Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 Habari Kuu: JE, MUNGU NI MKATILI?

Kwa Nini Watu Husema Mungu Ni Mkatili?

Kwa Nini Watu Husema Mungu Ni Mkatili?

JE, UNASHANGAZWA na swali lililo kwenye ukurasa wa kwanza wa gazeti hili? Watu fulani wanashangazwa nalo, lakini wengi wanajiuliza kama Mungu ni mkatili, au wanadhani ni mkatili. Kwa nini?

Watu fulani wanaopatwa na misiba ya asili huuliza: “Kwa nini Mungu anaruhusu mambo haya yatendeke? Je, kweli anajali? Au je, ni mkatili?”

Wengine hujiuliza swali hilo wanaposoma Biblia. Kwa mfano, wanaposoma simulizi la Gharika ya siku za Nao wanajiuliza, ‘Kwa nini Mungu mwenye upendo aliwaangamiza watu wengi hivyo? Je, ni mkatili?’

Je, umewahi kujiuliza maswali kama hayo? Au je, unashindwa kuwajibu watu wanaodhani Mungu ni mkatili? Vyovyote vile, acheni tuchunguze swali tofauti linaloweza kutusaidia.

KWA NINI TUNACHUKIA UKATILI?

Kwa ufupi, tunachukia ukatili kwa sababu tunaweza kutofautisha kati ya mema na mabaya. Kuhusu hilo, sisi ni tofauti sana na wanyama. Muumba wetu alituumba “kwa mfano wake.” (Mwanzo 1:27) Hilo linamaanisha nini? Alitupatia uwezo wa kuonyesha sifa na viwango vyake vya maadili, uwezo wa kutofautisha kati ya mema na mabaya. Fikiria hili: Ikiwa tulipokea uwezo wa kutofautisha mema na mabaya kutoka kwa Mungu na tuna mwelekeo wa kuchukia ukatili, je, hilo halionyeshi kwamba Mungu pia anauchukia?

Biblia inathibitisha ukweli huo, kwa kuwa katika Biblia, Mungu anatuhakikishia hivi: ‘Njia zangu ziko juu kuliko njia zenu, na mawazo yangu kuliko mawazo yenu.’ (Isaya 55:9) Kwa hiyo, tukisema Mungu ni mkatili, hilo litamaanisha kwamba njia zetu ziko juu kuliko zake. Lakini ni jambo la hekima kuchunguza zaidi kabla ya kuamua hivyo. Labda badala ya kuuliza kama Mungu ni mkatili, tunapaswa kuuliza kwa nini baadhi ya matendo yake yanaonekana kuwa ya kikatili? Ili tuelewe, acheni tuchunguze maana ya kuwa “mkatili.”

Tukisema mtu ni mkatili, tunamaanisha ana nia mbaya. Mtu mkatili hufurahia kuona watu wakiteseka au hajali wanapoteseka. Hivyo, baba anayemwadhibu mwanawe kwa sababu anafurahia kumuumiza hisia ni mkatili. Lakini baba anayemwadhibu mwanawe ili kumfundisha au kumlinda ana nia nzuri. Si rahisi kuelewa nia ya mtu, huenda hata wewe umewahi kudhaniwa una nia mbaya.

Acheni tuchunguze sababu mbili zinazofanya watu wafikiri Mungu ni mkatili. Kwanza, misiba ya asili tunayoona leo, na pili, hukumu za Mungu zilizoandikwa katika Biblia. Je, kweli mambo hayo yanaonyesha kwamba Mungu ni mkatili?