Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 SIRI YA FURAHA YA FAMILIA

Kushughulika na Familia ya Kambo

Kushughulika na Familia ya Kambo

MARGARET, * MAMA WA KAMBO NCHINI AUSTRALIA: “Mke wa zamani wa mume wangu aliwaambia watoto wake wasisikilize chochote ninachowaambia—hata jambo rahisi kama ‘Kumbukeni kupiga mswaki.’” Margaret anahisi ndoa yake inakosa furaha kwa sababu ya mgawanyiko huo.

Mara nyingi familia za kambo hukabili matatizo ya pekee kuhusiana na wale walio nje ya familia zao. * Wazazi wengi wa kambo wanahitaji kuwasiliana na mzazi halisi wa mtoto, hasa inapohusu kumtembelea mtoto, kumtia nidhamu, na mahitaji ya pesa. Pia, inaweza kuwa vigumu kwa watu wa ukoo na marafiki kuzoeana na washiriki wapya wa familia. Ona jinsi ushauri wa Biblia unavyoweza kusaidia familia za kambo kukabiliana na matatizo hayo.

UHUSIANO WA KWANZA: MZAZI HALISI WA MTOTO

Mama mmoja wa kambo nchini Namibia aitwaye Judith anasema: “Mama ya watoto wangu wa kambo aliwaambia kwamba nilikuwa mke mpya wa baba yao, na watoto wangu wasingekuwa ndugu zao. Maneno yake yaliniumiza kwa sababu nawapenda watoto wangu wa kambo kama tu watoto wangu mwenyewe.”

 Wataalamu wanasema kwamba uhusiano kati ya mzazi wa kambo na mzazi halisi unaweza kuwa na matatizo na hata kusababisha mgawanyiko. Mara nyingi, mama wa kambo na mama halisi hushindwa kuelewana. Ni nini kinachoweza kusaidia?

Siri ya kufanikiwa: Weka mipaka. Ukijaribu kumpuuza kabisa yule mzazi mwingine, huenda mtoto wako akateseka kihisia. * Wazazi halisi wa mtoto, yaani, ‘waliomzaa’ wana sehemu muhimu katika maisha yake. (Methali 23:22, 25) Kwa upande mwingine, ukimruhusu mwenzi wako wa zamani aingilie sana familia yako, hilo linaweza kumkasirisha mwezi wako wa sasa. Jitahidi kuwa na usawaziko, weka mipaka inayofaa ili kulinda ndoa yako, wakati huohuo endelea kushirikiana na mzazi wa mtoto kwa kiwango kinachofaa.

MADOKEZO KWA WAZAZI

  • Unapozungumza na mwenzi wako wa zamani, zungumzeni tu kuhusu watoto na uepuke kuzungumzia sana mambo mengine. Pia, kwa busara unaweza kumwomba apange wakati hususa wa kupiga simu mchana. Hilo ni afadhali kuliko kupiga simu wakati wowote au usiku wa manane.

  • Ikiwa huna haki ya kumtunza mtoto, labda unaweza kupiga simu, kuandika barua, kutuma ujumbe mfupi, au barua pepe ili kudumisha mawasiliano ya kawaida. (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7) Wazazi fulani huzungumza kwa kutumia video iliyo kwenye kompyuta iliyounganishwa na Intaneti. Kufanya hivyo kutakusaidia kumfahamu mtoto vizuri zaidi—na kukuwezesha kutoa ushauri—kwa kiwango kikubwa.

MADOKEZO KWA MAMA WA KAMBO

  • Mwonyeshe “hisia-mwenzi” mama halisi kwa kumhakikishia kwamba yeye ni muhimu katika malezi ya watoto. (1 Petro 3:8) Mjulishe kwa ukawaida hali ya watoto, hasa ukikazia mambo mazuri. (Methali 16:24) Mwombe ushauri, na usisahau kumshukuru.

  • Epuka kuwaonyesha watoto upendo sana mbele ya mama halisi. Beverly, mama wa kambo nchini Marekani, anasema: “Watoto wangu wa kambo walitaka kuniita Mama. Niliwaambia wanaweza kufanya hivyo tukiwa nyumbani lakini hawangeniita Mama wanapokuwa pamoja na mama yao Jane, au watu wake wa ukoo. Baada ya hapo mimi na Jane tukawa na uhusiano mzuri. Kwa kweli, tulisaidiana kulea na kuwatunza watoto.”

Unaweza kuwa na uvutano mkubwa juu ya mtoto wako kuliko unavyodhani

MADOKEZO YA KUWASAIDIA WAZAZI HALISI NA WA KAMBO

    Fadhili na heshima husaidia kudumisha amani

  • Usiseme vibaya kuhusu mzazi halisi au wa kambo ambaye hayupo ikiwa mtoto yuko karibu. Ni rahisi kusema mambo yasiyofaa, lakini hilo linaweza kumvunja moyo mtoto. Pia, hujui jinsi maneno yako yanavyoweza kuwa na madhara baadaye. (Mhubiri 10:20) Ikiwa mtoto anasema kwamba mzazi mwingine amesema vibaya kukuhusu, zingatia hisia za mtoto. Unaweza kusema hivi: “Pole kwa kusikia jambo  hilo. Mama yako ana hasira na mimi, na wakati mwingine watu wanapokasirika wanasema vibaya.”

  • Jaribuni kuwa na kanuni zinazolingana katika familia zote mbili. Ikiwa hilo haliwezekani, eleza kwa fadhili kwa nini kuna tofauti bila kumvunjia heshima mzazi mwingine. Fikiria hali ifuatayo:

    Mama wa kambo: Tim, anika taulo yako.

    Tim: Nyumbani kwa mama huwa tunaacha taulo chini na mama ndiye anayeanika.

    Mama wa kambo (kwa ukali): Sawa, anakufundisha kuwa mzembe.

    Huenda ingefaa kujibu hivi:

    Mama wa kambo (kwa upole): Ehee, sawa. Hapa kila mtu huwa anaanika taulo yake mwenyewe.

  • Epuka kuwapa watoto kazi wakati ambapo wanapaswa kuwa na mzazi mwingine. (Mathayo 7:12) Ikiwa huwezi kubadili ratiba hiyo, kwanza mwombe ruhusa mzazi mwingine kabla ya kuwahusisha watoto.

JARIBU KUFANYA HIVI: Fuata madokezo haya utakapokutana na mwenzi wa zamani wa mke au mume wako:

  1. Mtazame na utabasamu. Epuka kuhema-hema, kununa, au kutazama kando.

  2. Msalimu kwa kumtaja jina. Kwa mfano, unaweza kusema, “Habari, Jane.”

  3. Ikiwa mko katika kikundi mhusishe katika mazungumzo.

UHUSIANO WA PILI: WATOTO AMBAO NI WATU WAZIMA

Kitabu Step Wars kilimnukuu mwanamke aliyelalamika kuhusu mume wake ambaye aliwatetea watoto wake ambao ni watu wazima bila kujali kwamba walimtendea vibaya. “Mimi hukasirika haraka,” mwanamke huyo anasema. Unawezaje kuzuia uhusiano wako na watoto ambao ni watu wazima usiharibu ndoa yako?

Siri ya kufanikiwa: Onyesha upendezi. Biblia inasema: “Kila mmoja na aendelee kutafuta, si faida yake mwenyewe, bali ile ya yule mtu mwingine.” (1 Wakorintho 10:24) Jaribu kuelewa hisia za mwingine. Huenda watoto ambao ni watu wazima wakaogopa kupoteza upendo wa mzazi wao. Au huenda wakafikiri kwamba kumkubali mzazi wa kambo ni kukosa ushikamanifu kwa familia yao. Wakati uleule, huenda wazazi wakaogopa kuwakosoa watoto wao wakidhani watachukiwa kwa kufanya hivyo.

Badala ya kulazimisha urafiki, acha uhusiano kati yako na watoto wa kambo ukue wenyewe. Kwa kawaida, si jambo la busara kumlazimisha mtu akupende. (Wimbo wa Sulemani 8:4) Kwa hiyo, uwe na matarajio halisi na yenye usawaziko unapositawisha uhusiano pamoja na watoto wa kambo.

Usiseme kila kitu unachohisi au kufikiri, hata unapotendewa isivyofaa. (Methali 29:11) Unaposhindwa kudhibiti usemi wako, unaweza kusali kama Mfalme Daudi wa Israeli: “Uweke mlinzi, Ee Yehova, kwa ajili ya kinywa changu;uweke mwangalizi juu ya mlango wa midomo yangu.”—Zaburi. 141:3

Ukiamua kuishi katika nyumba ambayo watoto walilelewa, huenda utashangaa kuona jinsi wanavyopenda nyumba hiyo. Hivyo, usifanye mabadiliko mengi, hasa katika vyumba vyao vya zamani. Huenda ikafaa kuhamia katika nyumba mpya.

 JARIBU KUFANYA HIVI: Ikiwa watoto wa kambo ambao ni watu wazima hawakuheshimu, mweleze mwenzi wako kuhusu hali hiyo na usikilize kwa makini maoni yake. Usimlazimishe mwenzi wako kuwatia nidhamu watoto. Badala yake, jitahidini kuelewana. Mnapoanza “kufikiri kwa upatano” kuhusu hali hiyo, itakuwa rahisi kufanya marekebisho.—2 Wakorintho 13:11.

Jitahidi kuwapenda watoto wote katika familia

UHUSIANO WA TATU: WATU WA UKOO NA MARAFIKI

Marion, mama wa kambo nchini Kanada, anasema: “Mara kwa mara wazazi wangu walimpa zawadi mwanangu lakini hawakuwapa watoto wa mume wangu. Tulijitahidi kuwanunulia wao pia lakini wakati mwingine hatukuwa na pesa.”

Siri ya kufanikiwa: Tanguliza familia yako mpya. Waambie watu wa ukoo na marafiki kuhusu wajibu wako kuelekea familia mpya. (1 Timotheo 5:8) Ingawa hutarajii kwamba watu wa ukoo na marafiki watapenda familia yako mpya mara moja, waombe waonyeshe heshima. Waeleze jinsi watoto watakavyoumia kihisia ikiwa hawataonyeshwa upendo na matendo mengine ya fadhili.

Waruhusu wazazi wa mwenzi wako wa zamani wawe na uhusiano na watoto wako. Mama mmoja nchini Uingereza anayeitwa Susan anasimulia: “Niliolewa miezi 18 baada ya mume wangu wa kwanza kufa, na ilikuwa vigumu kwa wazazi wake kumkubali mume wangu wa pili. Mambo yalibadilika tulipoanza kushirikiana nao, tulipowaruhusu watoto wawapigie simu, na kuwashukuru kwa msaada wao.”

JARIBU KUFANYA HIVI: Fikiria mtu wa ukoo au rafiki ambaye hamna uhusiano mzuri, na mzungumzie jinsi ya kuboresha uhusiano huo pamoja na mwenzi wako.

Uhusiano na watu wengine unaweza kuleta matatizo katika familia yako ya kambo. Hata hivyo, ukifuata ushauri wa Biblia, wewe na familia yako mtapata baraka zinazoahidiwa katika Biblia: “Nyumba hujengwa kwa hekima, na kwa utambuzi itasimamishwa imara.”—Methali. 24:3.

^ fu. 3 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

^ fu. 4 Kwa habari zaidi kuhusu kukabiliana na matatizo mengine, ona mfululizo wa makala wenye kichwa “Jinsi Familia za Kambo Zinavyoweza Kufanikiwa,” katika gazeti la Amkeni! la Aprili 2012 lililochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 8 Bila shaka, ikiwa mwenzi wako wa zamani ni mkatili au anamtendea mtoto vibaya, huenda ukahitaji kuweka mipaka zaidi ili kulinda familia yako.

JIULIZE . . .

  • Ninawezaje kuwa na uhusiano mzuri na mwenzi wa zamani wa mke au mume wangu?

  • Tunawezaje kuwasaidia watu wa ukoo na marafiki wasivuruge familia yetu bila kukusudia?