwanza? Anasema hivi: “Nilikuwa na wasiwasi mwingi hivi kwamba nilisali kuomba msaada! Kisha nikapiga simu. Na Tyrone akapokea.” b

 Tyrone na mke wake, Edith, wanaishi katika maeneo ya kijijini ya Kentucky, Marekani. Tyrone ana umri wa miaka 83 na hawezi kuona vizuri. Hata hivyo, alikubali kujifunza Biblia na Ed. Alisoma chapisho la funzo kwa kutumia kioo cha kuongeza ukubwa wa maandishi na akaanza kujifunza Biblia kwa ukawaida na Ed kupitia simu.

 Mwezi mmoja hivi baadaye, Tyrone na Edith walianza kuhudhuria mikutano iliyofanywa na kutaniko la eneo lao. Hata hivyo, kwa kuwa hawana Intaneti, waliunganishwa kupitia simu. Ni nini kilichochochea upendezi wa Edith?

 Ed na Jennie walipokuwa wakijifunza na Tyrone, walimsikia Edith akimsaidia Tyrone kupata majibu na pia kufungua maandiko katika Biblia yao. Lakini hakushiriki katika funzo hilo. Jennie anasema hivi: “Mimi na Ed tulihisi kwamba sauti yake ilikuwa na huzuni lakini hatukujua sababu.”

Ed na Jennie wakihubiri kupitia simu

 Siku moja, Jennie aliamua kumhusisha Edith katika mazungumzo. Kwa hiyo, hali ziliporuhusu alimwomba Ed simu. Alisema hivi: “Tyrone ninasikia sauti ya mke wako kwa mbali, ningependa kumwomba atusomee andiko au atoe maelezo.”

 Baada ya ukimya wa muda mfupi, Edith akazungumza kwa sauti nyororo akasema, “Nimekuwa nikitaka kuzungumza nanyi.” Kisha akasema: “Mimi ni Shahidi wa Yehova. Nimekuwa asiyetenda kwa miaka 40.”

 Jennie alishangaa na kusema hivi kwa msisimuko: “Wewe ni dada yangu!” Na wote wawili wakaanza kulia.

 Muda mfupi baada ya hapo, Ed alimpa Edith nakala ya broshua Mrudie Yehova. Katika majuma yaliyofuata, Ed na Jennie walitambua kwamba Edith alianza kuchangamka. Ed anasema: “Mwanzoni, sauti yake ilisikika kuwa yenye huzuni nyingi. Lakini sasa ina shangwe.” Edith alifanya maendeleo ya kiroho na sasa kwa mara nyingine tena yeye ni mhubiri mwenye shangwe wa habari njema. Mume wake alibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova mnamo Julai 2022.

 Ed anapofikiria jinsi alivyohisi mwanzoni kuhusu mahubiri ya simu, anakumbuka mazungumzo fulani kati yake na Tyrone. Baada ya Ed kumsomea Yohana 6:44 na kumweleza kwamba Yehova anawavuta watu kwenye kweli, Tyrone alikubali na kusema hivi: “Nilikuwa nikisubiri mnipigie simu.” Jennie pia anafurahi kwamba yeye na mume wake walijipa ujasiri wa kuhubiri kupitia simu. Anasema hivi: “Yehova hubariki jitihada zetu tunapofanya mambo ambayo ni magumu kwetu.”

a Mashahidi wa Yehova hufuata sheria zinazohusu kulinda taarifa za kibinafsi za mtu wanaposhiriki huduma yao

b Baadhi ya majina yamebadilishwa.